KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Friday, December 26, 2014

FIVE STARS YAJA NA TATU MPYA, ISHA MASHAUZI APAKUA SURA SURAMBI




KIKUNDI cha taarab cha Five Stars, ambacho kimezidi kujiimarisha kwa kuwanyakua waimbaji wapya kadhaa, wiki iliyopita kiliingia studio kurekodi vibao vitatu vipya.

Vibao hivyo vipya ni Ubaya hauna soko kilichoimbwa na Mwanaidi Ramadhani, Kishtobe kilichoimbwa na Salha na Sina Gubu kilichoibwa na Mape Kibwana.

Kiongozi wa kundi hilo, Ally J, ametamba kuwa vibao hivyo vitakuwa moto wa kuotea mbali kutokana na kupigwa katika miondoko ya kisasa zaidi.

Wakati huo huo, kiongozi wa kundi la Mashauzi Classic, Isha Ramadhani, ameachia kibao kipya kinachokwenda kwa jina la Sura Surambi.

Kibao hicho ni utunzi na uimbaji wake Isha Mashauzi na tayari kimesharekodiwa wikiendi iliyopita kwenye studio za Sound Crafters, zilizoko Temeke jijini Dar es Salaam chini ya producer Enrico.

“Sura Surambi” inategemewa kuendelea kumweka juu Isha Mashauzi kwa namna alivyoimba wimbo huo na hapana shaka itatosha kabisa kuthibitisha ni kwanini alistahili tuzo ya mwimbaji bora wa kike wa taarab.

Gita la solo katika wimbo huo limepigwa na Ramadhani Kalenga, besi limepigwa na Rajabu Kondo wakati kinanda kimepapaswa na Kalikiti Moto.

MBILI MPYA ZA WAKALI WAO MODERN TARADANCE USIPIME



KUNDI la muziki wa taarab la Wakali Wao Modern Taradance limedhihirisha kuwa ni moto wa kuotea mbali katika taarab ya kisasa baada ya kuibuka na kibao kipya kinachokwenda kwa jina la Siioni thamani ya pendo.

Kibao hicho kilichotungwa na kuwekwa muziki na kiongozi wa kundi hilo, Thabiti Abdul, kimeimbwa na mwanadada Asia Mariam.

Kibao hicho na kile cha Mtu Mzima hovyo, vimerekodiwa katika studio za Marlon Linje, na vimekolezwa vikorombwezo vyenye mvuto wa aina yake.

Kibao cha Siioni Thamani ya Pendo kimepigwa katika miondoko ya taratibu, ni rhumba fulani lililokwenda shule huku ndani yake kukiwa kumechombezwa vitu fulani kutoka kwa baadhi ya nyimbo maarafu.

Kwa mfano, kipo kipande ambacho kimetoholewa kutoka kwenye wimbo wa Makumbele, uliotamba na bendi ya Orchestra Maquis Original ya hapa nchini zaidi ya miaka 15 iliyopita.

Aidha utakutana pia na vipande kutoka kwa wimbo unaendelea kulitingisha bara la Afrika “Kuchi Kuchi (Oh Baby)” ulioimbwa na J’odie wa Nigeria.

Vibao hivyo vimerekodiwa siku chache baada ya kundi hilo kuzindua albamu yao ya kwanza, inayojulikana kwa jina la Kalieni Viti siyo Umbea”.

OGOPA KOPA WAJA NA TATU KALI MPYA


KUNDI jipya la muziki wa taarab la Ogopa Kopa, linaloongozwa na Malkia wa muziki huo nchini, Khadija Omar Kopa, limedhihirisha kuwa ni tishio baada ya kuibuka na vibao vipya  vitatu.

Moja ya vibao hivyo vipya ni Stop Red Card, kilichoimbwa na Anifa Maulid, almaarufu kwa jina la Jike la Chui, mwanadada mwenye sauti murua inayoleta starahamu ya aina yake masikioni.

Kibao kingine ni Chozi la mnyonge, kilichoimbwa na kijana anayechipukia katika muziki huo, Hassan Ali, ambaye amejaliwa kuwa na sauti maridhawa.

Kiongozi wa kundi hilo, Khadija Omar Kopa, naye ameibuka na kibao kikali kinachotarajiwa kubeba jina la albamu mpya ya kundi hilo, Mama mukubwa.

MZEE YUSSUF AJA NA NGOMA MPYA 'MAHABA NIUE'


Huu ni wimbo mpya kabisa, umepewa jina la “Mahaba Niue” ikiwa ndio ‘singo’ mpya ya albam ijayo ya Jahazi Modern Taarab.

Ni utunzi na uimbaji wake Mfalme Mzee Yussuf, ngoma kali ambayo inakuwa zawadi nzuri ya kufungia mwaka 2014 na kufungua 2015.

