KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Tuesday, December 20, 2016

SIJAWAHI KUOMBA TALAKA KWA MUME WANGU-LEYLA


MWIMBAJI nyota wa muziki wa taarab nchini, Leyla Rashid amesema kamwe hajawahi kuomba talaka kutoka kwa mumewe, Mzee Yusuph.

Aidha, Leyla amesema anajisikia upweke kuendelea kuimba nyimbo za muziki huo bila kuwa karibu na Mzee.

Leyla alisema hayo hivi karibuni, baada ya kudaiwa kuwepo na shinikizo la kumtaka aachane na muziki huo na kuungana na mumewe, ambaye kwa sasa ameacha kuimba taarab na kuwa alhaji.

Hivi karibuni, dada wa Mzee Yusuph, Khadija Yusuph, alikaririwa akisema kuwa, Layla anafanya makosa kuendelea kuimba taarab wakati mumewe ameachana na muziki huo.

Khadija alisema kwa mujibu wa sheria za dini ya kiislamu, mke anapaswa kufuata maelekezo ya mumewe iwapo amemtaka kuachana na fani ambayo yeye ameshaiacha.

Akijibu tuhuma hizo, Leyla alisema ni kweli amewahi kugombana na mumewe mara kadhaa, lakini kamwe hakuwahi kuomba talaka.

Pia, alisema sio kweli kwamba Mzee aliwahi kumtishia kwamba atampa talaka iwapo hataacha kuendelea kujihusisha na muziki huo.

"Hajaniambia acha, isipokuwa mimi mwenyewe najihisi kupungukiwa na kitu fulani.Nilizoea tunakuwa pamoja stejini, lakini sasa hayupo tena,"alisema Leyla.

Mwanamama huyo alisema hadi sasa hajaamua nini la kufanya, bali anamuachia Mungu na kusisitiza kuwa, ni kawaida kwa binadamu kutokosa la kusema, lakini hababaishwi na maneno yao.

"Kama mtu anasema, mwache aseme, mdomo ni mali yake," alisema mwanamama huyo mwenye watoto wawili na kusisitiza kuwa, muda wa kuachana na muziki huo ukifika, atafanya hivyo.

Leyla alisema mumewe hadi sasa hajaonyesha shaka yoyote kwake kwa uamuzi wake wa kuendelea na muziki huo, zaidi ya kumtia moyo na kufuatilia maendeleo yake kila anaposafiri mikoani kwa maonyesho mbalimbali.

TMK MODERN TAARAB YAZINDULIWA KWA KISHINDO




KIKUNDI kipya cha taarab cha TMK Modern, mwishoni mwa wiki kilifanya onyesho kabambe la uzinduzi, lililofanyika kwenye ukumbi wa Dar Live, Mbagala, Dar es Salaam na kuhudhuriwa na mashabiki lukuki.

Katika onyesho hilo, kundi hilo lilisindikizwa na bendi ya Twanga Pepeta, Madada sita na mwimbaji nyota wa muziki huo, Leila Rashid kutoka Jahazi.

Wakiongozwa na waimbaji nyota na wakongwe, Mwanahawa Ali, Omar Tego na Maua Tego, kundi hilo liliwafanya mashabiki wafurike kwa wingi stejini kucheza muda wote wa onyesho.

Wakati huo huo, uongozi wa kundi jipya la muziki wa taarab nchini, 'Yah TMK Modern Taarab', umewataka wapenzi wa muziki huo, kuipokea bendi yao ambayo inaanza rasmi maonyesho yake ya katika kumbi mbalimbali hapa nchini.

Mkurugenzi wa kundi hilo, Said Fella amesema baada ya kufanya utambulisho wa kundi hilo mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye ukumbi wa Dar Live, sasa wanaanza rasmi maonyesho katika kumbi mbalimbali za burudani hapa nchini.

Fella alisema kundi hilo litaanza onyesho lake la kwanza Desemba 23, mwaka huu, kwenye ukumbi wa CCM Kigamboni, wakati siku ya mkesha wa Krismas watakuwa kwenye ukumbi wa Mpo Africa, ulioko
Tandika.

Alisema Desemba 25, kundi hilo litakuwa ndani ya ukumbi wa Lekam ulioko Buguruni na Desemba 26, litakuwa kwenye ukumbi wa Lanch Time, Mazense.

Fella alisema kuwa kundi hilo limejipanga kutoa burudani ya aina yake na kudhihirisha kuwa, kwa sasa ndilo moto wa kuotea mbali.

"Lengo letu ni kutoa burudani, tumejipanga kutoa burudani ya aina yake, wanamuziki wapo vizuri na kila mtu anajisikia kufanya kazi yake vizuri kabisa," alisema Fella.

Kundi hilo linaundwa na wasanii mbalimbali nguli, akiwepo Mwanahawa Ali, Fatma Mcharuko, Aisha Vuvuzela, Omar Tego, Maua Tego na wapiga vyombo kina Mohamed Mauji, Mussa Mipango, Chid Boy (kinanda) na Babu Ally Kichupa.

Tuesday, December 13, 2016

ISHA MASHAUZI KUFUNGA NA KUFUNGUA MWAKA NA "KISS ME"

Mwanamuziki maarufu wa muziki wa taarabu hapa nchini Aisha Ramadhani a.k.a Isha Mashauzi (pichani)  anataraji kuachia kibao kipya cha kufunga na kufungua mwaka kitachokwenda kwa jina la "Kiss Me".

