KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Friday, December 28, 2012

JAHAZI YAPAGAWISHA MASHABIKI USIKU WA DAR LIVE


Mzee Yusuf akiongea na mashabiki wake.
Bi. Leila Rashid akiendeleza makamuzi.
...Khadija Yusuf kazini.
Mwimbaji wa Jahazi Modern Taarab, Fatma Mahmoud 'Mcharuko' akiwapa raha mashabiki.

Sehemu ya nyomi iliyotia timu mahali hapo.
Wapenzi wa taarab wakijiachia kwa raha zao na Jahazi.
Mzee Yusuf akizidi kukoleza burudani ndani ya Dar Live.

Thursday, December 27, 2012

KHADIJA KOPA APAGAWISHA MASHABIKI KIVULE




Na Peter Mwenda
MALKIA wa Mipasho nchini, Khadija Kopa na kundi lake cha Tanzania One Theatre (TOT)leo kitatoa shoo kabambe kusherekea sikukuu ya Krismas kwa wakazi wa Kata ya Kivule, Ilala kusherekea sikukuu ya Krismas kwenye ukumbi wa Vegetable Garden Pub.
Akizungumza jana, Kopa alisema kikundi hicho ambacho kitamba na nyimbo kemkem za taarab zinazotingisha katika miundoko ya Pwani ukiwemo Full Stop, Stop in Town na Mjini Chuo Kikuu ameahidi kukonga nyoyo za mashabiki wake katika eneo hilo kwenye sikukuu hiyo.
Alisema TOT taarab imesheheni kila idara ikiwa na wanamuziki wenye uwezo mkubwa wa kupiga taarab yenye mahadhi yanayokubalika akiwepo mkongwe Abdul Misambano, Mwanamtama Amir, Ali Star, Rukia Juma na Kopa Junior anayeimba nyimbo za Omar Kopa.
Mkurugenzi wa Vegetable Garden Pub, Anicety Mkwaya alisema maandalizi ya burudani hiyo imekamilika na zawadi zitatolewa kwa wale watakacheza taarab vizuri na watakaovaa vizuri.
Alisema burudani katika ukumbi huo zinaendelea ambako Januari 29 bendi ya Msondo Ngoma itatoa burudami katika ukumbi huo

Friday, December 21, 2012

ALBAMU MPYA YA JAHAZI KUZINDULIWA DESEMBA 30



KIKUNDI cha taarab cha Jahazi kinatarajia kupakua albamu mpya ya Wasiwasi wako katika onyesho litakalofanyika Desemba 30 mwaka huu kwenye ukumbi wa Travertine, Magomeni, Dar es Salaam.
Akizungumza na blogu ya rusha roho leo, kiongozi wa kundi hilo, Mzee Yusuph amesema maandalizi yote muhimu kwa ajili ya uzinduzi huo yameshakamilika.
Kwa mujibu wa Mzee, albamu hiyo itakuwa na nyimbo sita, ambazo amejigamba kuwa zote zitakuwa moto wa kuotea mbali.
Mzee alisema tayari nyimbo zote sita zimeshakamilisha na baadhi zimeshaanza kupigwa na kusikika kwenye vituo mbalimbali vya redio na televisheni nchini.
Alizitaja nyimbo hizo kuwa ni Wasiwasi wako aliouimba yeye mwenyewe, Kazi mnayo ulioimbwa na Ahmed Ally  na Sitaki Shari ulioimbwa na mahabuba wake, Leila Rashid.
Alizitaja nyimbo nyingine kuwa ni Nipe Stara ulioimbwa na Rahma Machuppa, Hata bado hamjanuna ulioimbwa na Fatma Ally na Mambo bado ulioimbwa na Khadija Yussuf.
Mzee alisema amepania kufanya mabadiliko makubwa kwenye muziki wa taarab ili kuwapa mashabiki ladha tofauti badala ya ile waliyoizoea.
"Sisi kama Jahazi tunapenda tufanye kile kitu mashabiki wanapenda, hivyo tunawaahidi mambo mapya kabisa katika albamu yetu hii mpya,"alisema.
Alisema wakati wa onyesho hilo, wanatarajia kuuza CD na DVD za albamu hiyo kwa mashabiki ili wakapate starehe zaidi majumbani kwao.
Albamu hiyo itakuwa ya tisa tangu kundi la Jahazi lilipoanzishwa mwaka 2006. Albamu zingine zilizopita za kundi hilo ni Tupendane wabaya waulizane, Wagombanao ndio wapatanao, Mpenzi chokolate, Daktari wa mapenzi, Two in one, VIP na My Valentine.

Monday, December 17, 2012

THABITI ABDUL AJA NA HABIBI



HUWEZI kuamini, lakini ndivyo ilivyo. Baada ya kutamba katika utunzi na upapasaji kinanda kwenye nyimbo nyingi za taarab, hatimaye mwanamuziki Thabiti Abdul ameamua kujitosa kwenye uimbaji.
Mwanamuziki huyo, ambaye pia ni mahiri katika muziki wa dansi, ameibuka na kibao kipya kinachokwenda kwa jina la Habibi.
Thabiti ameimba kibao hicho kwa kushirikiana na baadhi ya wasanii wa kundi la Mashauzi Classic, ambalo yeye ni miongoni mwa wakurugenzi wake.
Mpiga kinanda huyo amekiimba kibao hicho kwa umahiri mkubwa, akimlalamikia kimwana, ambaye amekuwa akimtesa kimapenzi.
Wakati Thabiti akijitosa kwenye uimbaji taarab, mwimbaji mkongwe wa fani hiyo, Ally Hemed Star ameibuka na kibao kipya kinachokwenda kwa jina la Ni wewe.
Hii ni mara ya kwanza kwa Ally Star kuibuka na kibao cha taarab baada ya kuwa kimya kwa takriban miaka miwili.

MASIKINI KHADIJA YUSSUF, AANGUA KILIO CHA UCHUNGU. KISA? WIFIYE LEILA RASHID!


MWIMBAJI nyota wa taarab wa kikundi cha Jahazi, Khadija Yussuf mwishoni mwa wiki iliyopita aliangua kilio wakati alipokuwa akihojiwa katika kipindi cha Mitikisiko ya Pwani kilichorushwa hewani
na kituo cha ITV.
Sababu kubwa iliyomfanya Khadija aangue kilio ni kuzuka kwa tofauti kubwa kati yake na kaka yake, Mzee Yussuf, ambaye ndiye mkurugenzi wa kikundi hicho.
Mtangazaji wa kipindi hicho alimuuliza Khadija ni kitu kipi kinachomkera katika maisha yake. Naye bila kutafakari kwa muda mrefu alijibu kuwa, ni kile kitendo cha mtu kutoka aendako na kwenda kumzushia maneno ya uongo kwa Mzee.
"Kinachoniuma zaidi ni kwamba afadhali hayo maneno ningekuwa nimeyasema, lakini sijafanya hivyo.
Hawa watu wanapaswa kutambua kwamba kuna Mungu na mimi na Mzee Yussuf tumezaliwa baba mmoja mama mmoja, atakapozikwa Mzee Yussuf ndipo nitakapozikwa mimi,"alisema Khadija huku machozi yakianza kumlengalenga.
"Kusema kweli maisha ninayoishi na Mzee Yussuf hivi sasa ni tofauti na huko nyuma tulikotoka. Inaniuma sana,"alisema Khadija na kuangua kilio kikali, ambacho kilisababisha mtangazaji wa kipindi hicho naye machozi kumlenga.
Mapema Khadija alisema kuna kikundi cha watu ndani ya Jahazi, ambacho kimekuwa kikimchonganisha yeye na wifi yake, Leila Rashid, ambaye ni mke wa pili wa Mzee.
Alisema watu hao wamekuwa wakipeleka maneno ya umbeya kwa Leila wakidai kuwa yeye ndiye ameyasema na vivyo hivyo wamekuwa wakija kwake na kumweleza maneno kama hayo.
"Kuna wakati Leila amekuwa akinitumia meseji zenye maneno machafu. Ninapomjibu anakasirika. Sielewi tunachogombea ni kipi,"alisema Khadija.
"Binafsi sina tatizo na Leila na sioni kwa nini tugombane. Sielewi na ninashangaa. Lakini hii yote ni kwa sababu kuna watu ndani ya Jahazi wanaotuchonganisha kwa makusudi,"aliongeza.
Khadija alisema kwa sasa anajiandaa kuibuka na kibao chake kipya kitakachojulikana kwa jina la Na bado. Alisema kibao hicho kitazinduliwa katika onyesho maalumu litakalofanyika Desemba 30 mwaka huu.