Kazi hii imefanyika katika studio za Sound Crafters, Temeke jijini Dar es Salaam, chini ya producer Enrico. Ndani ya wimbo huu utakutana na mipini mikali ya Mohamed Mauji aliyetambaa vizuri na gitaa lake la solo huku kwenye kinanda kazi kubwa ikiwa imefanywa na Chid Boy.

Kama ilivyo kawaida ya Mzee Yussuf kwenye ngoma ambapo hufunika na vionjo vikali, humu nako ametisha sana, utakutana na vitu vya “Songa Ugali Tule” na vikorombwezo vingine kibao.

Je huu ndio wimbo wa mwisho wa Mzee Yussuf? Sahau kabisa hiyo kitu. Mzee Yussuf ameiambia Saluti5 kuwa lolote linaweza kutokea.

“Ningependa kuacha kuimba mwaka huu, lakini ni mapokeo ya kazi hii ndiyo yatakayoamua, nitaangalia mashabiki wanaipokea vipi, nitaangalia pia namna malengo yangu mengine yatakavyokuwa.

Ninatamani “Mahaba Niue” uwe wimbo wangu wa mwisho, lakini sisemi kuwa huu ni wimbo wangu wa mwisho,” alisema Mzee Yussuf katika maongezi yake na Saluti5

Monday, December 15, 2014

FIVE STARS MODERN TAARAB YAJA KIVINGINE, YAMNYAKUA SALHA, KUZINDUA ALBAMU MPYA DESEMBA 19 DAR

SALHA Aboud
MARYAM Aboud
MUSSA Kijoti
KIONGOZI wa Five Stars Modern Taarab, Ally J (kushoto)

MWIMBAJI nyota wa taarab nchini, Salha Abdul, amejiunga na kikundi cha taarab cha Five Stars kinachoongozwa na mpiga kinanda mahiri, Ally J.
Salha alitangaza uamuzi wake huo mwishoni mwa wiki kwa kile alichodai kuwa, umelenga zaidi kukuza kipaji chake.
Mwanadada huyo mwenye sura jamali na umbo lenye mvuto alisema amefikia uamuzi huo baada ya kushawishiwa kufanya hivyo na Ally J na pia baada ya kupata barakaa za mama yake mzazi.
"Nilipigiwa simu na Ally J akinieleza kwamba ana mazungumza na mimi na bila kusita nilimkubalia kwa sababu namheshimu sana,"alisema Salha, ambaye kabla ya kujiunga na Five Stars alikuwa kwenye kikundi cha Kings Modern Taarab.
Tayari Salma ameshaibuka na kibao kipya kinachokwenda kwa jina la Kishtobe, ambacho kimeshaanza kusikika kwenye vituo mbalimbali vya redio nchini.
Kwa mujibu wa Ally J, kikundi hicho kinatarajiwa kufanya uzinduzi wa albamu yake mpya Desemba 19 mwaka huu, utakaofanyika kwenye ukumbi wa Travertine, Dar es Salaam.
Ally J alisema kikundi chake kimeamua kutoka kivingine, ikiwa ni pamoja na kuboresha mipigo yake ya taarab kwa kuweka vionjo vipya kwa lengo la kuleta mvuto kwa mashabiki.
Aliwashukuru wadau mbalimbali wa taarab, ambao wameamua kukiongezea nguvu kikundi hicho ili kiweze kuwa tishio kama ilivyokuwa wakati kilipoanzishwa.
Five Stars ilipata pigo miaka miwili iliyopita baada ya wasanii wake 11 kufariki dunia katika ajali ya gari iliyotokea mkoani Morogoro.
All J alisema uzinduzi wa albamu ya kikundi hicho utapambwa na wasanii mbalimbali maarufu wa taarab nchini, wakiwemo wakongwe Khadija Omar Kopa, Mwanahawa Ally na Jokha Kassim.
Kwa upande wake, waimbaji Mussa Kijoti na Maryam Aboud walisema ujio wa albamu yao mpya utakuwa na kishindo kizito kwa vile wameamua kutoka kivingine.