Akizungumza na Globu ya Jamii jijini Dar es salaam leo Isha Msahauzi amesema kuwa amekuwa kimya kwa kipindi kirefu hivyo kibao hicho kitaweza kuwarudisha mashabiki wake katika mstari.

“Hii ni zawadi ya kufunga na kufungua mwaka kwa mashabiki wangu. Hivyo mashabiki wangu wapendwa wajue kuwa nyimbo hiyo ambayo ipo katika viwango vya hali ya juu itakonga nyoyo zao",   amesema Isha Mashauzi, akiongezea kuwa imefanywa katika studio za Sophia Records  zilizopo kinondoni”

Ameongeza: "Waliniona  nimekuwa kimya katika taarabu sasa nimerudi tena na hiki kibao ambacho watafurahi wenyewe...."

Tuesday, December 6, 2016

TMK TAARAB KUTAMBULISHWA RASMI KWA MASHABIKI DESEMBA 17



NA VICTOR MKUMBO

TANZANIA ni miongoni mwa nchi za Ukanda wa Pwani, ambazo zina bendi nyingi za muziki wa taarabu.

Muziki wa taarabu umekuwa ukipandachati kila kukicha na wasanii mbalimbali wanaibuka na kufanya vyema.

Hata hivyo,kuna aadhi ya bendi zimekuwa zikianzishwa mara kwa mara na kufanya vizuri, lakini zingine zikifa kutokana na sababu mbalimbali.

Pia,uongozi mbovu unachangia wasanii wengi kuhama bendi moja hadi nyingine kutokana na maslahi duni, tofauti na zamani, ambapo walifanyakazi kwa moyo hata kama hawapati kiwango cha fedha cha kuridhisha.

Kwa sasa, kuna ushindani mkubwa ndani ya muziki huo huku wasanii wakongwe wakitamani kutoka kwenye bendi kubwa na kuhamia katika bendi zisizokuwa na majina makubwa ili kufuata neema.

Bendi mpya ya taarabu ya TMK Modern, imeanzishwa kwa mara ya kwanza waka huu, ikiwa imesheheni wasanii wakongwe, ambao kwa namna moja au nyingine wanaweza kuipa mafanikio kutokana na umahiri wao.

Wasanii, wakongwe waliojiunga na bendi hiyo, wametoka katika bendi za muziki wataarabu ambazo zinatamba kwa sasa kwa ajili ya kuongeza upinzani ndani ya tasnia hiyo.

Kutokana na jinsi uongozi waTMK Modern Taarab, kujipanga vyema, huenda ikawa moja ya bendi ambazo zitatikisa kwenye muziki huo na watu wanasubiri kwa hamu kuona vitu vipya.

Bendi hiyo inaongozwa na Mkurugenzi, Said Fella, mbaye ni mmoja wa watu waliodumu kwenye tasnia ya muziki kwa muda mrefu.

Wasanii ambao wapo chini ya Fella wamekuwa akifanikiwa zaidi kila kukicha na kufanya matamasha ndani na nje ya nchi.

Fella anamiliki kituo cha wasanii cha kubwa na Wanawe, ambapo ndani yake kuna wasanii wa kila sanaa.

Kituo hicho kimetambulika kwa kuwatoa wasanii wachanga na kufanya vyema kwenye tasnia ya muziki, tofauti na jinsi ilivyokuwa inatarajiwa na wengi.

Wapo wasanii ambao wametokea kwa Fella na kwa sasa wanafanya vizuri na nyimbo zao haziishi kusikilizwa na kutazamwa na mashabiki wa muziki katika ukanda wa AfrikaMashariki.

Kundi la TMK Modern Taarab, linaundwa na wasanii nguli kina Mwanahawa Ally, FatmaMcharuko, Aisha Vuvuzela, Maua Tego na OmaryTego.

Wasanii waliotoka Mkubwa na Wanawe ni Amina Mnyalu, Jeza Adam, Hassan Saleh na Ibrahim Said.

Wapiga ala ni Mussa Mipango, Father Mauji, Chid Boy na Babu Ally ambao wamejikitika katika upande wa kupiga gita na kinanda.

Akizungumzia kundi hilo hivi karibuni, Mkurugenzi Mtendaji, OmaryTego, alisema wameanzisha bendi hiyo mwaka huu ili kuhakikisha wanaleta mapinduzi katika muziki wa taarab nchini.

Alisema kwa kiasi kikubwa wamejipanga, hivyo wana imani kubwa yakuufikisha mbali muziki wa taarab.

Alisema bendi hiyo inaundwa na wasanii wakongwe waliopitia katikabendi mbalimbali za muziki wa aarab ili kuhakikisha wanasimama vyema.

Alisema kuna changamoto mbalimbali wasanii wanaounda kundi hilo,
ambazo wamepitia awali na hivyo kuamua kuunda kundi la pamoja na kurudi upya katika muziki huo.

“Wasanii wanaounda kundi la TMK Modern Taarab, wametokea atika bendi mbalimbali, ili kuhakikisha tunafikia malengo kwani pia wamepitia kwenye changamoto nyingi hadi kufika hapa walipo sasa,” amesema.

Anasema kuwa adi sasa wameshakamilisha kurekodi jumla ya nyimbo saba ambazo zitakuwepo kwenye albamu zao mpya zitakazotoka mwakani.

Amesema kuwa baadhi ya nyimbo zimeshaanza kusikika katika vituo mbalimbali vya redio na kufanya vizuri.