Sunday, December 9, 2012

RAIS KIKWETE AMTUNIKIA NISHANI BI KIDUDE




RAIS Jakaya Kikwete amewatunukia nishani ya heshima ya Jamhuri ya Muungano wanamuziki watatu, msanii mmoja wa maigizo na mwanariadha mkongwe.
Wasanii na wanamichezo hao wamepewa tuzo hizo leo jioni katika hafla iliyofanyika kwenye viwanja vya Ikulu, Dar es Salaam.
Utoaji wa nishani hizo ni sehemu ya maadhimisho ya sherehe za miaka 51 ya uhuru wa Tanzania Bara, zilizofanyika kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Wasanii na wanamichezo waliopewa nishani hizo ni kiongozi wa bendi ya muziki wa dansi ya Msondo Ngoma, Muhidin Gurumo, kiongozi wa zamani wa bendi ya Dar es Salaam International, marehemu Marijani Rajabu na mwimbaji mkongwe wa taarab, Fatuma Baraka 'Bi Kidude'.
Wengine ni aliyekuwa msanii maarufu wa maigizo na filamu nchini, marehemu Fundi Saidi 'Mzee Kipara' na mwanariadha mkongwe, John Steven Akwari.
Gurumo, Bi Kidude na Akwari walihudhuria hafla hiyo na kuvishwa nishani zao na Rais Kikwete wakati nishani za Marijani na Mzee Kipara zilipokelewa na watoto wao.
Nishani ya sanaa na michezo, hutolewa kwa wasanii na wanamichezo mashuhuri, ambao kazi zao za sanaa au michezo zimeipatia sifa kubwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Bi Kidude hakuweza kwenda eneo la kupokea nishani kutokana na hali ya afya yake kutokuwa nzuri. Ilibidi Rais Kikwete amfuate mahali alipokuwa ameketi na kumtunukia nishani yake.
Bi Kidude, anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka zaidi ya 100 ni mwimbaji taarbab mkongwe aliyedumu kwenye fani hiyo kwa zaidi ya miaka 50. Ni msanii pekee wa taarab mwenye sifa zilizotukuka kutokana na ukongwe wake na umahiri wake katika kuimba taarab.
Gurumo alianza muziki 1960 na kushiriki katika bendi mbalimbali kama vile NUTA, JUWATA, OTTU, Atomic Jacc, Kiko Kids, Jamhuri Jazz, Kilwa Jazz, Rufiji Jazz, Mlimani Park, Msondo Ngoma. Ametunga nyimbo nyingi zinazoelimisha jamii kuhusu kuheshimu na kufanyakazi kwa juhudi na maarifa, kulinda uhuru wa nchi, kudumisha usawa, haki na amani na kuwaasa wazazi kutimiza wajibu wao kwa kulea watoto na vijana kutimiza wajibu wao.
Marehemu Marijani, maarufu kama Jabali la Muziki, alifariki dunia mwaka 1995. Alitoa mchango mkubwa katika tasnia ya muziki, alishiriki kutunga na kurekodi nyimbo zaidi ya 103, ambazo zilirekodiwa RTD, nyimbo zake zilikuwa na mafunzo mengi kwa jamii na zinaendelea kupigwa katika vituo mbalimbali vya redio nchini.
Mzee Kipara mwaka 1962 alijiunga na waigizaji wa Redio Tanzania, pia ameshiriki maigizo na tamthiria nyingi za kwenye televisheni kama vile Hujafa hujaumbifa, Fukuto, Radi, Gharika, Tufani na Tetemo.
Mzee Akwari aliweka historia ya pekee nchini mwaka 1968 pale aliposhiriki mbio za marathoni za Olimpiki na kuumia goti na kutoka malengelenge, lakini aliushangaza ulimwengu alipoendelea na kumaliza mbio hizo. Alipoulizwa, alisema 'mimi sikutumwa kuja kuanza mbio, nimetumwa kumaliza mbio'. Maneno hayo yamekuwa yakitumika kama mifano duniani.

Friday, November 23, 2012

RAHMA, NYOTA MPYA YA TAARAB INAYONG'ARA JAHAZI


NA MOHAMMED ISSA
RAHMA Machupa ni muimbaji chipukizi wa taarab anayeibukia kwa kasi katika tasnia ya muziki huo hapa nchini.
Muimbaji huyo, anayetokea kwenye familia ya wanamuziki, katika siku za hivi karibuni ameonyesha uwezo mkubwa katika kundi lake la Jahazi Morden Taarab 'Wana wa nakshinakshi'.
Akizungumza na liwazozito mwishoni mwa wiki iliyopita jijini Dar es Salaam, Rahma anasema kipaji chake cha uimbaji  kilianza kuibuka akiwa katika shule ya sekondari ya Sinza.
Anasema  akiwa katika shule hiyo alikuwa akishiriki kuimba nyimbo mbalimbali kwa kushirikiana na wanafunzi wenzake hususan wakati wa sherehe.
Rahma, anasema mwaka 2010 baada ya kuhitimu kidato cha nne katika shule hiyo alijiunga na kundi la Mashauzi Classic chini ya Isha Mashauzi 'Jike la Simba'.
Anasema baada ya kujinga na kundi hilo na kuonyesha uwezo mkubwa, alitunga wimbo unaofahamika kama 'Sijamuona kati yenu wa kunirusha roho'
Rahma anasema wimbo huo, ulikonga vilivyo nyoyo za wapenzi wa burudani na kuanzia hapo jina lake lilianza kusikika kila kona ya mtaa.
Anasema pamoja na kuachia kibao hicho, hakufanikiwa kukaa sana kwenye kundi hilo kutokana na sababu mbalimbali na ndipo alipojiunga na Jahazi.
Muimbaji huyo mwenye umbo la wastani na sauti maridhawa, anasema baada ya kujiunga na Jahazi chini ya 'Mfalme' Mzee Yussuf aliendelea kuonyesha uwezo wake wa uimbaji.
"Kwa kweli baada ya kujiunga na Jahazi kipaji changu kimezidi kukua na kadri siku zinavyokwenda nazidi kujipatia umaarufu kwa mashabiki wangu.
"Juhudi na uwezo mkubwa nilizozionyesha katikan kundi la Jahazi ndio zimemshawishi Yussuf kunipa wimbo katika albamu yetu mpya itakayozinduliwa hivi karibuni," anasema.
Anasema kutokana na uwezo na umahiri alionyesha akiwa na kundi hilo, amekabidhiwa wimbo unaofahamika kama nipe stara.
Rahma anasema wimbo huo, ni miongoni mwa nyimbo zitakazokuwemo kwenye albamu mpya ya Jahazi itakayozinduliwa mwezi ujao.
Anasema kwa mara ya kwanza wimbo huo, atautambulisha kwa mashabiki wake kesho katika ukumbi wa Buliaga Temeke, Dar es Salaam.
"Nimejipanga vya kutosha katika utambulisho ya wimbo wangu huo, nawaahidi wapenzi na mashabiki wangu sitowaangusha," alijigamba muimbaji huyo.
Anasema akiwa katika kundi hilo atatumia uwezo wake wote kufikia lengo lake la kuwa muimbaji bora na mwenye uwezo mkubwa kama walivyo waimbaji wengine.
Rahma, anasema binafsi anavutiwa sana na muimbaji mkongwe wa taarab Rukia Ramadhani kutokana na uimbaji wake na tungo zake maridhawa.
Anasema mbali na muimbaji huyo, anavutiwa na Hadija Yussuf na Leila Rashid na kwamba anatamani siku moja awe na uwezo kama walionao waimbaji hao.
Akimzungumzia Mzee Yussuf, Rahma anasema ni muimbaji mahiri asiyependa makuu na hana upendeleo ndani ya kundi lake.
Anasema Yussuf, amekuwa na mchango mkubwa kwa waimbaji wake na kwamba anawafundisha mambo mengi hususan ya muziki.
Rahma, anasema matarajio yake ni kumiliki kundi lake la muziki na kuwa muimbaji bora ndani na nje ya nchi.
Pamoja na kuwa muimbaji bora, anaelekeza nguvu zake kwenye elimu na kwamba anafikiria kurudi darasani kuendelea na masomo mpaka afike chuo kikuu.
Muimbaji huyo, anasema amezaliwa miaka 22 iliyopita jijini Dar es Salaam na ni mtoto wa mwisho kati ya wanane katika familia yao.

Wednesday, November 21, 2012

SALHA ABDALLA: SIMUHOFII MWIMBAJI YEYOTE WA TAARAB



MWIMBAJI chipukizi wa muziki wa taarab nchini, Salha Abdalla amesema hana mpango wa kukihama kikundi chake cha Dar Modern Taarab kwa vile ameridhika kwa anachokipata.
Salha amesema tabia ya wasanii kuhamahama kutoka kundi moja hadi jingine, haiwezi kuwaletea maendeleo zaidi ya kuwashusha kiusanii.
Mwanadada huyo amesema binafsi anakipenda na kukiheshimu kikundi cha Dar Modern Taarab kwa sababu ndicho kilichomlea na kumkuza katika fani ya muziki wa taarab.
Salha alisema hayo hivi karibuni wakati alipokuwa akihojiwa na kituo cha televisheni cha Star TV mjini Mwanza.
Mwimbaji huyo mwenye sauti maridhawa na sura yenye mvuto alisema wakati alipojiunga na Dar Modern Taarab, hakuwa akifahamu kuimba, kutunga na kuimudu steji, lakini kwa sasa anaweza kuvimudu vyema vitu hivyo.
"Hivi sasa simuhofii mwimbaji yoyote wa kike kwa sababu nina uwezo wa kuimba, kutunga nyimbo na hata kuimiliki steji,"alisema mwimbaji huyo mwenye macho ya mwito.
Salha alisema hajawahi kuhama katika kikundi hicho kwa sababu ameshawaona wasanii wengi wakihama kutoka kikundi kimoja hadi kingine, lakini hawana mabadiliko yoyote makubwa kimaisha.
Amewataka wasanii wa muziki huo wajifunze kuridhika kwa kidogo wanachokipata kwa sababu maisha ni safari ndefu inayohitaji uvumilivu na subira.
"Mimi hapa Dar Modern Taarab nimefika, sina tamaa kwa sababu zinaweza kunifikisha pabaya. Ukiwa na tamaa, kuna siku unaweza usijue wapi unakoelekea,"alisisitiza mwimbaji huyo asiye na makeke.
Kwa sasa, Salha anatamba kwa kibao chake kinachojulikana kwa jina la Nauvua ushoga huku akiwa anajiandaa kuipua vibao vingine viwili vipya, vinavyojulikana kwa jina la Hasidi hana sababu na Kuomba Mungu sichoki.
Alisema kibao cha Hasidi hana sababu kinazungumzia watu wenye tabia ya kuzungumza mambo ya wenzao bila kuwa na uhakika nayo huku wakitambua wazi kwamba si ya kweli.
Alisema kibao cha Kuomba Mungu sichoki kinazungumzia dhamira aliyonayo ya kuendelea kumtegemea Mola katika kutafuta riziki huku akimuomba amwepushe na marafiki wanafiki.
Katika moja ya beti za wimbo huo, Salha anasikika akisema: "Unaweza kula, kunywa naye na kucheka naye, kumbe mbaya wako ndiye huyo huyo."
Salha ametoa mwito kwa wasanii wa kike nchini, kuzinduka na kuacha kuzubaa. Pia amewataka waache tabia ya kuwachuna wanaume kwa sababu maradhi yamekuwa mengi na kufanya hivyo ni kujikomoa wenyewe.
"Tuache kufuatilia fulani anafanya nini, tuwe na wivu wa maendeleo,"alisema Salha, ambaye tangu alipojiunga na Dar Modern Taarab, hajawahi kutoa mguu wake nje.
"Mimi nashangaa sana, sijui kwa nini sisi wanawake hatuna tabia ya kuombeana mema. Tunapenda kufurahia pale mwenzetu mmoja anapofikwa na balaa,"alisema.
"Tunapaswa kupendana, tusaidiane na kuombeana mema. Huwezi kujua Mungu amekuandikia nini,"alisisitiza.