Monday, November 10, 2014

TAARAB YA MIAKA MINNE YA UONGOZI WA DK. SHEIN Z'BAR

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar
Dk.Ali Mohamed Shein (wa pili kushoto) akiwa na Viongozi wengine katika  Tamasha maalum la taarab ya kusherehekea miaka minne ya ushindi wa CCM katika  Ukumbi wa Salama Hall Bwawani jana.[Picha na Ikulu.]
 Viongozi mbali mbali  waliohudhuria katika Tamasha maalum la taarab ya kusherehekea miaka minne ya ushindi wa CCM katika  Ukumbi wa Salama Hall Bwawani jana wakifuatilia kwa makini wakati
vikundi mbali mbali vikiburudisha .[Picha na Ikulu.] 
 Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein (kutoka kushoto) Mama Pili Balozi na Mama Asha Suleiman Iddi wake wa Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Iddi wakiwa katika Tamasha maalum la taarab ya kusherehekea miaka minne ya ushindi wa CCM katika  Ukumbi wa Salama Hall Bwawani jana wakifuatilia kwa makini wakati vikundi mbali mbali vikiburudisha .[Picha na Ikulu.]
 Mwimbaji wa kikundi cha Zanzibar One Rukia Moriss alipoburidisha kwa wimbo “Achekwe hana stara”wakati wakati wa Tamasha maalum la taarab ya kusherehekea miaka minne ya ushindi wa CCM na kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein, katika  Ukumbi wa Salama Hall Bwawani jana [Picha na Ikulu.]
 Kikundi cha Taifa cha Muziki wa Taarab cha Culture musical Club kilipotumbuiza wakati wa Tamasha maalum la taarab ya kusherehekea miaka minne  ya ushindi wa CCM na kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein, katika  Ukumbi wa Salama Hall Bwawani jana [Picha na Ikulu.]
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai wakiteta jambo wakati wa Tamasha maalum la taarab ya kusherehekea miaka minne ya ushindi wa CCM katika  Ukumbi wa Salama Hall Bwawani jana wakifuatilia kwa makini wakati vikundi mbali mbali vikiburudisha .[Picha na Ikulu.]

Waimbaji wa Kikundi cha Zanzibar Modern Taarab Khadija Khamis na Marium Juma wakiimba wimbo wa  Pika Dk.Shein BigUp wakati wa Tamasha maalum la taarab ya kusherehekea miaka minne (4) ya ushindi wa CCM na kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein, katika  Ukumbi wa Salama Hall Bwawani jana [Picha na Ikulu.]

Sunday, October 12, 2014

MWANAHAWA ALLY AMBWAGA KHADIJA KOPA KATIKA NANI MKALI WA RUSHA ROHO


 Mwanahawa Ally, mwimbaji mkongwe  ameshika nafasi ya kwanza
 Khadija Kopa, mwimbaji wa TOT ameshika nafasi ya pili
 Khadija Yussuf, mwimbaji wa Jahazi ameshika nafasi ya tatu
LEILA Rashid, mwimbaji wa Jahazi ameshika nafasi ya nne
Isha Mashauzi, kiongozi na mwimbaji wa Mashauzi Classic ameshika mkia

MWIMBAJI mkongwe wa muziki wa taarab nchini, Mwanahawa Ally ameibuka mshindi katika shindano la kumsaka mwimbaji bora wa muziki huo.

Mwanahawa, ambaye amewahi kuimbia vikundi mbalimbali vya taarab nchini, aliibuka kidedea baada ya kuwabwaga waimbaji wengine wanne.

Shindano hilo liliandaliwa na blogu ya Rusha Roho, ambayo ni mahsusi kwa ajili ya kuandika habari na  makala za wasanii wa muziki wa taarabu.

Katika shindano hilo, Mwanahawa alipata kura sita, ambazo zimepigwa na wasomaji wa blogu hiyo, zikiwa sawa na asilimia 50 ya kura zilizopigwa.

Mwimbaji mwingine mkongwe wa muziki huo, Khadija Kopa alishika nafasi ya pili kwa kupata kura tano, ambazo ni sawa na asilimia 41.

Khadija Yussuf alishika nafasi ya tatu kwa kupata kura nne, ambazo ni sawa na asilimia 33, akifuatiwa na Leila Rashid, aliyepata kura tatu, ambazo ni sawa na asilimia 25. Isha Mashauzi alishika mkia kwa kupata kura mbili, sawa na asilimia 16.

Blogu ya Rusha Roho inawashukuru wale wote walioshiriki kupiga kura za kumtafuta msanii bora wa taarab kati ya wasanii hao watatu.
  KHADIJA KOPA   5 (41%)
  LEILA RASHID   3 (25%)
  ISHA MASHAUZI   2 (16%)
  KHADIJA YUSUF   4 (33%)
  MWANAHAWA ALLY   6 (50%)

Wednesday, October 1, 2014

MBILI MPYA ZA ISHA MASHAUZI USIPIME






MWIMBAJI nyota wa muziki wa taarab na kiongozi wa kundi la Mashauzi Classic, Isha Ramadhani, ameibuka na kibao kingine kipya kinachokwenda kwa jina la Mapenzi hayana dalali.

Kibao hicho ni mwendelezo wa nyimbo mpya za Isha, ambaye kwa sasa anatamba na kibao chake kipya cha Nimlaumu nani, ambacho amekiimba kwa miondoko ya rhumba, akiimba sauti zote.