Nyimbo zilizoanza kusikika ni pamoja na Figisufigisu zimekwisha, mtunzi akiwa Tego, Sina pupa Mungu atanipa, iliyoimbwa na Manahawa, Kibaya kina mwenyewe ya Aisha Vuvuzela na Ndoa, iliyoimbwa na Jeza Adam.
 “Nyimbo ambazo zimeshakamilika zimetungwa kwa ustadi mkubwa na hivyo msikilizaji hatachoka kupata burudani safi, ikiwa ni pamoja na ujumbe uliopo,” amesema.

Mkurugenzi huyo anasema kuwa bado wapo katika mikakati ya kuboresha kundi lao ili kuhakikisha linaimarika zaidi.

Amesema kuwa apo wasanii wakubwa kutoka kwenye bendi kongwe, ambao wanatarajiwa kujiunga nao hivi karibuni.

“Tumejipanga vyema kuhakikisha tunafanya mapinduzi kwenye muziki wa taarab kwani pia bado tupo kwenye mikakati ya kuimarisha kundi letu. Kuna baadhi ya wasanii ambao watajiunga na sisi hivi karibuni na wanatoka kwenye bendi kongwe,” amesema.

Ameongeza uwa wanatarajia kufanya uzinduzi wa kuitambulisha rasmi bendi hiyo Desemba 17, mwaka huu, katika onyesho la kwanza litakalofanyika kwenye ukumbi wa Dar Live.

Amesema uwa uzinduzi huo unatarajiwa kuwa wa aina yake kutokana na maandalizi ya muda mrefu waliyoyafanya.

Katika uzinduzi huo, watasindikizwa na wasanii mbalimbali, wakiwemo  Amani Temba na Said Chege, Dullah Makabila, Madada sita kutoka Mkubwa na Wanawe na kundi zima la The African Stars ‘TwangaPepeta’.

Baada ya uzinduzi huo, wataendelea kufanya maandaliziyaalbamu zao mbili, ambazo zitatoka kwa mpigo.

Monday, October 31, 2016

KUNDI JIYA LA TAARAB LA TMK LAIBOMOA JAHAZI, COAST MODERN TAARAB


Ule usemi unaosemwa na baadhi ya wadau wa taarab ya kuwa "Jahazi Modern Taarab bila ya Mzee Yussuf linasuasua" unaonekana kama unakubalika kwa asilimia fulani baada ya bendi hiyo kupoteza waimbaji muhimu pamoja na wapiga vinanda.

Majina ya Fatma Nyoro, Chidi Boy, Moh'd Mauji, Mussa Mipango, Kichupa kwa sasa hayatosikika kwenye maonesho ya Jahazi.

Pia kuna tetesi kuwa Khadija Yussuf ameenda Wakaliwao kwa Thabit Abdul.

Bendi ya TMK pia imeibomoa Coast Modern Taarab kwa kumpa shavu Omary Teggo na dada yake.
Pia Bi Mwanahawa Ali (JEMBE GUMU) ametilishiwa saini katika bendi hiyo huku akipewa wimbo wa "SINA PUPA MUNGU ATANIPA".

Thursday, October 20, 2016

ISHA MASHAUZI, LEYLA RASHID NANI ZAIDI KUONYESHANA KAZI KESHOKUTWA DAR




NI vita ya “Sura Surambi” na “Nina Moyo Sio Jiwe”.  Ndiyo unavyoweza kusema kuelekea mpambano wa waimbaji nyota wa taarab malkia Leyla Rashid na Isha Mashauzi.

Onyesho hilo linasosubiriwa kwa hamu kubwa litafanyika Jumamosi ya tarehe 22 mwezi huu ndani ya ukumbi wa Dar Live Mbagala, jijini Dar es Saalam.

Bendi mbili kubwa za taarab, Jahazi Modern Taarab na Mashauzi Classic ndiyo zitakazosindikiza mpambano wa mahasimu hao wawili.

“Sura Surambi” ni moja ya nyimbo ambazo piga ua lazima iwe kweye ratiba ya Isha Mashauzi wakati iwe isiwe Leyla naye lazima aidumbukize ngoma yake ya “Nina Moyo Sio Jiwe” katika orodha ya nyimbo atakazotumbuiza.

Tangu onyesho hilo litangazwe, waimbaji hao wameingia kwenye vita vikubwa vya maneno ambapo kila mmoja amejinasibu kuibuka na ushindi.

Tuesday, September 27, 2016

DK SHEIN AONGOZA HARAMBEE YA KUCHANGIA UJENZI WA TAASISI YA SITI BINTI SAAD

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akimkabidhi picha ya kuchora Mmiliki na Mkurugenzi wa Kampuni ya Pennyroyal inayojenga Hoteli Kubwa ya Kimataifa huko Matemwe Kaskazini Unguja Bw.Brian Thomson (kulia) iliyonadishwa na kuinunua kwa Shilingi za Kitanzania Milioni nane(8) pia  akiwa amechangia Shilingi Miliion Ishirini na tano katika  Harambee ya kuchangia ujenzi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Sadi,hafla ilifanyika jana katika Ukumbi wa Hayat Hotel Mjini Unguja,wakati huohuo ameahidi kuanzisha Chuo cha Muziki Academy katika Mkoa wa Kaskazini,ambapo mradi huo utagharimu shilingi za kitanzania Miliioni mia sita, wakiwemo  na walimu pamoja na zana  zote