 

BI KIDUDE KUENDELEA KUTUNZWA



Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
KAMPUNI ya Sauti za Busara Zanzibar imesema, haitaachana na mwimbaji mkongwe wa muziki wa taarabu nchini, Fatuma Binti Baraka, maarufu zaidi kwa jina la Bi Kidude.
Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Yusuf Mahmoud alisema juzi mjini hapa kuwa, wataendelea kumuenzi msanii huyo mkongwe kwa vile bado wanathamini mchango wake katika kuendeleza muziki huo.
"Tunapenda kuwahakikishia watanzania wote kwamba, kampuni yetu itaendelea kumsaidia Bi Kidude katika maisha yake yote,"alisema Mahmoud.
Mkurugenzi huyo alisema pia kuwa, kampuni yake ipo tayari kukabidhi fedha za Bi Kidude kwake mwenyewe ama kwa mtu yeyote, ambaye atampendekeza.
Alisema cha msingi ni makabidhiano hayo kufanyika kisheria, yakiwahusisha mashahidi wakiwemo wanasheria, mwakilishi kutoka serikalini na waandishi wa habari ili kuepuka utata.
Kampuni hiyo imeelezea msimamo wake huo siku chache baada ya kutoa taarifa ya mapato na matumizi ya fedha za msanii huyo, ambazo zilikuwa zikihifadhiwa na Sauti za Busara.
Kutolewa kwa taarifa hiyo kulitokana na taarifa zilizoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari kwamba, kampuni hiyo ilidhulumu fedha za msanii huyo.

Thursday, November 15, 2012

KALALE PEMA MARIAM KHAMIS



MWIMBAJI nyota wa muziki wa taarab nchini, Mariam Khamis 'Paka Mapepe' amefariki dunia na kuzikwa jana katika makaburi ya Magomeni Makuti wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam.
Mariam, ambaye ni mwimbaji wa kikundi cha Tanzania One Theatre (TOT), alifariki dunia usiku wa kuamkia juzi kutokana na matatizo ya uzazi.
Mwimbaji huyo mwenye sauti tamu na yenye mvuto, alipelekwa kwenye hospitali hiyo kwa ajili ya kujifungua baada ya kupatwa na uchungu.
Habari kutoka ndani ya hospitali hiyo zimeeleza kuwa, Mariam alilazimika kufanyiwa operesheni ili aweze kujifungua, lakini akafariki dunia. Mtoto wa mwimbaji huyo yuko salama.
Awali, familia ya marehemu Mariam ilipanga mazishi hayo yafanyike juzi, lakini iliamua kuyasogeza mbele hadi jana kutokana na maombi ya uongozi wa TOT.
Mkurugenzi wa TOT, Kepteni John Komba aliomba mazishi hayo yasogezwe mbele ili wasanii wenzake waweze kuhudhuria.
Wakati wa msiba huo, wasanii wa TOT walikuwepo mjini Dodoma kwa ajili ya kuwatumbuiza wajumbe wa mkutano mkuu wa CCM uliomalizika kwenye ukumbi wa Kizota.
Marehemu Mariam alianza kujipatia umaarufu mkubwa baada ya kuimba kibao cha Paka Mapepe alipokuwa katika kikundi cha East African Melody kabla ya kuhamia Zanzibar Stars na baadaye Five Stars Modern Taarab.
Akiwa Five Stars, Mariam aliendelea kung'ara kutokana na vibao vyake viwili vya
Uzushi wenu haunitii doa na Ndio basi tena.
Alijiunga na TOT mwaka jana na kuibuka na kibao cha Sidhuriki na lawama, ambacho kilikuwa ni majibu kwa wasanii wenzake waliokuwa wakimlaumu kwa uamuzi wake wa kujiunga na kundi hilo.
  WASEMAVYO WASANII
Baadhi ya wasanii nyota wa muziki huo wameeleza kusikitishwa kwao kutokana na kifo hicho, ambacho wamekielezea kuwa ni pigo kubwa katika fani ya muziki wa taarab.
Mkurugenzi wa Jahazi, Mzee Yusuph alisema juzi kuwa, ameumizwa vibaya kutokana na msiba huo kwa vile Mariam alikuwa ni zaidi ya msanii kwake na kwamba alikuwa karibu mno na familia yake.
"Nashindwa kupata maneno ya kuzungumza kwa sababu kifo cha Mariam kimeniuma mno kutokana na ukaribu aliokuwa nao na familia yangu. Alikuwa zaidi ya msanii kwangu,"alisema Mzee.
"Mara nyingi nilikuwa nikimkuta nyumbani akiwa na wake zangu, akishirikiana nao kwa mambo mbalimbali. Alikuwa akishirikiana nao kwa raha na shida,"aliongeza.
Kwa mujibu wa Mzee, aliwahi kumtungia Mariam kibao cha Huliwezi bifu, ambacho kilichangia kumfanya aonekane kuwa tishio kutokana na wororo na utamu wa sauti yake.
Mpiga kinanda maarufu, Issa Kamongo alisema kifo cha mwimbaji huyo ni pigo kubwa kwa sababu alikuwa na sauti tamu, inayoweza kumsahaulisha binadamu yoyote matatizo aliyonayo.
  MANENO YA MWISHO
Alipohojiwa na Burudani kwa mara ya mwisho mwaka jana baada ya kujiunga na TOT, Mariam alisema hajutii uamuzi wake huo na kwamba hajioni kama amepotea njia kufanya hivyo.
Mariam alisema uamuzi wake huo umelenga kutafuta maslahi bora zaidi na pia kujiandaa kwa maisha yake ya baadaye.
Alisema hakuondoka Five Stars kwa kufukuzwa bali alifanya hivyo kwa hiari yake mwenyewe kwa vile maisha ni kutafuta na ahangaikaye siye sawa na mkaa bure.
“Unajua linapotokea jambo, huwa yanasemwa mengi, lakini huo ndio ukweli wenyewe,”alisema.
Mariam alisema ameamua kujiunga na TOT kwa sababu ajira yake ni ya uhakika tofauti na vikundi vingine vya mitaani.
Alisema wasanii wote wanaounda kundi la TOT hawategemei mapato ya milangoni kulipana mishahara na hata wasipofanya maonyesho, malipo yao kwa mwezi yapo pale pale.
“Nawaomba mashabiki wangu wasichukie kwa sababu maisha ni kutafuta, wakubali matokeo,”alisema.
Mwimbaji huyo mwenye sura yenye mvuto alikiri kuwa, tangu alipojiunga na TOT, yalisemwa mengi juu yake, lakini hajali na anayachukulia kama changamoto katika maisha yake.
“Wengine wanasema nimekwenda TOT kujimaliza kiusanii, wengine wanasema nitakufa, lakini mimi sijali. Tangu nilipozaliwa, nilishatia saini mbele ya Mungu kwamba nitakufa siku fulani,”alisema.
Alisisitiza kuwa, ili msanii aweze kukomaa kiusanii, anapaswa kutembea katika vikundi mbalimbali kama ilivyo kwa waimbaji nyota wa muziki huo, Khadija Omar ‘Kopa’, Sabah Salum na wengineo.
“Hata mimi utafika wakati nitakuwa hivyo na kuamua kutulia kama wakongwe hao,”alisisitiza.

Tuesday, November 13, 2012

Mariam Khamis wa TOT afariki dunia




Mwimbaji nyota wa taarab nchini, Mariam Khamis amefariki dunia.
Habari kutoka kwa ndugu wa marehemu zimesema kuwa, Mariam alifariki dunia leo asubuhi kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa habari hizo, Mariam amefariki dunia kutokana na matatizo ya uzazi.
Habari kamili kuhusu kifo cha mwimbaji huyo wa zamani wa kundi la Five Stars Modern Taarab zitafuata baadaye.

00000

Haya ni mahojiano ya mwisho kati ya Mariam gazeti la Burudani yaliyochapishwa kwenye gazeti la Burudani, mtandao wa liwazozito. blogspot.com na ramozaone.blogspot.com mwaka jana.