HII NI NGOMA MPYA YA AZIA MZINGA WA MASHAUZI CLASSIC



'Wema Hauozi Ubaya Haulipizwi' - Asia Mzinga ndani ya Mashauzi Classic

Wednesday, September 24, 2014

HIVI NDIVYO VIBAO VIPYA VINAVYOTAMBA MITAANI HIVI SASA


                                                      Hammer Q - Kibakuli

                                          Sina Makuu - Ashura Machupa - G5 Modern Taarab...

                                         Hassan Voucher Ft Hasna - Sindano na Golkeeper

                                        Mtu Mzima hovyooo- Wakali wao Modern Taradance

ABDUL MISAMBANO AFUFUKA, AJA NA MPYA ISEMAYO 'SI MIE NI MOYO'




Msanii mkongwe katika muziki wa miondoko ya taarabu nchini,  Abdul Misambano, ameibuka na kibao kipya kinachokwenda kwa jina la 'Si mie ni moyo'.

Hii ni mara ya kwanza kwa Misambano kutoa kibao kipya baada ya kuwa kimya kwa miaka kadhaa.

Msanii huyo aliyewahi kung'ara katika kikundi cha Tanzania One Theatre (TOT Plus), alisema hivi karibuni kuwa, alifanikiwa kurekodi kibao hicho hivi karibuni baada ya kukifanyia mazoezi kwa wiki
kadhaa.

Misambano amesema katika kibao hicho, kinanda kimepigwa kwa umaridadi mkubwa na mkali wa kupapasa ala hiyo, Omary Kisira.

Kwa wanaomkumbuka Misambano, alijipatia umaarufu mkubwa kupitia kibao chake cha Asu kilichotamba miaka ya 1990.

ISHA MASHAUZI AACHIA RHUMBA NZITO, AMEIMBA PEKE YAKE MWANZO MWISHO



NYOTA wa miondoko ya taarab, Isha Ramadhani 'Mashauzi' amekuja kivingine
ambapo ameachia rhumba kali la miondoko ya muziki wa dansi.
Ngoma hiyo inakwenda kwa jina la 'Nimlaumu Nani'.

Ni wimbo wa dakika tano uliorekodiwa katika studio ya Soft Records
chini ya producer Pitchou Meshaa.

Sauti zote utakazozisikia katika wimbo huu, zimewekwa na Isha Mashauzi mwenyenye – ameimba
peke yake mwanzo mwisho.

Sunday, July 20, 2014

MASHAUZI CLASSIC KUZINDUA ALBAMU MPYA IDDI MOSI



KIKUNDI cha Taarab cha Mashauzi Classic, chini ya uongozi wake Isha Mashauzi, siku ya Idd Mosi kitafanya onyesho la uzinduzi wa albamu yake mpya ya 'Asiyekujua hakuthamini.'

Onyesho hilo litakaloanza saa tatu usiku, limepangwa kufanyika kwenye ukumbi wa Buzuruga Plaza na kiingilio kitakuwa sh. 10,000 kwa mtu mmoja.

Katika onyesho hilo, kutakuwepo  wasanii machachari wenye sauti za kuvutia kama vile Isha Mashauzi (mkurugenzi), Hashim Said,  Thania Msomali, Saida Ramadhani na Zubeidah Andunje.

DAR MODERN TAARAB KUZINDUA ALBAMU YAKE MPYA IDDI MOSI


Kundi zima la Dar Modern Taarab limeachia Albam yake mpya kabisa inayokwenda kwa jina la "Ubinadamu kazi."

Uzinduzi wa albam hii utafanyika siku ya Idd Mosi pale kwenye ukumbi wa Travertine, Magomeni, Dar es Salaam.

WAIMBAJI WAWILI WASIMAMISHWA KAZI MASHAUZI CLASSIC


KIKUNDI cha muziki wa taarab cha Mashauzi Classic chenye maskani yake mjini Dar es Salaam, kimewasimamisha wasanii wake wawili kwa tuhuma za utovu wa nidhamu.

Taarifa za uhakika kutoka ndani ya kundi hilo zimeeleza kuwa, wasanii waliosimamishwa ni Thania Msomali na Fatma Seif.

Fatma amewahi kuimba nyimbo iitwayo 'Mdomo wako utakuponza' uliomo kwenye albami ya 'Si bure una mapunngufu'.

Kwa mujibu wa habari hizo, kisa cha Fatma kusimamishwa ni kutohudhuria onyesho la kundi hilo na kudaiwa kuonekana katika kundi lingine la muziki huo la Gusagusa siku hiyo.

Alipoulizwa kuhusu adhabu hiyo, Fatma alisema: “Mimi siku hiyo sikwenda kazini kwa sababu nilikuwa naumwa. Kiongozi wangu alinipigia simu kuniambia nihudhurie kwenye onyesho nikamwambia siwezi kwa sababu naumwa."