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akimkabidhi picha ya kuchora Mmiliki na Mkurugenzi wa Kampuni ya Pennyroyal inayojenga Hoteli Kubwa ya Kimataifa huko Matemwe Kaskazini Unguja Bw.Brian Thomson (kulia) iliyonadishwa na kuinunua kwa Shilingi za Kitanzania Milioni nane(8) pia  akiwa amechangia Shilingi Miliion Ishirini na tano katika  Harambee ya kuchangia ujenzi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Sadi,hafla ilifanyika jana katika Ukumbi wa Hayat Hotel Mjini Unguja,wakati huohuo ameahidi kuanzisha Chuo cha Muziki Academy katika Mkoa wa Kaskazini,ambapo mradi huo utagharimu shilingi za kitanzania Miliioni mia sita

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein,(kushoto) na Mtoto wa Mwanahamis Ali 9years mkaazi wa Shaurimoyo Mjini Unguja akichora kaburi alilozikwa Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad (katika picha ya kuchora chini) baada ya kukabidhiwa picha hiyo Rais, wakati wa harambee ya Ujenzi wa Ofisi ya taasisi hiyo  iliyofanyika jana katika ukumbi wa Hayyat Hotel Mjini Unguja

Baadhi ya Mawaziri wakiwa katika hafla ya harambee ya Ujenzi wa Ofisi ya taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad inayotarajiwa kujengwa Fumba Mkoa wa Magharibi Unguja,wakiwa katika hafla iliyofanyika jana katika ukumbi wa Hayyat Hotel

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein,(katikati) Rais Mstaafu wa Jamhuri ya muungano Mzee Mwinyi(kushoto)  pia Mlezi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad na Mwenyekiti wa taasisi hiyo Bi Nasra Mohamed Hilal (wa pili kuli) wakimuangalia Mtoto wa Mwanahamis Ali 9years mkaazi wa Shaurimoyo Mjini Unguja akichora kaburi alilozikwa Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad wakati wa harambee ya Ujenzi wa Ofisi ya taasisi hiyo inayotarajiwa kujengwa Fumba Mkoa wa Magharibi Unguja,katika hafla iliyofanyika jana katika ukumbi wa Hayyat Hotel

Kikundi cha Muziki cha Rahatul Zamani kikitumbuiza  wakati wa Harambee ya kuchangia   ujenzi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad hafla iliyofanyika jana katika Ukumbi wa Hayatt Hotel Mjini Unguja,mgeni rasmi akiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein

Mmiliki na Mkurugenzi wa Kampuni ya Pennyroyal inayojenga Hoteli Kubwa ya Kimataifa huko Matemwe Kaskazini Unguja Bw.Brian Thomson (wa pili kushoto) akiwa na msaidizi wa kampuni ya ujenzi ya Pennyroyal inayojenga Hoteli Kubwa ya Kimataifa huko Matemwe Kaskazini Unguja Bw.David Haycok (kushoto)pamoja na Wasaidi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein,(kutoka kulia) Mzee Burhani Saadat Haji na Chimbeni Kheir wakiwa katika Harambee ya kuchangia   ujenzi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad iliyofanyika jana katika Ukumbi wa Hayatt Hotel Mjini Unguja

Baadhi ya Viongozi na Wafanyabishara wa makampuni mbali mbali wakiwa katika Harambee ya kuchangia   ujenzi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad iliyofanyika jana katika Ukumbi wa Hayatt Hotel Mjini Unguja

Baadhi ya Viongozi na Wafanyabishara wa makampuni mbali mbali wakiwa katika Harambee ya kuchangia   ujenzi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad iliyofanyika jana katika Ukumbi wa Hayatt Hotel Mjini Unguja

Baadhi ya Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakijaza fomu maalum za kuchangia fedha kwa ajili ya ujenzi wakati wa harambee ya Ujenzi wa Ofisi ya taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad inayotarajiwa kujengwa Fumba Mkoa wa Magharibi Unguja, katika hafla iliyofanyika jana ukumbi wa Hayyat Hotel

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akimkabidhi picha ya kuchora ya Marehemu Bibi Siti Binti Saad Mkurugenzi wa Kampuni ya Azam Marine Fasty Ferry Huseein Mohamed wakati wa harambee ya Ujenzi wa Ofisi ya taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad inayotarajiwa kujengwa Fumba Mkoa wa Magharibi Unguja, katika hafla iliyofanyika jana ukumbi wa Hayyat Hotel Mjini Zanzibar,[Picha na Ikulu.]