MWIMBAJI nyota wa taarab nchini, Mariam Khamis amesema hajapotea njia kutokana na uamuzi wake wa kujiengua kutoka katika kundi la Five Stars Modern Taarab na kujiunga na kundi la Tanzania One Theatre (TOT).
Mariam alisema mjini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita kuwa, uamuzi wake huo umelenga kutafuta maslahi bora zaidi na pia kujiandaa kwa maisha yake ya baadaye.
Alisema hakuondoka Five Stars kwa kufukuzwa bali alifanya hivyo kwa hiari yake mwenyewe kwa vile maisha ni kutafuta na ahangaikaye siye sawa na mkaa bure.
“Unajua linapotokea jambo, huwa yanasemwa mengi, lakini huo ndio ukweli wenyewe,”alisema.
Mariam, ambaye aliwahi kutamba kwa kibao chake cha ‘Paka mapepe’ alisema, ameamua kujiunga na TOT kwa sababu ajira yake ni ya uhakika tofauti na vikundi vingine.
Alisema wasanii wote wanaounda kundi la TOT hawategemei mapato ya milangoni kulipana mishahara na hata wasipofanya maonyesho, malipo yao kwa mwezi yapo palepale.
Tayari mwimbaji huyo mwenye sauti maridhawa, ameshatungiwa wimbo unaojulikana kwa jina la ‘Sidhuriki kwa lawama’, na unatarajiwa kuanza kusikika hewani hivi karibuni.
“Nawaomba mashabiki wangu wasichukie kwa sababu maisha ni kutafuta, wakubali matokeo,”alisema.
Mwimbaji huyo mwenye sura yenye mvuto alikiri kuwa, tangu alipojiunga na TOT, yamesemwa mengi juu yake, lakini hajali na anayachukulia kama changamoto katika maisha yake.
“Wengine wanasema nimekwenda TOT kujimaliza kiusanii, wengine wanasema nitakufa, lakini mimi sijali. Tangu nilipozaliwa, nilishatia saini mbele ya Mungu kwamba nitakufa siku fulani,”alisema.
Alisisitiza kuwa, ili msanii aweze kukomaa kiusanii, anapaswa kutembea katika vikundi mbalimbali kama ilivyo kwa waimbaji nyota wa muziki huo, Khadija Omar ‘Kopa’, Sabah Salum na wengineo.
“Hata mimi utafika wakati nitakuwa hivyo na kuamua kutulia kama wakongwe hao,”alisisitiza.
Mbali na kuimbia kundi la Five Stars, Mariam pia aliwahi kung’ara alipokuwa katika vikundi vya East African Melody na Zanzibar Stars.Baadhi ya vibao alivyotamba navyo katika vikundi hivyo ni pamoja na ‘Huliwezi bifu’, ‘Raha ya mapenzi’ na ‘Ndo basi tena’.

Friday, October 26, 2012

IDD EL HAJJ NJEMA



Allaahu Akbar, Allaahu Akbar, Allaahu Akbar
Allaah is Great, Allaah is Great , Allaah is Great
Mwenyezi Mungu ni mkubwa, Mwenyezi Mungu ni mkubwa, Mwenyezi ni mkubwa

                  Laa ilaaha illaLlaah
there is no God, but Allaah
Hakuna Mola isipokuwa Allaah


Allaahu Akbar, Allaahu Akbar
Allaah is Great, Allaah is Great
Mwenyezi Mungu ni mkubwa, Mwenyezi ni mkubwa
 
                     Walillaahil Hamd
to Him belongs all Praise
Kwake ndiye anaestahiki kushukuriwa

Tuesday, October 23, 2012

TAARAB YA ASILI NI URITHI USIOSTAHILI KUPOTEA



Na Sammy Makilla
KWENYE miaka ya hivi karibuni kumekuwa na jitihada zenye mwelekeo potofu katika vyombo vya habari mbalimbali kupotosha maana na dhana halisi ya taarabu na kile ambacho taarabu inastahili kuwa na kuitwa.
Baada ya Watanzania kugeukawavivu wa kila kitu ikiwemo kupiga ala za muziki na kutaka mteremko katika kila jambo wale waliozuka na mitindo inayotumia mashairi, au tungo zenye vina na mizani, au isivyo hivyo wakaona urahisi ni kuita miziki yao 'modern taarab'. Miziki hiyo ninakaata sio taarabu bali inastahili kuitwa mipasho, kiduku,  rusha na roho, au mnanda na vitu kama hivyo, lakini kamwe sio taarabu.
Muziki wa taarabu una asili na fasili yake katika  watu wa Pwani na visiwani na maeneo ya mwambao wa Afrika Mashariki.Umeathirika kwa kiasi kikubwa na muziki wa Mashariki ya Kati, India na kaswida za Kiislamu.
Sifa moja kubwa ya muziki wa taarabu tofauti na wengi wanavyofikiri sio maneno na mpangilio wake, bali ala za muziki huo na mipangilio yake na ule ufundi wa kila mwanataarabu kuwa bingwa au stadi katika kupiga chombo fulani. Taarabu isipokuwa na ala hizi sio taarabu ni igizo tu  kwa kiasi fulani la kitu kama taarabu. Taarabu kwa kawaida ni kitulizo cha fikra ndani ya nyumba na katika hadhara isiyoshawishiwa na usasa na umagharibi kiasi cha kupuuza maadili na mila za wahusika.
Ala za taarabu ni nyingi na swahiba wangu Ali Salehe ambaye sio tu shabiki wa taarabu bali ni mtunzi pia wa nyimbo za taarab anaweza baadaye kunipokea hapa na kuelezea zaidi kwanini tunastahili kuwekeza kwenye taarab asilia, kama eneo la utamaduni linalostahili kuhifadhiwa na kuenziwa.
Taarabu kama walivyoiendelza kina  Siti binti Sadi, Bi Kidude, Juma Bhalo na kina Sheikh Ilyas, Machapurala bila kuwasahau mamia ya wanawake na wanaume wa Kizanzibar na Kimrima waliochangia maendeleo ya  tasnia hii adimu, lakini iliyo na  sifa ya kuwa sehemu muhimu ya utamaduni wa mwambao ya Pwani ya Afrika Mashariki na usiostahili kuachiwa kupotea.
Taarabu ni muziki wa enzi na enzi.  Ni sehemu ya utamaduni endelevu na hususan katika mikoa ya  pwani ya Afrika Mashariki. Taarabu ni ustaarabu, utaratibu, upole na uungwana.  Taarabu ni kitulizo cha mawazo na gundi ya kuunganisha familia kama sio ukoo mzima.  Sifa ambayo si mipasho, sio rusha roho sio mnanda unayo.
Taarabu kiasili sio muziki wa kucheza bali wa kutazama, kusikiliza, kutafakari na kutunza. Huu ni muziki uliokuwa ukisikilizwa na watu wenye fikira, busara na hekima kuwapa muda wa kuwaza na kuwazua juu ya hili au lile. Muziki wa kupayuka, kujiona, msshauzi, kusemana, kutukanana, kuumbuana na wenye nyimbo ambazo hazina staha, usiri wala taadibu ya kuimbwa katika mafumbo hauwezi kuitwa taarab.
Ni muziki ambao kwa kawaida una ala takriban ya ishirini. Na kwa wapenzi halisi wa taarabu hufuatilia upigaji wa kila ala na ufundi au ugwiji wa yule anayetumia ala husika. Aidha, mashairi ya taarab hayaangalii tu mlingano wa vina na mizani bali maudhui na mantiki ya kile kilichomo tena kikiwe kwenye mafumbo kuweza kusomeka vyema na wanaosikiliza wimbo husika.
Ni muziki ambao hutungwa kwa mafumbo na kwa namna ambayo hauzui familia nzima, yaani, babu, bibi, baba, mama, kaka na dada wote kujumuika kwa pamoja bila kutokea chochote ambacho kinaweza kuwafanya washindwe kuzungumza au kutazamana. Taarab kiasili uliunga pamoja familia za wakazi wa mji husika. Tofauti na hiyo inayoitwa 'modern taarab' ambayo kwa kiasi kikubwa inazivunja familia katika kila mji na kijiji.
Siti bint Saad  (1928) ndiye nyota wa kwanza wa taarab ambaye kwa mara ya kwanza badala ya kuimba kwa Kiarabu aliimba kwa Kiswahili. Alifyatua mamia ya santuri za nyimbo India na wapenda muziki wa enzi hizo hakuna aliyekosa wimbo wake nyumbani.
Muziki wa taarab asili hauna tofauti na 'Classical Music' wa Ulaya au 'Country Music' wa Marekani. Miziki hiyo ilikuwepo, imekuwepo na itakuwepo bila kubadilika wala kuitwa kwa jina jingine wala kupigwa kwa namna nyingine tofauti na ilivyokuwa, ilivyo sasa na itakavyokuwa kesho. Ni sehemu ya kudumu ya utamduni wa watu na sio kitu cha kupita na kusahaulika.
Aina hizo za miziki pamoja na kuzuka kwa miziki ya kila aina Ulaya na Marekani bado inatambulika kwa nembo na jina lake. Country ni country na classical ni classical. Hapajakuwapo muziki mwingine uliopewa umodern kuhusiana na miziki hii, hakuna kitu kama modern country au modern classic.
Rouget katika Music and Trance anafafanua kwamba  neno taarabu linatokana na neno la kiarabu  'tariba' likiwa na maana ya hisia za kusisimka, kudhihirisha au kutaka kufanya kitu Fulani, kama vile kuimba au kucheza taarab.
Kama jitihada zinavyofanyika kukarabati na kutunza maeneo kama vile Mji Mkongwe Zanzibar, Bagamoyo na Kilwa ili iendelee  kuwepo basi upo umuhimu pia wa wanaohusika katika serikali zetu kuhakikisha kuwa muziki wa taarab asili na wanamuziki wake wanakumbukwa na kuenziwa na kisha kizazi kipya kinajengwa ili kuendeleza muziki huu  kwa faida ya vizazi vijavyo. Kwa maana, ukweli ni kwamba taarabu asili ikipotea ndio utakuwa mwisho wa taarabu hapa Afrika Mashariki.
Kwanini tuhifadhi taarab asilia
Kwa bahati mbaya wengi tumezoea kuchukulia vitu kama ardhi, fedha, nyumba, magari kuwa ndio rasilimali tu. Lakini muziki wa kiasili nao ni rasilimali muhimu kimaendeleo na kisaikolojia. Bila urithi wa namna hii tutakuwa ni taifa lipolipo tu ambalo si jambo zuri.
Pamoja na mambo mengine kuifufua, kuitunza na kuiendelza taarab asili ni jambo lenye faida kadhaa ikiwemo kuendeleza mila na utamaduni wetu, kuzileta familia pamoja mara kwa mara, kujenga maadili bora katika jamii, kuwa na muziki usioendana kinyume na maadili ya dini, kukuza na kuendeleza ushairi na Kiswahili, kuwa kivutio kwa wageni wa leo na kesho na kuzienzi  na kuendeleza ala asili za muziki na upigaji wake.
Ninatoa wito maalumu pia kwa vyombo vya habari kuacha kuuchanganya umma juu ya muziki wa taarabu. Tafadhali Bi Hindu, Dida, Mzee Chapuo, Bi Chau, Miriam wa Migomba, Kristina wa Mbezi kwa kuturahisisishia hili na kubaini kwamba Afrika Mashariki kuna taarabu moja tu, nayo ni taarabu asilia ambayo kwa kawaida hupigwa na vyombo vingi, hutumia mafumbo na usiri katika nyimbo zake na hauchezwi achilia mbali kunenguliwa na kutingishiwa mawowowo.
Miziki inayojiita modern taarau iitwe kwa majina yao yanayostahili kama ni kiduku basi kiduku, au rusha roho basi rusha roho fulani, kama ni mipasho basi ni ‘Mipasho’ na kama ni mnanda uitwe ‘Mnanda’ na miziki hii isiruhusiwe kutumia mgongo wa taarabu kujijenga isipostahili.
Nikiri kuwa nilitaka sana nitembelee Lamu, Malindi, Mombasa, Tanga na Zanzibar kuzungumza na wakereketwa wenzangu wa taarabu asili kabla ya kuandika makala haya, lakini haikuwezekana. Ninaamini, hata hivyo kupitia makala haya ujumbe unaweza kufika kwa kiasi fulani.
Ninawashauri wanaharakati wa kulinda na kuendeleza utamaduni wetu kuangalia uwezekano wa haya yafuatayo: Kusaidia juhudi binafsi zilizopo za kufufua na kuendeleza vikundi vya taarabu kupitia vilabu na vyuo vya  upigaji ala za asili za taarab (mathalani juhudi za Bi Hamndani, Zanzibar), Kushirikiana na Unescokuhifadhi taarabu asili kwa kutumia Teknohama; Kuwatafuta wanataarab asilia waliko na kuwaunganisha ili kuufufua  na kuchochea kuwepo kwa muziki huo kiasili na kuongeza vionjo viwili vitatu vya kuvutia familia zaidi kuliko mtu mmoja mmoja.
Aidha, kusaidia vikundi vilivyopo, lakini havina ala za kutosha za muziki toka Misri na Uarabuni, kuenzi Ushairi katika vyombo vya habari kukuza vipaji vya washairi chipukizi na  kuchukulia Taarabu asili kama urithi usiostahili kupotea kwa msaada wa Unesco na wapenda utamaduni wetu wengineo.
Pepe: sammy.i.makilla@gmail.com

