KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Friday, August 31, 2012

HALI YA BI KIDUDE INALETA MATUMAINI


HALI ya msanii mkongwe wa taarab nchini Fatma bint Baraka ‘Bi kidude’, inaendelea vizuri licha ya kulazwa tena hospitali Jumapili iliyopita, na taarifa zimeeleza kuwa, kuna uwezekano mkubwa akaruhusiwa leo.
Mwanzoni mwa mwezi huu, msanii huyo aliugua na vipimo vya kitabibu vilibaini kuwa, anasumbuliwa na ugonjwa wa kisukari, lakini kabla ya kulazwa majuzi, alikuwa akiuguzwa nyumbani kwa mwanawe Bububu meli nane.
Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu kutoka katika hospitali ya Zanzibar Medical Group iliyopo Shangani, Mkurugenzi wa kikundi cha Tausi Taarab, Maryam Hamdan, alisema hali ya Bi Kidude inaendelea vyema  tafauti na alivyokuwa wakati akipelekwa hospitalini hapo.
 Maryam, mtu wa karibu sana na Bi Kidude, amesema awali, hali ya msanii huyo ilikuwa hairidhishi kutokana na kuvimba miguu  pamoja na tumbo.
 “Alipofikishwa hapa hakuwa katika hali nzuri kwani sukari ilikuwa ikipanda na kushuka, lakini sasa tunashukuru ameanza kupata nafuu na kama hali itaendelea vizuri kama hivi, huenda kesho (leo), atapewa ruhusa”,
"Akipimwa sukari asubuhi inakutwa iko nane na ikifika saa kumi jioni hupanda hadi 29,  jambo linalotia wasiwasi kwamba kuna chakula anachokula mchana kina sukari", aliongeza Maryam.
Naye Juma Mohammed wa HABARI MAELEZO, anaripoti kuwa, wadau wa sanaa nchini wamewatupia lawama baadhi ya wasanii wa Zanzibar kwa kumtelekeza mwenzao huyo.
Mmoja wa watu wa familia ya Bi Kidude ambaye hakutaka kutajwa jina, amesema  tangu alipoanza kuugua, ni wasanii wachache mno  waliopita kwake angalau kumjulia hali licha ya kutolewa matangazo mbalimbali juu hali msanii huyo.
“Tunashangazwa sana na hawa wasanii wenzake, si wengi wanaokuja kumjulia hali… kwa namna anavyoishi nao kwa ukaribu na kupendwa na kila mmoja, hatukutarajia kama wangefanya hivi”, alilalamika mwanafamilia huyo.
Hivi karibuni, Makamu wa Kwanza wa Rais  Maalim Seif Sharif Hamad, alifanya ziara kwenda  kumjulia hali msanii huyo anayekisiwa kuwa na umri wa zaidi ya miaka 90, ambaye  ameitangaza sana Zanzibar kwa kuimba nyimbo mbalimbali mashuhuri zilizorekodiwa na magwiji kama Sitti Bint Sadi aliyekuwa akitamba kwa muziki wa taarab katika upwa wa Afrika Mashariki na nje.

No comments:

Post a Comment