"Akaniacha, siku ya pili yake akanipigia simu tena kuniulizia hali yangu, nikamwambia bado nipo nyumbani tu, lakini cha kushangaza akanitumia ujumbe wa kunisimamisha kazi miezi mitatu. Kesho yake akanitumia ujumbe tena kuwa nimeachishwa kabisa kazi, hivyo niko huru kutafuta bendi yoyote, kwa kweli imeniuma sana maana sijui kama ndo hili tatizo la mimi kuugua,"alisema.

Alipoulizwa kuhusu uamuzi aliochukua, Fatma alisema: "Sijachukua uamuzi wowote na hivi sasa nipo tu nyumbani, bado akili yangu haijatulia, hivyo sijajua kitu cha kufanya, acha kwanza nitulie."

Kwa upande wake, akizungumzia adhabu hiyo, Thonia alisema:  “Mimi nilikuwa naumwa na nilitoa taarifa kwa uongozi, nimeenda hospitali kufanyiwa uchunguzi, nikaonekana (akataja ugonjwa), hivyo nikaandikiwa dawa ambazo niliendelea kuzitumia."

"Baada ya kama wiki mbili, nikawa najisikia vizuri na nikaamua kwenda kuripoti kazini, lakini cha kushangaza kidogo nikaambiwa niendelee kupumzika kwanza mpaka nipone ndo niende. Nimekaa nyumbani tena baada ya siku kadhaa, Mashauzi walikuwa wanapiga Mango Garden, nikaomba tena nihudhurie kazini, lakini nikaambiwa nisubiri tu ila nikaomba basi niende kuangalia onyesho nikaruhusiwa ila sikuimba,"alisema.

"Sasa kinachoniweka njia panda ni kuwa, hali yangu ni nzuri, nimeimarika ki-afya na nina hamu ya kuimba ila nikiuelezea uongozi wangu kuwa nataka kuripoti kazini, wanasema nisubiri tu sasa nitasubiri hadi lini!? Kwa kweli sijajua muafaka upo wapi na hatma yangu sijajua maana naendelea kusubiri tu na wala sijaelezwa kitu,” alisema.

Kiongozi wa wasanii katika kundi la Mashauzi Classic, Hashim Said alisema: "Fatma tulimuondoa katika bendi kwa utovu wa nidhamu. Alitega kuja kazini kwa kisingizio cha kuumwa.
Yote hayo yametokana na siku hiyo ilikuwa ni Alhamisi na bendi tuliigawa mara mbili, baadhi walikwenda Mwanza kikazi na baadhi wakabaki DSM. Waliokwenda Mwanza waliambatana na Mkurugenzi, waliobaki Dsm walibaki na mimi pale Mango Garden kikazi akiwemo Fatma."

"Lakini cha kushangaza, Fatma alinitumia ujumbe muda wa saa moja usiku akidai anaumwa! Nikamuuliza huu ugonjwa umeanza saa hizi kwa kuwa ni muda wa kuja kazini? Nikamwambia lazima aje kazini sababu waimbaji waliokuwapo ni wachache,"alisema.

"Kinachoonekana ni kuwa Fatma alimaindi suala la yeye kubakishwa Dsm! La kushangaza zaidi kazini hakuja na akaonekana huko Mbagala akiwa na bendi hizi za mitaan akiimba, hapo ndipo nilipomsimamisha kazi. Kibaya zaidi alishindwa kuomba msamaha. Uongozi ukaamua kumuondoa katika bendi sababu hatuwezi kuwa na msanii asiyekuwa na uzalendo na bendi yake,"alisema.

"Thania naye tumemsimamisha kutokana na kiwango chake kila kukicha kinashuka na tumempa nafasi ya kufanya mazoezi zaidi ili akiwa vizuri basi atarudi kazini, "aliongeza.

JAHAZI YAFUNIKA UZINDUZI WA ALBAMU YA CHOZI LA MAMA


Mzee Yusuf akisalimia mashabiki kabla ya kuanza kwa onyesho


Mzee Yusuf (kulia) akiongea jambo kabla ya uzinduzi wa "Chozi la Mama". Katikati ni Aisha Abushily 'Mama wa madikodiko' kutoka Kenya.

Meneja wa Jahazi Modern Taarab, Mohammed Rashid Mauji 'Father Mauji' pamoja na shabiki wa Jahazi wakizindua albamu mpya iitwayo "Chozi la Mama" ndani ya ukumbi wa Dar Live.

KIKUNDI cha muziki wa taarab cha Jahazi hivi karibuni kilifunika katika uzinduzi wa albamu yake mpya inayokwenda kwa jina la Chozi la Mama.