Monday, October 22, 2012

FUNGAKAZI MODERN TAARAB: WATANGAZAJI WANAZIBANIA NYIMBO ZETU




KIONGOZI wa kikundi kipya cha muziki wa taarab cha Fungazi, Karia Temba
amesema, kikundi chake kinatisha ndio sababu wapinzani wao wanafanya kampeni ili nyimbo zao zisipigwe kwenye vituo vya redio na televisheni nchini.
Karia, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la Kepteni Temba, alisema mjini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita kuwa, wamesambaza nyimbo zao kwenye vituo mbali mbali vya televisheni, lakini vingine havizipigi.
Temba, ambaye ni mchaga wa kwanza kuimba taarabu alisema, licha ya kufanyiwa hila hizo, hawawezi kukata tamaa kwa sababu lengo lao kubwa ni kufanya maajabu katika muziki huo.
Alisema kamwe hawawezi kutoa pesa ili nyimbo zao zipigwe redioni na kwenye vituo vya televisheni kwa sababu siku zote kizuri kinajiuza na kibaya kinajitembeza.
"Tumejipanga, tupo kwa ajili ya kuwapa burudani mashabiki,"alisema msanii huyo, ambaye ni ndugu wa mkali wa bongo fleva, Mheshimiwa Temba.
Alisema kabla ya kuingia kwenye gemu, waliwasoma wapinzani wao na kufahamu nini wanachokifanya, ndio sababu wamekuja kivingine na kuwashika kisawasawa.
"Watu wanafanya juhudi za kutuzuia tusitoke, lakini wasisahau kwamba tumeaga kwetu na hatufanyi muziki kwa kubahatisha,"alisema msanii huyo mwenye sauti maridhawa.
Temba alisema kundi la Fungakazi Modern Taarab linaundwa na wasanii chipukizi kutoka katika makundi mbali mbali ya muziki huo. Aliyataja makundi hayo kuwa ni Machupa Family lililotokea Mashauzi Classical na Kings Modern Taarab.
Kwa mujibu wa Temba, baadhi ya nyimbo zao mpya zinazotesa hivi sasa kwenye maonyesho yao ni Nimeiteka himaya, Usipende, Fungakazi, Maradhi ya moyo, Sweet language, Hakuna kaburi la mjinga na Usisemwe wewe nani.
Alisema wanatarajia kuizindua albamu yao hiyo mpya katika maonyesho
yatakayofanyika kwenye kumbi mbali mbali za burudani za mjini Dar es Salaam.
Fungakazi Modern Taarab wamekuwa wakirekodi nyimbo zao kwa kuwashirikisha baadhi ya wasanii nyota wa muziki wa kizazi kipya kama vile Z Anto na mwanamama mkongwe wa taarab, Khadija Omar Kopa.

Sunday, September 23, 2012

MWANAHAWA APAGAWISHA MASHABIKI DAR LIVE

Mwimbaji mkongwe wa taarab, Mwanahawa Ally (juu) akiimba wakati wa onyesho la usiku wa dhahabu lililofanyika jana kwenye ukumbi wa Dar Live uliopo Mbagala, Dar es Salaam. Picha ya chini ni waimbaji wa kundi la East African Melody wakiimba wakati wa onyesho hilo.

KHADIJA KOPA AMTUNGIA WIMBO MUMEWE

Mwimbaji nyota wa taarab nchini, Khadija Kopa akiwa na mumewe kabla ya kupanda stejini katika moja ya maonyesho yake.
Khadija Omar Kopa akilishambulia jukwaa akiwa sanjari na mabinti zake

Mwimbaji nyota wa taarab nchini, Khadija Omar Kopa ameibuka na kibao kipya kinachokwenda kwa jina la Nampenda mume wangu.
Kibao hicho alichokiimba kwa tashtiti ya hali ya juu kimeshaanza kutikisa anga za muziki kwa kupigwa mara kwa mara kwenye vituo mbalimbali vya redioni nchini.
Katika kibao hicho, Khadija anaelezea umuhimu wa wanawake kuwapenda na kuwaheshimu waume ama wapenzi wao badala ya kuwakashifu.
Anasema yeye binafsi anampenda mumewe na kumpatia kila anachokihitaji na kwamba katu hawezi kumuhini chochote.

MDOGO WAKE MASHAUZI AFUATA NYAYO

Binti mdogo Saida, ambaye ni mdogo wake wa nne wa Isha Mashauzi, ameanza kuonyesha cheche katika uimbaji wake na kuleta tegemeo la  kufikia upeo wa dada yake. Salma ni mmoja wa waimbaji katika kundi la Mashauzi Classic

Monday, September 17, 2012

JOKHA KASSIM AKANA KUWAPIGA VIJEMBE MZEE YUSSUF NA LEILA RASHID


"KUPIGANA vijembe katika tungo za taarab hakujaanza leo wala jana, tangu enzi za marehemu Leila Khatib, ambaye alikuwa akirushiana maneno na Khadija Kopa."
"Sisi waimbaji chipukizi tumerithi kwao. Siwezi kushangaa kusikia mtu anampiga vijembe mwenzake kwenye nyimbo za taarab," ndivyo alivyoanza mazungumzo yake mwimbaji taarab mwenye sura na sauti yenye mvuto, Jokha Kassim,ambaye kwa sasa yupo katika kundi la T-Moto.
Jokha alitoa ufafanuzi huo kutokana na kuwepo kwa madai kuwa, nyimbo zake nyingi anaziomba zimelenga kuwapiga vijembe, mkurugenzi wa kikundi cha Jahazi, ambaye pia ni mumewe wa zamani, Mzee Yussuf na mkewe wa sasa, Leila Rashid.
Baadhi ya mashabiki wa muziki huo wanadai kuwa, tangu Jokha alipoachana na Mzee, amekuwa akitunga nyimbo zenye mwelekeo wa kumpifa vijembe mumewe huyo pamoja na mkewe Leila, ambaye pia ni mwimbaji wa Jahazi.
Mzee alibahatika kuzaa na Jokha mtoto mmoja wa kiume, anayejulikana kwa jina la Yussuf na waliwahi kufanyakazi pamoja katika makundi mbali mbali ya muziki huo.
Jokha alisema kwa kawaida, muziki wa taarab ni wa malumbano na majibizano na kwamba imekuwa ikifanyika hivyo tangu enzi na enzi.
Alisema tangu akiwa mdogo, waimbaji wengi wa muziki huo walikuwa wakiimba nyimbo za kujibimizana hivyo haoni ajabu kwa waimbaji wa sasa nao kufuata mkondo huo.
"Nakumbuka marehemu Leila Khatib alikuwa akipigana vijembe sana na Khadija Kopa. Lakini lengo lao halikuwa baya, ilikuwa ni njia fulani ya kuvuta mashabiki kwenye maonyesho yao,"alisema.
"Hivyo hata sisi tumerithi kutoka kwao hao, ambao tunaamini ni wakongwe kwetu na wanaheshimika kwenye tasnia ya muziki wa taarab,"alisisitiza Jokha.
Hata hivyo, mwimbaji huyo alisema si kweli kwamba nyimbo nyingi anazoimba zimewalenga Yussuf na Leila. Alisema lengo lake ni kufikisha ujumbe kwa jamii kuhusu masuala mbali mbali.
Jokha alisema majibizano kwenye taarab ni mambo ya kawaida na kwamba kufanya hivyo kunaleta changamoto kwa mashabiki na vikundi vya muziki huo.
Alisema kibao chake kipya kinachojulikana kwa jina la 'Domo la udaku' hakimlengi mtu yeyote kama baadhi ya mashabiki wanavyodai. Alisema mpangilio wa mashairi ya wimbo huo yamekuwa yakileta tafsiri mbaya, ambapo wengi wanaamini kuna mtu aliyekusudiwa.
Jokha alisema lengo lake katika kutunga wimbo huo ni kuielimisha jamii juu ya mambo mbali mbali kama ulivyo wajibu kwa msanii.
Mwimbaji huyo mwenye macho yenye mvuto pia alisema kwa sasa anajiandaa kuachia kibao kingine kipya, ambacho alitamba kwamba kitakuwa moto wa kuotea mbali.
Akizungumzia maisha yake ya sasa baada ya kujiunga na T-Moto, alisema mambo yanamwendea vizuri na kipaji chake kinazidi kuongezeka.
Alisema tayari wamesharekodi albamu inayoitwa 'Aliyeniumba hajakosea', ambayo imekuwa gumzo mkubwa kwa mashabiki wa muziki huo.
Jokha alisema baada ya albamu hiyo, wanatarajia kuipua albamu zingine mbili zitakazojulikana kwa majina ya Mimi staa na Domo la udaku.
Alizitaja baadhi ya nyimbo zitakazokuwemo kwenye albamu hizo kuwa ni Mwanamke hashuo na Wewe si daktari wa mapenzi.