Sunday, August 21, 2016

JK, MAKAMU WA RAIS SAMIA WAONGOZA MAZISHI YA MAREHEMU SHAKILA SAIDI

HII ni picha aliyopiga kwa mara ya mwisho marehemu Bi Shakila Saidi alipohudhuria mkutano mkuu maalumu wa CCM uliofanyika Julai 23, mwaka huu mjini Dodoma
Rais mstaafu Jakaya Kikwete akitia saini kitabu cha maombolezo baada ya kuwasili nyumbani kwa marehemu Bi Shakila Saidi, Mbagala Charambe, Dar es Salaam jana.
MAKAMU wa Rais Samia Suluhu Hassan akitia saini kitabu cha maombolezo baada ya kuwasili nyumbani kwa marehemu Bi Shakila Saidi
MKE wa Rais mstaafu Jakaya Kikwete, Mama Salma Kikwete akitia saini kitabu cha maombolezo nyumbani kwa marehemu
WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Michezo na Sanaa, Nape Nnauye akimkaribisha Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan nyumbani kwa marehemu Bi Shakila Saidi
Makamu wa Rais akiwafariji baadhi ya ndugu wa marehemu
WAZIRI Nape akiteta jambo na mmiliki wa blogu ya Michuzi, Ankal Muhidin Issa Michuzi. Katikati ni Mwenyekiti wa Chama Cha Muziki wa Dansi, Athumani Msumari
BAADHI ya waumini wa dini ya kiislamu wakijiandaa kuuswalia mwili wa marehemu Bi Shakila
MAKAMU wa Rais akishiriki kwenye dua ya kumuombea marehemu Shakila
JENEZA lenye mwili wa Bi Shakila likipelekwa makaburini. PICHA KWA HISANI YA BLOGU YA MICHUZI NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS

Saturday, August 20, 2016

MKONGWE WA TAARAB NCHINI BI SHAKILA SAIDI AFARIKI DUNIA



Bi Shakila Tatu Said Msengi muimbaji maarufu wa Taarab, hatunae tena. Jioni leo ameanguka ghafla na alipokimbizwa hospitali moja jirani na kwake Mbagala Charambe alipofika huko Bi Shakila alikata roho.

Bi Shakila alikuwa mzaliwa wa peke yake kwa baba na mama yake, alizaliwa tarehe 14 June 1947, tarehe moja na mwanamuziki mwingine mkongwe Mabruk Khamis wa Kilimanjaro Band anaejulikana kwa jina la Babu Njenje.

Mama yake Babu Njenje alikuwa na tatizo la kutoa maziwa hivyo Babu Njenje alianza kwa kunyonyeshwa na mama yake wa Bi Shakila.

Kwa kadri ya maelezo yake mwenyewe Bi Shakila alianza muziki akiwa na miaka 6, alipokuwa na umri wa miaka 12, aliteuliwa kumuimbia Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alipotembelea Pangani, wakati wa kutafuta Uhuru.

Na ni baada ya hapa ambapo aliweza kusikika na Bwana Khatibu ambaye aliweza kumshawishi kujiunga na kundi la Taarab lililokuwa pale Pangani lililoitwa Taarab Kijamvi, hakukaa sana katika kundi hilo akalazimika kuhamia Tanga kumfuata Bwana Khatib ambaye walibahatika kuzaa watoto watano.

Huko Tanga alijiunga na kundi la Shaabab Al Watan. Katika kundi hili hakupata nafasi ya kuimba katika kadamnasi, hivyo baada ya muda si mrefu Bi Shakila akiambatana ma mumewe walihamia kundi lililokuwa likimilikiwa na Mzee Kiroboto lililoitwa Young Noverty.
Pamoja na Bi Shakila kupata uzoefu mkubwa wa kuimba mbele za watu kundi hili lilikuwa ni kutumbuiza bure katika vikao vya kahawa.

Hatimae kundi hili lilikufa na zaidi ya nusus ya wasanii kujiunga na kundi la Black Star lililokuwa la mwarabu mmoja aliyekuwa anafanya kazi bandarini aliyeitwa Hassan Awadh na hapo ndipo Bi Shakila alipoanza kufahamika, na akapewa nyimbo kama Jongoo Acha Makuu, Mpenzi Amini, Majuto Yamenipata.

Sifa zake zikaanza kuenea Afrika Mashariki. Mwaka 1972 tajiri mwingine Mwarabu aliyeitwa Sudi Said akanunua vyombo vipya vizuri na kuanzisha kundi la Lucky Star Musical Club, hapo Bi Shakila na wenzie tisa walihama Black Star na kuhamia Lucky Star.

Kwa kuwa kundi lilianzishwa wakati Bi Shakila alikuwa mja mzito, mtoto aliyezaliwa alimuita Lucky kwa ajili ya tukio hilo. Nyimbo nyingi zinazofahamika hadi leo za Bi Shakila zilirekodiwa wakati yuko kundi hili.

Mapenzi Yamepungua, Kifo cha Mahaba. Macho Yanacheka. Bi Shakila aliendelea na kundi hili hadi mwaka 1984, Baada ya kifo cha mumewe alipumzika kwa muda kasha akahamia Dar es salaam ambapo alijiunga na kundi la JKT alilodumu nalo mpaka alipostaafu.
CHANZO CHA HABARI: BLOGU YA KITIME

Monday, August 15, 2016

MZEE YUSSUF AACHANA NA MUZIKI WA TAARAB, AAMUA KUMREJEA ALLAH



Gwiji wa mziki wa taarabu nchini Mzee Yusuf ‘Mfalme wa Taarab’ amethibitisha kuwa ameachana na kazi hiyo takribani miezi miwili iliyopita.

Taarifa zilizoenea katika mitandao ya kijamii hasa kuanzia jana zimeeleza kuwa mwanamziki huyo ameachana na mziki na kuamua kumrudia Mungu.

Akizungumza, mmiliki huyo wa bendi ya Jahazi Modern Taarab amethibitisha kuwa taarifa hizo ni za kweli: “Nashangaa taarifa hizi zinasemwa leo. Ni suala la muda mrefu… takribani miezi miwili iliyopita na sababu ni kuwa nimeamua kumrudia Allah,” Mzee Yusuf alisema.