Uzinduzi wa albamu hiyo ulifanyika kwenye ukumbi wa Dar Live ulioko Mbagala, Dar es Salaam na kuhudhuriwa na mashabiki lukuki.

Kama ilivyo kawaida, wimbo uliobeba jina la albamu hiyo uliimbwa na Mzee Yusuph, ambaye pia aling'ara katika kikao cha Wasiwasi wako.

Monday, May 26, 2014

DK SHEIN AKICHANGIA KIKUNDI CHA ZANZIBAR MODERN TAARAB SH. MILIONI NANE

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la  Mapinduzi Dkt.Ali Mohamed Shein akipokea album mbili za nyimbo kutoka kwa Mkurugenzi wa kikundi cha muziki wa taarab cha  Zanzibar Modern Taarab, Abdalla Ali, alipokuwa akiwa mgeni rasmi katika sherehe za kikundi hicho kutimiza miaka saba tangu
kuanzishwa kwake. Katika sherehe hiyo, Rais alikichangia kikundi hicho shillingi za kitanzania milioni nane. Hafla hiyo ilifanyika katika ukumbi wa Salama wa Hoteli ya Bwawani, Zanzibar.[Picha na Ramdhan Othman,Ikulu.]

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt.Ali Mohamed Shein (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wasanii wa kikundi cha muziki wa taarab cha Zanzibar Modern Taarab, alipokuwa mgeni rasmi katika sherehe za kikundi hicho kutimiza miaka saba tangu kuanzishwa kwake. [Picha na Ramdhan Othman,Ikulu.]

Monday, May 19, 2014

BURIANI JUMA BHALO, GWIJI WA TAARAB ASILIA



Na John Kitime

Mfalme wa Taarab nchini Kenya ambaye pia amejijengea jina katika nchi za Afrika Mashariki, Mohamed Khamis Juma Bhalo, amefariki dunia. Bhalo amefariki dunia usiku wa Jumamosi akiwa nyumbani kwake eneo la mji wa zamani Mombasa, baada ya kuugua kwa muda mrefu.

Juma Bhalo  alizaliwa 1942 huko  Shela katika wilaya ya Malindi. Mwaka1954, alijiunga na shule ya msingi ya Sir Ali bin Salim , wakati huohuo familia yake ilihakikisha anahudhuria Madrassa ili kupata elimu ya dini.

Bhallo mwenyewe aliwahi kusema hamu yake ya kuimba ilimuanza katika wakati huu na sauti yake kuwa na mvuto kutoka kipindi hiki alipokuwa Madrassa Akiwa na miaka 9 tayari muda wake mwingi ulitumika kusikiliza santuri, na akili yake ilianza kupenda sana muziki.

Hakumaliza elimu ya msingi kwa kuwa wazazi wake walishindwa kulipa ada ya shule. Mwaka 1957 alihamia Mombasa na kupata kazi Forodhani, akiwa Mombasa alianza kukutana na kushirikiana na wanamuziki wa Taarab wa Mombasa.

Hakuipenda sana kazi ya Forodha hivyo 1959 akahamia Tanga kwa mjomba wake, na hapo akajiunga na kundi maarufu la Taarab wakati ule lililoitwa Young Noverty, hapa alipata ujuzi mkubwa wa muziki wa Taarab.

Alirudi kwao Malindi kwa muda mfupi na hatimae kurudi tena Tanga 1962 na kujiunga na kundi la Young Stars Taarab.

Mwaka 1966 alirudi Mombasa na kuanzisha kundi la Bhalo and Party, kundi ambalo amedumu nalo mpaka Mauti yake.

Mwaka 2007 baada ya zaidi ya miaka 50 ya kuwemo katika muziki wa Taarab, Juma Bhalo ambaye wapenzi wake walimuita Profesa na hata Mfalme wa Taarab alitangaza kuacha kufanya maonyesho ya wazi ya taarab, alitangaza hilo siku alipopiga katika harusi ya mwanae.
Alistaafu kazi hiyo kwa maneno yafuatayo: 

"Waswahili wasema kiwate kitu kabla hakijakuata. Kwa hivyo kama mulivyo nishuhudiya usiku huu nlivyowatumbuiza ambavyo ni kama kawaida yangu basi leo hii usiku huu kabla hawajaja watu wakasema ahhhhh Bhalo ashazeeka hawezi tena kuimba kwa hivyo najiuzulu ningali bado niko fiti. Kwa hivyo siimbi tena hadharani kikazi. Nawashkuru kwa ushabik wenu na musijali Mungu akiniwezesha Kasseti mpya ntawatoleya".