REHEMA TAJIRI, MWANAMUZIKI ALIYEAMUA KUJITOSA KWENYE TAARAB


BAADA ya ukimya wa muda mrefu, mwanadada Rehema Tajiri ameibuka upya, lakini safari hii ameamua kujitosa kwenye muziki wa miondoko ya zouk na taarab.
Rehema, ambaye alianza kuchomoza kimuziki mwaka 2002, anatarajia kurekodi albamu ya zouk kwa ajili ya kuuaga muziki wa dansi kabla ya kuhamia kwenye mipasho.
Mwanamama huyo ameamua kujitosa kwenye taarab kwa kile anachodai kuwa, muziki huo una mvuto mkubwa ikilinganishwa na dansi na kwamba ameshaanza kufanya vizuri katika kikundi cha Jahazi Korongwe chenye maskani yake Temeke, Dar es Salaam.
Kikundi hicho ni maalumu kwa ajili ya kupiga nyimbo za kuiga za vikundi mbali mbali vya taarab na kwa Rehema, amekuwa akipendelea zaidi kuimba nyimbo za Mwanahawa Ally wa kundi la East African Melody, Leila Rashid na Khadija Yussuf wa kundi la Jahazi.
Akizungumza na Uhuru mwishoni mwa wiki iliyopita mjini Dar es Salaam, Rehema alisema anaamini kuwa, huo ni mwanzo tu wa safari yake ndefu katika muziki huo kwa vile lengo lake kubwa ni kuimba nyimbo zake mwenyewe za taarab.
Mama huyo wa watoto wawili alisema amekuwa kimya kwa muda mrefu kutokana na kutingwa na masomo na pia matatizo ya kifamilia. Hata hivyo, alisema kwa sasa anamshukuru Mungu kwamba ameweza kuvivuka vikwazo vingi vilivyokuwa vikimkwaza katika kazi yake hiyo.
Rehema alianza kung’ara kimuziki baada ya kuibuka na albamu yake ya kwanza inayojulikana kwa jina la Sumu ya Ndoa. Alirekodi albamu hiyo kwa kushirikiana na baadhi ya wanamuziki nyota waliokuwa wakiunda bendi ya Msondo Ngoma, wakiwemo marehemu Moshi William na Maneno Uvuruge.
Baadhi ya vibao vilivyokuwemo kwenye albamu hiyo ni pamoja na Maisha Vijijini, Binadamu hawana wema, Karibu shemeji na muziki ni kazi.
Rehema alisema alipata mafanikio makubwa kutokana na mauzo ya albamu hiyo kwa vile aliweza kuwalipa wanamuziki alioshirikiana nao pamoja na kupata faida kidogo.
Alirekodi albamu yake ya pili mwaka 2005, inayojulikana kwa jina la Ni wako tu, lakini safari hii hakuwatumia wanamuziki maarufu. Alimtumia mwanamuziki mwingine nyota wa kike, Dotnata.
Baadhi ya nyimbo zilizomo kwenye albamu hiyo ni Sirudi nyuma, Namsaka mbaya wangu, Penzi la uongo na Nicheze na nani.
“Katika albamu hii, sikutaka kuwashirikisha wanamuziki wengine kwa sababu mara ya kwanza nilisakamwa sana na maneno. Wapo waliodai kuwa, nyimbo zote za kwenye albamu ya kwanza nilitungiwa na marehemu Moshi, wengine wakazua uongo kwamba alikuwa mpenzi wangu wakati si kweli,”alisema Rehema.
“Na hata nilipomshirikisha Dotnata, walimwengu hawakukosa maneno ya kuzungumza. Na nilipotengeneza video ya wimbo wangu kwa kumshirikisha Dokta Cheni, pia yakasemwa maneno mengi. Ndio sababu niliamua kuwa kimya kwa muda,”aliongeza mwanamuziki huyo.
Rehema, ambaye ni mke wa zamani aliyekuwa kipa namba moja wa Yanga, marehemu Sahau Kambi alisema, albamu yake itakayofuata hivi karibuni itakuwa ya muziki wa zouk.
Alisema ameshaanza maandalizi kwa ajili ya kurekodi albamu hiyo, lakini hakuwa tayari kuzitaja nyimbo zitakazokuwemo ndani yake. Alisema atazitangaza baada ya kuzikamilisha.
Baada ya albamu hiyo, Rehema alisema itakayofuata itakuwa ya taarab, ambayo atarekodi kwa kushirikiana na wasanii mbali mbali nyota wa muziki huo.
Pamoja na kurudi kwenye gemu kivingine, Rehema pia ameamua kuwa mwanasiasa na hivi karibuni alichaguliwa kuwa mjumbe wa mkutano mkuu wa UWT mkoa wa Dar es Salaam na mjumbe wa baraza la UWT la wilaya ya Temeke.
Aliibuka wa pili katika uchaguzi wa mkoa baada ya kuzoa kura 448 wakati katika uchaguzi wa wilaya, aliibuka kinara kwa kuzoa kura 538.
Rehema alisema hii ni mara yake ya pili kujitosa katika uchaguzi wa jumuia hiyo, mara ya kwanza ikiwa miaka mitano iliyopita, ambapo kura hazikutosha.
Mwanamama huyo alisema ameamua kujitosa kwenye siasa kwa lengo la kufuata nyayo za baba yake, marehemu Hamisi Tajiri, ambaye aliwahi kushika nyadhifa kadhaa za uongozi za CCM katika ngazi ya tawi na kata.
Marehemu Tajiri, ambaye alikuwa mmoja wa waigizaji magwiji wa maigizo wa Redio Tanzania Dar es Salaam (RTD) miaka ya 1970 hadi 1980, pia aliwahi kuwa mwenyekiti wa Chama cha Baiskeli Tanzania (CHABATA).
“Nimeamua kujitosa kwenye siasa kwa lengo la kufuata nyayo za baba yangu na pia kutetea haki za akina mama,”alisema Rehema.
Kwa mujibu wa Rehema, uamuzi wake huo hauna lengo la kutaka kuwania ubunge ama udiwani katika uchaguzi mkuu ujao, bali kuwatumikia wanawake wenzake.
“Nataka kuwanasua akina mama, hasa wa vijijini, ambao wanatumika zaidi katika kazi za kilimo na kijamii kuliko akina baba,”alisisitiza.
Hata hivyo, alikiri kuwa kazi hiyo ni ngumu na inahitaji moyo kutokana na ukweli kwamba, ni hulka kwa akina mama kutokuwa na utamaduni wa kupendana zaidi ya kusemana.
Alisema kutokana na mapenzi yake katika kuwainua kina mama, hata nyimbo nyingi anazotunga zimekuwa zikizungumzia maisha yao na matatizo yanayowakuta katika jamii.
Pamoja na kujitosa kwenye siasa, Rehema alisema hatarajii kuitumia fani ya muziki kumbeba kama ilivyo kwa wanasiasa wengine. Alisema atatumia nguvu ya marehemu baba yake na ushawishi alionao kwa wanawake wenzake.
Rehema amewahi kutunga wimbo wa kumpongeza Rais Jakaya Kikwete kwa kutoa nafasi nyingi za uongozi kwa wanawake na pia kwa uongozi wake mzuri na uliotukuka kwa watanzania.
Alisema kwa sasa, ameshatunga nyimbo mbili kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa CCM unaotarajiwa kufanyika mwezi ujao mkoani Dodoma, lengo likiwa kuwahamasisha wanachama wake kuchagua viongozi wenye uwezo wa kukivusha na kukifikisha chama mbali zaidi.
Amewashukuru waandishi wa vyombo mbali mbali vya habari kwa kumpa ushirikiano mkubwa katika kipindi chote alichokuwa kwenye fani hiyo na kusisitiza kuwa, bila wao asingeweza kufika alipo sasa.
“Kwa moyo wa pekee, nawashukuru sana waandishi wa habari, walifanyakazi kubwa sana ya kunitangaza hadi nikafahamika nchi nzima. Bila wao, nisingekuwa Rehema ninayejulikana sasa,”alisema.
“Pia nawaomba mashabiki wangu wasiwe na wasiwasi wowote. Najua hawajaniona kwa muda mrefu, lakini nipo, nilikuwa nasoma na pia nilipatwa na matatizo ya kifamilia, lakini sasa mambo yapo safi,”alisema.
Rehema alisema baadhi ya mashabiki wake walikuwa wakimtumia barua pepe na wengine kuwasiliana naye kwenye facebook kutaka kujua alipo. Alisema alishindwa kujibu meseji zingine kutokana na matatizo aliyokuwa nayo.
“Lakini nawapenda sana wote. Watarajie kuniona tena kwenye muziki hivi karibuni na pia kwenye ulingo wa kisiasa,”aliongeza.