Mwimbaji huyo wa huyo wa taarabu mzaliwa wa Zanzibar alipoulizwa kuwa ni suala gani lililomsukuma hata achukue maamuzi hayo magumu, alijibu kwa kifupi, “ndivyo tunavyofundishwa na viongozi wa dini.”

Yusuph aliyetamba na vibwagizo kama “Nichumu, nikisi….mwaaaa,” katika baadhi ya nyimbo zake, amesema familia yake imeupokea uamuzi wake kwa mtazamo chanya na kwamba inamuunga mkono.

“Kwa sasa nitaimba kaswida zenye mafundisho ya dini,” amesema nyota huo huku akiahidi kufanya mkutano rasmi kuelezea suala hilo.

Mfalme huyo aliyeonekana kuwa ni gwiji wa taarabu ya kisasa (modern taarab) amezaliwa visiwani Zanzibar mwaka 1977. Aidha amejihusisha na sanaa nyingine kama maigizo.

Ni mshindi wa tuzo katika tasnia ya muziki wa taarab zikiwemo ya Kilimanjaro Music Award 2014-15.

    Kikundi bora cha mwaka taarab – Jahazi Modern Taarab
    Mtunzi bora wa mwaka taarab- Mzee Yussuf
    Mwimbaji bora wa kiume taarab – Mzee Yussuf

Wednesday, May 25, 2016

KHADIJA YUSUPH: SIWEZI KUONDOKA JAHAZI KWA SABABU YA LEILA RASHID


MWIMBAJI nyota wa taarab wa kikundi cha Jahazi, Khadija  Yusuph amesema kamwe hawezi kuondoka katika kikundi hicho kwa sababu ya kutokuelewana kwake na wifiye, Leila Rashid.

Khadija amesema hawezi kuliacha kundi hilo kwa sababu ya maneno ya wanadamu na kwamba kwa kuwa kazi yao ni kusema, atawaacha wafanye hivyo hadi watakapochoka.

"Mimi nipo Jahazi na nitaendelea kuwepo kama kawaida,"alisema Khadija, ambaye ni dada wa kiongozi wa kundi hilo, Mzee Yusuph.

Khadija alitoa ufafanuzi huo baada ya kuulizwa swali kuhusu uhusiano wake na Leila, mke wa Mzee Yusuph, ambaye wamekuwa hawaelewani kwa muda mrefu sasa.

Alisema uhusiano kati yake na Mzee Yusuph ni mzuri na wamekuwa karibu zaidi, tofauti na ilivyokuwa miaka ya nyuma,  lakini tatizo kubwa lipo kwa wifiye Leila.

Mwanamama huyo mwenye sauti ya chiriku alisema kamwe ugomvi wake huo na Leila hauwezi kuwagawa mashabiki wa kundi hilo kwa sababu kila wanapokuwa kazini, kila mmoja anaheshimu kazi yake.

Khadija alisema inawezekana hali ya kutokuelewana kati yake na Leila, imekuwa ikijitokeza mara kwa mara kutokana na kufanyakazi katika kundi moja, lakini wangekuwa makundi tofauti, huenda uhusiano wao ungekuwa mzuri.

"Kaka yangu anao wake wawili, lakini siwezi kusema simpendi mke mdogo, nampenda mke mkubwa, nawapenda wote,"  alisisitiza mwimbaji huyo wa zamani wa kundi la East African Melody.

"Ukewenza haukuanza kwa Leila na mke mkubwa wa Yusuph, ulianza tangu enzi ya mabibi na mababu zetu. Hata mimi niliwahi kuolewa ukewenza, lakini sikuwahi kugombana na wifi zangu wala
mkwe wangu. Ukewenza ni mume, kama mume hayupo vizuri, lazima tofauti zitazuka,"alisema.

Khadija alisema haamini iwapo wapo watu wanaomfitinisha yeye na Leila, isipokuwa huo ni uamuzi binafsi wa wifi yake kwa vile kila anapojaribu kumsalimia, amekuwa akimnunia na kukataa kumuitikia.

"Basi na ndio mpaka leo ipo hivyo, hanisalimii, simsalimii, hakuna fitina, labda yeye mwenyewe. Na hata kama yupo katika familia kweli, sawa na mimi sijamkataa kwa sababu ningemkataa, basi hata ile siku ya mwanzo aliyokwenda kuolewa ningemkataa,"alisema Khadija.

Akizungumzia uimbaji wake, Khadija alisema sauti yake imeendelea kuwa maridhawa kwa vile hatumii kilevi cha aina yoyote.

"Sauti hii ni orijino kama mashabiki wanavyoniita kwamba nina sauti ya chiriku. Situmii kitu chochote, nipo kikawaida tu. Hiki ni  kipaji kutoka kwa mama yangu, maana naye alikuwa mwimbaji
wa kikundi cha Culture,"alisisitiza.

Khadija pia alikanusha madai kuwa anapenda wanaume wenye umri mdogo kuliko wa kwake. Amesema madai hayo hayana ukweli wowote kwa sababu mara zote mbili, ameolewa na wanaume wenye umri mkubwa kuliko wa kwake.

Khadija amesema kitu pekee anachokijutia katika maisha yake ni ugomvi kati yake na Leila kutokana na kuihusisha familia yake, akiwemo mama yake mzazi.

"Mama yangu katukanwa sana. Nimelia saba kwa matusi yake. Kwa kweli najuta kuwemo katika muziki wa taarab,"alisema.