Taarab yake iliegemea sana muziki wa kihindi na hivyo kuwa tofauti na taarab nyingine

MUNGU AMLAZE PEMA PROFESA

Monday, May 5, 2014

KUMBUKUMBU YA MAREHEMU MOHAMED SLEYUM ZAHOR



SLEYUM MOHAMED ZAHOR (1922-2003)
HATIMAYE leo umetimiza miaka 11 tangu ulipofariki dunia mwaka 2003
baada ya kuugua kwa muda mrefu na kuzikwa katika makaburi ya Kigilagila,
Kiwalani, Dar es Salaam.
Kifo chako kimetuachia pengo na upweke mkubwa. Tunazikosa simulizi zako, maono yako, ucheshi wako, busara zako na hekima zako.
Unakumbukwa
sana na mke, Bibi Fatuma Rashid na watoto wako, Rashid, Pili, Amisa,
Shani, Asha, Saumu, Nuru na Hilali pamoja na wajukuu zako wote.
Hakika
sisi zote ni waja wa Mwenyezi Mungu na kwake lazima tutarejea.
Tunaamini maandiko ya kwamba kila chenye roho, lazima kitaonja mauti.
Mungu ailaze roho yako mahali pema, peponi. Amin

Monday, April 21, 2014

ASIA IDAROUS: MUZIKI WA MWAMBAO ASILIA UNA MGUSO WAKE


Na Andrew Chale
MWANAMITINDO mkongwe na mdau wa muziki wa mwambao asilia, Asia Idarous Khamsin, amesema muziki huo una mguso wake hivyo jamii inatakiwa kuupokea na kuuenzi.Asia ambaye pia ni Mkurugenzi wa Fabak Fashions, alisema hayo usiku wa April 19, wakati wa onesho maalumu la Usiku wa Mwambao Asilia, ambalo pia lilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU, sasa AU), Dk. Salim Ahmed Salim, aliyekuwa mgeni rasmi akiungana na wadau wengine katika kuenzi muziki huo ndani ya ukumbi wa Travertine, Magomeni jijini Dar es Salaam.Asia alisema katika kuenzi muziki huo ni pamoja na kuwakumbuka wanamuziki wakongwe walioufikisha hapo ulipo.“Baadhi ya nyimbo za mwambao asilia unapozisikiliza zinagusa moja kwa moja, na ujumbe wake hufika kwa haraka,” alisema Asia.Katika onesho hilo, Asia alidhihirisha umahiri wake na kuimba kibao cha ‘Raha ya Moyo Wangu’.Bendi za Dar Modern Taarab na Nadd Ikhwan (Malindi), zilikonga nyoyo wadau wa miondoko hiyo waliofurika ndani ya ukumbi huo huku wakipata pia wasaha wa kupita kwenye zuria jekundu na kupiga picha za ukumbusho, ambapo awali kwenye miondoko ya taarab hapa nchini haikuwa na utamaduni huo wa red carpert.Onesho hilo lilidhaminiwa na Times FM, Fabak Fashions na www.nakshi255.com  na wengine wengi wakiwemo mashughuli blog, Michuzi blog, Vijimambo blog simu tv na wengine wengi

Tuesday, April 1, 2014

SUNGURA MJANJA WA MASHAUZI ATOA KITU KIPYA


MWIMBAJI chipukizi wa tarab anayeinukia vizuri nchini, Saida Ramadhani ‘Sungura Mjanja’, ameibuka na wimbo mpya uitwao Ropokeni Yanayowahusu.

Akizungumza na BIN ZUBEIRY jioni hii katika hoteli ya Double Tree, Masaki, Dar es Salaam, mwimbaji huyo wa kundi la Mashauzi amesema wimbo huo ametungiwa na dada yake, Isha Ramadhani.
“Dada Isha katunga, mimi nimerekodi na umekwishakamilika, ni wimbo mzuri sana, naamini utapendwa ukitoka. Na utazidi kunipandisha matawi ya juu,”alisema Saida.
Saida ameingia kwenye kinyang’anyiro cha tuzo za Kili mwaka huu kupitia wimbo wa Asiyekujua Hakuthamini, ambao ameshirikiana na dada yake, Isha ulioingia kwenye kipengele cha wimbo bora wa Taarab.

ISHA MASHAUZI AIBUKA NA SURA SIYO ROHO



MWANAMUZIKI na kiongozi wa kundi la taarab la Mashauzi Classic, Isha Mashauzi, ametoa nyimbo mpya mbili, ambazo muda si mrefu zitaanza kusikika kwenye vituo mbalimbali vya Redio nchini.
Akizungumza na BIN ZUBEIRY jioni hii katika hoteli ya Double Tree, Masaki, Dar es Salaam wakati wa semina ya wanamuziki waliongia kwenye tuzo za Kili 2014, Isha au Jike la Simba amesema kwamba nyimbo zote ni nzuri.
Amezitaja nyimbo hizo kuwa ni Sura Siyo Roho na Mapenzi Hayana Dhamana, ambazo zote ametunga yeye mwenyewe.
“Kama kawaida, wapenzi na mashabiki wangu na mashabiki wa Mashauzi Classic kwa ujumla, wajiandae kwa kazi mpya, tutaanza na audio (sauti) baadaye itafuatia na kwenye video pia,”alisema Isha.