Thursday, September 13, 2012

UNAFAHAMU LOLOTE KUHUSU TAUSI WOMEN MUSICAL CLUB? SUBIRI KUSOMA HABARI ZAKE HIVI KARIBUNI

Wasanii wa kikundi cha (Tausi Women Musical Club) wakicharaza ala ya Muziki wakati wa uzinduzi wa kikundi hicho uliofanywa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,Dk Ali Mohamed Shein, katika ukumbi wa Salama Bwawani Hotel.(22/10/2011)

Watoto waliozaliwa katika familia za wanamuziki wa Taarab,Neema Suri,(kulia) na Nabil Mohamed wakionesha vipaji vyao katika fani ya kupiga udi katika uzinduzi wa kikundi cha Wanawake cha Taarab,kiitwacho (Tausi Women Musical Club),uzinduzi wa kikundi hicho umefanywa na Rais wa zanzibar Dk Ali Mohamed Shein,katika ukumbi wa salama Bwawani Hotel juzi.(22/10/2011).

Tuesday, September 11, 2012

VIDEO ZA ALBAMU TATU ZA DAR MODERN TAARAB ZAKAMILIKA


KIKUNDI cha Dar Modern Taarab kimekamilisha kazi ya kurekodi video za albamu zake tatu ilizozizindua hivi karibuni kwenye ukumbi wa hoteli ya Travertine iliyopo Magomeni, Dar es Salaam
Mkurugenzi wa kundi hilo, Mridu Ally alisema wiki hii kuwa, video hizo za albamu zote tatu zilikamilika wiki iliyopita.
Mridu alisema picha za video hizo zilipigwa katika maeneo mbali mbali ya Jiji la Dar es Salaam na Bagamoyo na lengo lilikuwa kuzipa vionjo tofauti.
Mkurugenzi huyo alitamba kuwa, video hizo ni moto wa kuotea mbali na kuongeza kuwa, anaamini zitakuwa kivutio kikubwa kwa mashabiki wao.
"Video za albamu zote tatu tumezitengeneza kwa umakini mkubwa na utaalamu wa hali ya juu, kilichobakia ni kuanza tu kuzisambaza kwa mawakala wetu,"alisema.
Mridu alisema tayari baadhi ya video hizo zimeshaanza kuonyeshwa katika vituo mbalimbali vya televisheni nchini kabla ya kuanza kuwafikia mashabiki.
Albamu hizo tatu, ambazo zilizinduliwa kwa mpigo ni Ndugu wa mume, Toto la Kiafrika na Ninauvua ushoga.

VIDEO YA DUNIA DUARA IPO TAYARI


VIDEO ya kibao cha Dunia Duara ya kundi la muziki wa taarab la Kings Modern Taarab, inatarajiwa kuanza kuonekana hivi karibuni kwenye vituo mbali mbali vya televisheni nchini.
Akizungumza na Spoti Leo, Mkurugenzi wa kundi hilo, Majaliwa Hamisi alisema kazi ya kurekodi video hiyo inatarajiwa kukamilika wiki hii.
Kibao hicho kipo kwenye albamu ya My Heart ya kundi hilo na kimeimbwa na mwimbaji mkongwe, Mwanahawa Ally, ambaye kabla ya kurejea Kings Modern alikuwa akiimbia kundi la T-Moto.
Mwanahawa, ambaye amewahi kupachikwa majina ya Kinyago cha Mpapure na Chipolopolo, alikiri hivi karibuni kuwa, hakuwa na furaha alipokuwa kwenye kundi la T-Moto kama ilivyo awapo Kings Modern.
Kibao cha My Heart kimeimbwa na Young Hassan Ally wakati kibao cha Full Style kimeimbwa na Hanifa Mpita, aliyejiunga na kundi hilo hivi karibuni akitokea Mashauzi Classics.
Kwa mujibu wa Majaliwa, kibao cha Riziki mwanzo wa chuki kilichoimbwa na mshindi wa shindano la Bongo Star Search mwaka jana, Mariam ndicho pekee, ambacho hakijatengenezewa video.
"Karibu vibao vyote vilivyomo kwenye albamu yetu mpya vimeshatengenezewa video zake, isipokuwa Riziki mwanzo wa chuki,"alisema.
CHANZO CHA HABARI: SPOTI LEO

ALBAMU YA SHAKILA YA MAMA NA MWANA YAJA


ALBAMU binafsi ya mwimbaji mkongwe wa taarab nchini, Shakila Saidi ya Mama na Mwana, imechelewa kukamilika baada ya binti yake kupatwa na matatizo.
Shakila kwa kushirikiana na binti yake wa kwanza, Mwape Kibwana walitarajia kutoa albamu hiyo, ambayo tayari walishaanza kurekodi nyimbo zake, lakini wameshindwa kuikamilisha baada ya binti huyo kuugua.
Shakila alisema wiki hii kuwa, binti yake huyo alikumbwa na matatizo ya uja uzito na kusababisha washindwe kukamilisha kazi hiyo kwa muda waliopanga.
"Binti yangu, ambaye nimeshirikiana naye kurekodi albamu hiyo amepata matatizo wakati wa uja uzito, ikawa bahati mbaya tumeshindwa kukamilisha kazi hiyo," alisema Shakila.
Naye Mwape alisema wanatarajia kuendelea na kazi hiyo baada ya afya yake kutengemaa. Alisema anaamini kazi hiyo itakamilika baada ya muda si mrefu.
Kwa mujibu wa Mwape, wanatarajia kukamilisha kazi hiyo baada ya kurejea kutoka Dodoma, ambako wamealikwa kwenda kutioa burudani.
CHANZO CHA HABARI: SPOTI LEO

Monday, September 3, 2012

BI KIDUDE MUZIKI SASA BASI


Kulia kwangu ni Bi Hidaya, anayemuuguza Bi Kidude hospitalini, tukizungumza huku tukipiga soga na mgonjwa pia ambaye yuko mbele yetu jioni ya leo, Hindu Mandal. 