Khadija pia amekiri kuwa tangu Leila alipojifungua hivi karibuni, hajawahi kwenda kumuona mtoto aliyezaliwa.


Tuesday, April 19, 2016

AMIN SALMIN WA T-MOTO AKANA KUWA NA BIFU NA MZEE YUSSUF


MKURUGENZI wa kikundi cha taarab cha Tanzania Moto, Amin Salmini, amesema hana ugomvi wala bifu na Mkurugenzi wa kikundi cha Jahazi, Mzee Yussuf.

Hata hivyo, Amin amekiri kuwepo kwa upinzani wa kibiashara kati yao, lakini umelenga zaidi katika kazi na kuinua biashara ya muziki huo.

Amin alisema ni kweli nyimbo nyingi zinazoimbwa na mkewe, Jokha Kassim, zimelenga kumpiga vijembe mke wa Mzee Yussuf, Leila Rashid, lakini ni katika ushindani wa kibiashara.

"Ni kweli kuna upinzani wa kibiashara kati yangu na Mzee Yussuf, lakini ni upinzani wa kibiashara uliopo kati yetu, ni upinzani wa kikazi zaidi.

"Halafu mimi huwa simjibu Mzee Yussuf, huwa najibu shairi. Ninavyofanya vile, nalenga kuonyesha ubora wangu katika kutunga nyimbo, si vinginevyo,"alisema Amin.

Mtoto huyo wa Rais wa zamani wa Zanzibar, Dk. Salmin Amour, alisema ukimya wa kundi la Tanzania Moto, umetokana na hali yake kiafya kutokuwa nzuri.

"Watu wengi wanadhani kuwa siasa ndio imenifanya niwe kimya, lakini ukweli ni kwamba siasa haiwezi kunipoteza katika muziki wa taarab.

"Hii ilikuwa ni kazi maalumu katika uchaguzi tu na sasa umekwisha, hivyo najipanga kurudi Dar es Salaam, kuendelea na mapambano ya kuinyanyua T Moto,"alisisitiza Amin.

Mkurugenzi huyo amekiri kuwa bado kundi lake halijapata mafanikio makubwa kutokana na muziki huo kwa vile bado halijasimama vizuri.

Alisema hadi sasa, kundi hilo limefanikiwa kurekodi albamu mbili, ikiwemo Domo la Udaku, ambayo ilishika chati katika vituo vya redio na televisheni nchini.

Amin alisema pia kuwa, si kweli kwamba majibizano ya nyimbo katika muziki wa taarab yanaweza kujenga chuki na uhasama kati yao. Alisema muziki wa taarab umelenga zaidi katika kujibizana.

"Kwa mfano, Khadija Kopa na marehemu Nasma Kidogo walikuwa wakiimba nyimbo za kujibizana, lakini hawakuwa na uhasama zaidi ya kujiongezea mashabiki.

"Vivyo hivyo hata mimi sioni kama kwa kufanya hivyo ninapoteza mashabiki, isipokuwa nimekuwa nikijiongezea mashabiki kutokana na tungo zangu,"alisisitiza.

Amin alikiri kuwa ni kweli kuwa kwa sasa wanajiandaa kurekodi wimbo mpya, ambao umelenga kuujibu wimbo mwingine wa Jahazi. Aliutaja wimbo huo kuwa ni 'Hakuna kuomba poo'.

Alisema wamefanya hivyo kutokana na ukweli kwamba Jahazi ndilo kundi lililopo juu kimuziki hivi sasa, hivyo si rahisi kufanya ushindani na kundi lingine zaidi ya Jahazi.

"Ukitaka ushindani katika muziki wa taarab, ni lazima ushindane na kundi lililo juu yako,"alisema.

Amin alisema katika albamu yao mpya wanayotarajia kuitoa hivi karibuni, itakuwa na nyimbo tano na wanatarajia kuwa na msanii mmoja mpya, ambaye hakutaka kumtaja jina lake.

Alisema kundi hilo litaendelea kuwa chini ya Jokha Kassim na kwa wapiga ala, watakuwa chini ya Omary Kisila.

JAHAZI YAWANYAKUA AISHA VUVUZELA, ZUBEDA MLAMALI



KUNDI la muziki wa taarab la Jahazi, limeendelea kujiimarisha baada ya kuwanyakua waimbaji wawili nyota, Aisha Othman 'Vuvuzela' na Zubeda Mlamali.

Aisha, anatokea kundi la Modern Taradance wakati Zubeda alikuwa mwimbaji wa kundi la East African Melody.

Mkurugenzi wa Jahazi, Mzee Yussuf amethibitisha kujiunga kwa nyota hao wawili katika kundi lake hilo.

Waimbaji hao walianza kuonekana kwenye maonyesho ya Jahazi, mwishoni mwa wiki iliyopita, wakati kundi hilo lilipofanya onyesho kwenye ukumbi wa Travertine, Magomeni, Dar es Salaam.

"Ni kweli nimeamua kuwachukua Aisha na Zubeda ili kuongeza nguvu katika kundi langu. Kikubwa ni kwamba nimezingatia uwezo mkubwa wa waimbaji hawa.

"Naweza kusema uwezo wao ndio umenishawishi kuwachukua na kuanzia sasa, wataendelea kuwepo Jahazi na Mungu akipenda katika albamu ijayo, naweza kuwapa nyimbo mpya,"alisema Mzee Yussuf.

Hata hivyo, Mzee alisema kupewa nyimbo kwa wasanii hao kutategemea kujituma kwao, nidhamu nzuri na utendaji mzuri wa kazi.