FATIHYA AKIWA NDANI YA MAONYESHO YA BIASHARA COCO BEACH



MFANYABIASHARA Fatihya Masoud (kushoto) akifurahia jambo wakati akimueleza mteja, Farida Shekigenda, bei ya mabegi alipotembelea banda lake juzi kwenye maonyesho ya biashara ya Kariakoo yanayofanyika kwenye ufukwe wa Coco Beach kwa udhamini wa Kampuni ya Simu ya Tigo.

MFANYABIASHARA Fatihya Masoud (kushoto) akimueleza mteja, Farida Shekigenda, bei ya mabegi alipotembelea banda lake juzi kwenye maonyesho ya biashara ya Kariakoo yanayofanyika kwenye ufukwe wa Coco Beach kwa udhamini wa Kampuni ya Simu ya Tigo.

MFANYABIASHARA Fatihya Masoud akifurahia vipodozi vyake wakati wa maonyesho hayo

Sunday, March 9, 2014

UZINDUZI ALBAMU YA NYONGA MKALIA INI WAFANA


 
 

Moja ya sehemu ambayo unaweza kumtambua msanii mzuri ni pale ambapo anaweza kuimba na kucheza na mashabiki wake wanaokuja kila mara kumuangalia kwenye shoo na matamasha tofauti.

Hassan Ally alidhihirisha uzuri na umahiri wake ambao haupo tu kwenye kuimba na kutunga mashairi lakini pia kutawala jukwaa na kucheza na mashabiki wake.

Kwa wale ambao hawakufika kwenye shoo ya jana kwa sababu tofauti tofauti nakushauri ukisikia huyu jamaa anafanya shoo nyingine,nenda ukahudhurie.

Kila shoo nzuri hupambwa na muunganiko wa maelewano na sapoti baina ya wasanii,na jana Kings Modern Taarab walifanya vizuri sana kwenye kumuunga mkono mwenzao.

Walitoa burudani nzuri sana iliyowafanya mashabiki waliofika watulie huku wakisubiri Hassan Ally.Baadhi ya wasanii kutoka Kings ambao walitoa burudani ni pamoja na Amina Mnyalu,Aysher Vuvuzela,Mwanahawa Chipolopolo.

Ingawa shoo ilichelewa sana kuanza ilia baada Kings walipoanza kazi mambo yalikuwa poa,Baada ya nyimbo kadhaa za Kings ndipo Joha Kassim akapanda stejini nae akatoa shoo kali kama kawaida yake.

Ndio Hassan Ally aliingia ukumbini kwa kuwasuprise mashabiki wake kupitia geti ambalo mara kwa mara huwa linafungwa huku akisindikizwa na ngoma.

Moja ya vitu ambavyo wengi walivipenda na kumshangilia sana ni kuwashukuru watu ambao walifanikisha shoo hiyo,huku akionyesha furaha yake na upendo kwa wote waliohudhuria.

Hassana Ally alijipanga sana kiasi cha kujua afanye nini na wakati gani,sio tu katika uimbaji lakini kucheza na vijana walioandalia kufanya kazi hiyo.

Kuna muda alishuka chini ya steji na kuanza kucheza na mashabiki wake kitu kilichowafanya wengi kuancha kucheza na kumuangalia jinsi walivyokuwa wanacheza vizuri sana tena kwa umoja wao.

“Wengi hawajui kuwa mimi nina mtoto,sasa leo nataka mumuone mwanamke niliyezaa naye” Hayo yalikuwa maneno na Hassan Ally ambapo alimuita ‘Nyonga mkalia Ini’ wake,ndio zipotoka shangwe kutoka kwa mashabiki.

Kabla ya Khadija Kopa Hajapanda stejini,Hassan Ally aliimba nyimbo “Nyonga Mkalia Ini” na Mr. Pendwa Pendwa. Lady with Confidence ilikuwa ni nyimbo moja wapo ambayo Malkia aliimba.

Ingawa Bi.Mwanahawa Ally na Mc Dida hawakuwepo,lakini shoo ilikuwa nzuri na ilipangilia sana kiasi cha kufanya watu kutowaulizia hao ambao hawakuwepo. Mwanahawa Chipolopolo alichukua jukumu la U-Mc na kwa maoni yangu aliufanyia haki sana,pia watangazaji Yunis Kanumba wa City Radio na Mwanne wa Eatv walitoa sapoti pia.

IMETOLEWA BLOGU YA NAKSHI 255