Na Mahmoud Zubeiry
HALI ya afya ya msanii mkongwe nchini, Fatuma Binti Baraka, maarufu kama Bi Kidude inaendelea vizuri katika hospitali ya Hindu Mandal, Dar es Salaam alipolazwa na wakati wowote kuanzia kesho anaweza kuruhusiwa kurudi nyumbani, ila familia imemstaafisha rasmi sanaa.
BIN ZUBEIRY alifika katika wadi namba 202 hospitali ya Hindu Mandal, jioni hii kumjulia hali Bi Kidude, mwimbaji maarufu na mkongwe haswa wa muziki wa Taarabu duniani na ‘alhamdulillah’, Bi Mkubwa anaendelea vizuri.
Watu wanapishana kuingia na kutoka kumsalimia Bi Kidude, wengine wakitoka nje ya nchi, baadhi mashabiki wake na baadhi ndugu na jamaa.
Lakini jambo moja tu Bi Kidude analaani vikali ni taarifa za kuzushiwa kufariki dunia mwishoni mwa wiki. “Watu wamenizushia kufa Zubeiry, na wewe hukuja kuniona, ulifikiri nimekufa? Mi mzima, si unaniona, cheki,”alisema Bi Kidude na kuuvuta mkono wa BIN ZUBEIRY kwa nguvu akiuminya ‘kibaunsa’ kuonyesha nguvu za misuli yake, kwamba yeye yuko mzima.
Bi Kidude alikuwa mcheshi wakati anazungumza na watu mbalimbali waliomtembelea hospitali na alimuambia BIN ZUBEIRY kwamba anasumbuliwa na maradhi ya sukari, ambayo ni maradhi yake kwa muda mrefu, ila yalimzidia kwa kukiuka taratibu za vyakula.
“Kweli nilikuwa naumwa, ngozi yote ilivuka hii, nilikonda sana, ila sasa Alhamdulillah mi mzima, mi mzima, naweza kuondoka,”alisema.
Mwonekano wa Bi Kidude ni mtu mwenye afya njema japokuwa amelala kitandani wadi namba 202, Hindu Mandal na sasa anainuka kwenda mwenyewe msalani.
Amezuiwa kuvuta sigara tangu alazwe hospitalini hapo na inaonekana kwa hamu ya sigara anaomba aondoke hata sasa hivi. Amewekewa waangalizi wawili, wa kike na wa kiume, wote wakiwa ni wanafamilia.
Hidaya Abdi Omar, mkwe wa Kidude ambaye ni mmoja wa waangalizi wake hospitalini hapo amesema kesho Bi Mkubwa huyo atafanyiwa vipimo ambayo kama vitakuwa namna ambavyo madaktari wa hospitali hiyo wanataka, ataruhusiwa.
Hidaya ni mke wa mtoto wa mdogo wake wa kiume Bi Kidude, aitwaye, Abdallah Baraka ambaye hivi sasa ni marehemu. “Bi Kidude hakubahatika kuzaa, lakini ndugu zake wamezaa, mimi ni mke wa mtoto wa kaka yake Bi Kidude, na kwa sasa ndiye naishi na huyu bibie kulingana utu uzima na hali yake pia,”anasema Hidaya.
Hidaya anasema msimamo wa familia umekwishapita kwamba Bi Mkubwa huyo sasa hataruhusiwa kufanya kazi yoyote ya sanaa, atakuwa wa kupumzika tu acheze na wajukuu.
“Hatapanda tena jukwaani popote, sasa basi tena, akae tu apumzike, familia imekwishaamua,”alisema. Familia hiyo hiyo imeamua Bi Kidude asipigwe picha yoyote akiwa wadini.
Ndugu zake wote watatu ambao ni wadogo zake Bi Kidude wamekwishafariki dunia na kwa sasa Bi Kidude anakula matunda ya watoto wa ndugu zake hao, ambao kwa sasa ndio wanamlea.
Hakuna promota yeyote wa tamasha au kiongozi wa serikali, au chombo chochote cha sanaa aliyekwenda kumjulia hali Bi Kidude wadini, zaidi baadhi ya wasanii wanapiga simu tu na kwa hilo wala Bi Mkubwa huyo hajali, watu wanaokwenda kumuona na kumfariji kwake wanatosha.
Bi Kidude alianza kusumbuliwa na maradhi mwezi uliopita, lakini baadaye akapata ahueni na kufanya mahojiano hadi na vyombo vya habari, lakini ghafla mambo yakabadilika tena na amerudi hospitali, ila kwa sasa unaposoma habari hii yuko vizuri Hindu Mandal.
Bi Kidude ni gwiji wa muziki katika Bara la Afrika, katika fani ya muziki wa mwambao ambao hujulikana kwa jina la Taarabu. Muziki huu ambao ni mchanganyiko wa muziki toka nchi za Kiarabu na vionjo vya muziki wa Kiafrika umekita sana katika mwambao wa Afrika Mashariki yaani Zanzibar, Mombasa, Lamu na kwingineko.
Fatuma binti Baraka au Bi Kidude, alizaliwa katika kijiji cha Mfagimarigo Zanzibar katika familia ya watoto saba (7). Baba yake Mzee Baraka alikuwa ni mfanyabiashara wa nazi, zao ambalo ni la kutumainiwa sana Zanzibar.
Bi Kidude anasema hafahamu tarehe halisi aliyozaliwa, isipokuwa anachojua ni kwamba alizaliwa wakati rupia ikitumika kama fedha, na vilevile ana hakika ni kabla ya Vita Kuu ya Kwanza ya Ulaya.
Wataalamu wa mahesabu baada ya kupata taarifa hizo wakampigia mahesabu na kumkabidhi miaka yake kwamba ni zaidi ya miaka 90.
Bi Kidude anasema uimbaji aliuanza tangu alipokuwa na umri wa miaka 10 na alijifunza kutoka kwa msanii mkongwe na aliyetamba sana enzi hizo Sitti Binti Saad. Anasema wageni wengi kutoka sehemu mbalimbali walikuwa wakifika Zanzibar kuja kumwona Sitti, na kwa vile Bi Kidude na Sitti walikuwa wako karibu basi yeye alikuwa akiwapeleka wageni wale nyumbani kwa Bi Sitti, wakifika huko wageni walikuwa wakiingia ndani na yeye kubakia nje, kule ndani Bi Sitti alikuwa akiwaimbia wale wageni, na yeye huku nje alikuwa akimsikiliza kwa makini na kumfuatiza jinsi alivyokuwa akiimba. Aliendelea hivyo hadi akawa mahiri sana katika uimbaji.
Alipokuwa na miaka 13, kwa mara ya kwanza alitoroka nyumbani kwao Zanzibar na kukimbilia Tanzania Bara, baada ya kulazimishwa kuolewa. Lakini alipokuwa kigoli wa kutosha kuolewa aliolewa ingawa ndoa hiyo nayo haikudumu kutokana na manyanyaso aliyokuwa akiyapata, hivyo aliamua kukimbilia kaskazini mwa Misri ikiwa ni katika miaka ya 1930, huko aling'ara sana katika fani yake ya uimbaji na uchezaji ngoma. Lakini ilipofika miaka ya 1940 aliamua kurudi nyumbani Zanzibar ambako aliendelea na shughuli zake uimbaji.
Bi Kidude hategemei kazi moja tu ya kuimba, kwani pia ni mfanyabiashara ya 'wanja' na 'hina' ambavyo anavitengeneza yeye mwenyewe, pia ni mtaalamu wa matibabu kwa dawa za mitishamba na zaidi ya hayo ni mwalimu mzuri sana wa 'Unyago' na ameanzisha chuo chake mwenyewe na anasema katika wanafunzi wake wote hakuna aliyepata talaka kutoka kwa mumewe.
Watu wanasema 'Utu uzima dawa' Bi Kidude ana upeo mkubwa sana wa akili kwani pamoja na kukulia katika mazingira yaliyogubikwa na tamaduni za kiarabu ambapo mwanamke anatakiwa wakati wote akiwa hadharani ajifunike, Bi Kidude aliliona hili katika upeo mwingine kwamba ni sheria tu ya kitamaduni toka Uarabuni, hivyo aliamua kuvunja sheria hiyo na kuondoa hijabu mwilini mwake, na sasa hivi anavaa kama Mtanzania na si kama Mwarabu. Lakini hakubakia hapo alivunja na miiko mingine zaidi ya kutokunywa na kuvuta, kwani Bi Kidude anakunywa pombe na kuvuta sigara jambo ambalo si kawaida kwa wanawake Zanzibar.
Bi Kidude amekwisha tembelea nchi nyingi sana ikiwa ni pamoja na Oman, Ufaransa, Hispania, Ufini, Ujerumani na Uingereza.
Amekwisha pata tuzo mbalimbali ikiwa ni pamoja na ile ya Tamasha la Filamu la Nchi za Jahazi (ZIFF) mwaka 1999 tuzo ni ya maisha. Pia mwaka jana tuzo ya WOMAX ilienda kwake.
Nyimbo alizowahi kuimba ni pamoja na Muhogo wa jang'ombe, na anaimba kwa Kiswahili na Kiarabu. Hakuwahi kupata elimu nyingine zaidi ya Quraan.
CHANZO CHA HABARI: BIN ZUBEIRY

Sunday, September 2, 2012

JAHAZI WAJA NA ALBAMU MPYA

Mmoja wa waimbaji wa kikundi cha Jahazi, Mariam Mwinjuma

Fatma Kassim, mmoja wa waimbaji wenye mvuto wa kundi la Jahazi

KIKUNDI cha taarab cha Jahazi kinatarajia kupakua albamu mpya hivi karibuni itakayojulikana kwa jina la Wasiwasi wako ndio maradhi yako.
Akizungumza na blogu ya rusha roho wiki hii, kiongozi wa kundi hilo, Mzee Yusuph alisema albamu hiyo itakuwa na nyimbo sita.
Mzee alisema tayari baadhi ya nyimbo zimeshakamilisha wakati zingine bado zipo kwenye hatua ya mwisho.
Kwa mujibu wa Mzee, miongoni mwa nyimbo zitakazokuwemo kwenye albamu hiyo ni Mgodi wa Dhahabu, ambao umeshaanza kusikika kwenye vituo mbali mbali vya redio nchini.
Mzee alisema amepania kufanya mabadiliko makubwa kwenye muziki wa taarab ili kuwapa mashabiki ladha tofauti badala ya ile waliyoizoea.
"Sisi kama Jahazi tunapenda tufanye kile kitu mashabiki wanapenda, hivyo tunawaahidi mambo mapya kabisa katika albamu yetu hii mpya,"alisema.
Albamu hiyo itakuwa ya tisa tangu kundi la Jahazi lilipoanzishwa mwaka 2006. Albamu zingine zilizopita za kundi hilo ni Tupendane wabaya waulizane, Wagombanao ndio wapatanao, Mpenzi chokolate, Daktari wa mapenzi, Two in one, VIP na My Valentine.

Saturday, September 1, 2012

MZEE YUSUPH AFUNGUA KAMPUNI YA KUSAMBAZA KAZI ZAKE


MSANII wa mziki wa Taarabu nchini Mzee Yussuf ameamua
kufungua kampuni yake ya usambazaji ijulikanayo kama MY
Collection kwa ajili ya kusambaza kazi zake.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Meneja Mauzo wa
Kampuni hiyo Mussa Msuba amesema wameamua kufungua duka
kwa ajili ya kuuza CD NA DVD za bendi ya Jahazi inayongozwa na
Mzee Yussuf.
Duka hilo lililopo makutano ya barabara ya likoma na
Muhonda, linajihusisha na uzaji wa DVD za taarabu kwa jumla na
rejareja kwa ajili ya kuwaweka karibu wapenzi wake ili waweze
kupata burudani kupitia nyimbo zao kwa kuwaburudisha wakiwa
majumbani.
Msuba amesema kuwa Mzee Yusufu yupo mbioni kutoa albamu
yake ya mduara itakayokuwa hivi karibuni ambayo ni yake binafsi.
Mbali na hilo, bendi hiyo itatoa video yake ya Live za albamu zake
zote za Two in One,Kazi ya Mungu, Nakula ka Naksh
Naksh,tupendane, Daktari wa Mapenzi, ambazo zitakuwa madukani kwa
ajili ya kuwapa wapenzi wao burudani wakiwa majumbani mwao.
Naye Mzee Yussuf aliongeza kwa kusema ameanzisha kampuni yake
binafsi baada ya kuona kwamba kazi zake nyingi zimekuwa
zikichakachuliwa kutokana na kuwepo kwa wizi wa kazi za sanaa.
Kampuni yake imekuwa ikisambaza kazi zake kwa ajili ya kuogopa
kuibiwa kutokana na wimbi la kazi za wasanii nchini.
Duka lililopo mtaa wa Muhonda na Likoma kwa ajili ya CD za
Jahazi pekee.
Mbali na duka hilo mzee Yusufu anamiliki duka lingine la Nguo
lililopo Magomeni Mapipa kwa ajili ya kujiongezea
kipato chake.
Bendi ya Jahazi mpaka sasa imekwisha toa albam nane ambazo
zipo madukani zinauzwa kwa ajili ya watu wotekupata burudani
wakiwa majumbani mwao.
Kwa sasa bendi hiyo ipo mbioni kuachia albamu yake ya tisa
ambayo aijapewa jina inatarajiwa kuzinduliwa mwezo Octoba kwa
ajili ya kutoa burudani kwa wapenzi wao na kuwataka mashabiki
wao kuja kuangalia na kusikiliza nyimbo mpya popote pale
wanapotoa burudani zao katika kumbi mbalimbali za jijini Dar es
salaam.