Sunday, March 27, 2016

TAARAB RASMI YA KUMPONGEZA DK.SHEIN KWA USHINDI WAKE

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akisalimiana na Katibu Mkuu wa CCM Taifa Abdulrahman Omar Kinana wakati alipowasili viwanja vya Ukumbi wa Salama Hotel ya Bwawani Mjini Zanzibar kuhudhuria katika Taarab rasmi ya kumpongeza kwa ushindi mkubwa wa Kishindo katika uchaguzi Mkuu wa marudio,iliyocharazwa na Vikundi vya Culture Muzicul Club,BigStar na Zanzibar One (katikati) Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akisalimiana na Mama Asha Balozi katika Ukumbi wa Salama Hotel ya Bwawani Mjini Zanzibar jana katika Taarab rasmi ya kumpongeza kwa ushindi mkubwa wa Kishindo aliyoupata katika uchaguzi Mkuu wa marudio,iliyocharazwa na Vikundi vya Culture Muzicul Club,BigStar na Zanzibar One.
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akisalimiana na Makamo wa Pili wa Rais Mstaafu wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi katika Ukumbi wa Salama Hotel ya Bwawani Mjini Zanzibar jana alipohudhuria katika Taarab rasmi ya kumpongeza kwa ushindi mkubwa wa Kishindo aliyoupata katika uchaguzi Mkuu wa marudio,iliyocharazwa na Vikundi vya Culture Muzicul Club,BigStar na Zanzibar One.
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein na Mkewe Mama Mwanamwema Shein (katikati) Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Mhe,Abdalla Mwinyi Khamis (kushoto) na Mama Asha Balozi (kulia) wakiangalia ratiba ya Taarab rasmi ya kumpongeza Rais kwa ushindi mkubwa wa Kishindo alioupata katika uchaguzi wa marudio,taarab rasmi iliyocharazwa na Vikundi vya Culture Muzicul Club,BigStar na Zanzibar One jana katika ukumbi wa Salama Hotel Bwawabi Mjini Unguja.
 Baadhi ya Viongozi na Wanachama wa Chama cha Mapinduzi CCM waliohudhuria katika taarab rasmi ya kumpomgeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein(hayupo pichani) kwa ushindi mkubwa wa Kishindo alioupata katika uchaguzi wa marudio,taarab rasmi iliyocharazwa na Vikundi vya Culture Muzicul Club,BigStar na Zanzibar One jana katika ukumbi wa Salama Hotel Bwawabi Mjini Unguja.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein na Mkewe Mama Mwanamwema Shein (katikati) Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Mhe,Abdalla Mwinyi Khamis (kushoto) na Mama Asha Balozi (wa pilikulia) na Mama Fatma Karume pamoja na Viongozi wengine wakiangalia Taarab rasmi ya kumpongeza Rais kwa ushindi mkubwa wa Kishindo alioupata katika uchaguzi wa marudio, Vikundi vya Culture Muzicul Club,BigStar na Zanzibar One ndio vilivyotoa burudani hiyo jana katika ukumbi wa Salama Hotel Bwawabi Mjini Unguja.
Msanii Makame faki (Sauti ya Zege) akiimba wimbo wa “Katumbukia Mwenyewe” wakati wa Taarab rasmi ya kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein kwa ushindi mkubwa wa Kishindo alioupata katika uchaguzi wa marudio, iliyocharazwa na Vikundi vya Culture Muzicul Club,BigStar na Zanzibar One jana katika ukumbi wa Salama Hotel Bwawabi Mjini Unguja.
Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein na Mke wa makamo wa Pili wa Rais Mstaafu Mama Asha Suleiman Iddi wakitunza wakati wa Taarab rasmi ya kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein kwa ushindi mkubwa wa Kishindo alioupata katika uchaguzi wa marudio, iliyocharazwa na Vikundi vya Culture Muzicul Club,BigStar na Zanzibar One jana katika ukumbi wa Salama Hotel Bwawabi Mjini Unguja.
Mwimbaji wa Rukia Ramadhan wa Zanzibar One akiimba wimbo unaosema”Kupata Majaaliwa”wakati wa Taarab rasmi ya kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein kwa ushindi mkubwa wa Kishindo alioupata katika uchaguzi wa marudio, iliyocharazwa na Vikundi vya Culture Muzicul Club,BigStar na Zanzibar One jana katika ukumbi wa Salama Hotel Bwawabi Mjini Unguja,[Picha naIkulu.]

Thursday, February 4, 2016

MAJAZ MODERN TAARAB YAJA KWA KISHINDO


Majaz Modern Taarab ambayo imekarabatiwa upya, inakuja na kete yake ya pili, safari hii ikiwa ni zamu ya Hamuyawezi Kondo na wimbo “Mshamba Haishi Kujigamba”. 


Wimbo huu unakuja wiki chache baada ya bendi hiyo kuachia ngoma inayokwenda kwa jina la “Penzi halina makombo” ya kwake Ashura Machupa. 

Katika wimbo huu wa Hamuyawezi Kondo aliyetamba huko nyuma na nyimbo kama “Kalieni Viti” na “Mtu Mzima Ovyo”, utasikia solo la Kisolo na kinanda cha Kalikiti Moto huku bass likipigwa na Mussa Mipango. 

Ni kazi iliyorekodiwa katika studio za Sound Crafters chini ya producer Enrico.