KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Tuesday, August 28, 2012

ISHA MASHAUZI: SIJAWAHI KUHUSIANA KIMAPENZI NA THABIT ABDUL AU MZEE YUSUPH



MWIMBAJI nyota wa muziki wa taarab nchini, Isha Ramadhani amesema hafikirii kuolewa kwa sasa kwa sababu lengo lake kubwa ni kukiimarisha kikundi chake cha Mashauzi Classic. Isha alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita alipohojiwa katika kipindi cha Mkasi kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha Channel Five. Makala hii ya ana kwa ana inaeleza mengi zaidi kuhusu mahojiano hayo kama yalivyonukuliwa na mwandishi wetu.
SWALI: Kwa nini wanawake wengi wanashindwa kudumu kwenye ndoa zao kwa muda mrefu?
JIBU: Si kweli kwamba wanaoshindwa ndoa, wanaume ndio wanaokuwa wakorofi.
Wakati mwingine ni wanawake wenyewe. Kila mmoja anakuwa na mtazamo wake.
Mi mwenyewe napenda kuolewa, lakini kwa sasa kutokana na kazi yangu, nimeona ni bora niimarishe bendi ndipo baadaye nifikirie suala la kuolewa, maana ndoa ni suala la majaliwa, unaweza kufikiria utaolewa, lakini kumbe usiolewe. Kwa hiyo baadaye naweza kufikiria kuolewa, lakini kwa sasa napumzika kidogo.
SWALI: Inawezekana hayo yote yametokea kwa sababu uliolewa mapema sana?
JIBU: Naweza kusema sikuolewa mapema sana kwa sababu sina ndoa moja. Nina ndoa mbili.
SWALI: Kwa maana hiyo inawezekana wewe ndiye unayetafuta bucha?
JIBU: Unajua kumpata mpenzi wa kweli ni sawa na kuingia kwenye pori kumsaka mnyama mkali, ambaye binadamu tunaogopa. Inategemea, unaweza ukabahatisha, lakini pia unaweza ukakosa. Lakini yote mawili yanawezekana, ni sawa na bahati nasibu. Ni sawa na kupapasa kizani, utakachoibuka nacho ndicho hicho hicho.
SWALI: Wanawake wengi maarufu huwa wameolewa, wakaachika ama wanakuwa na wachumba wengi sana. Hili likoje kwako?
JIBU: Mimi kwa upande wangu, naweza kusema wakati nilipoolewa kwa mara ya kwanza, nilikuwa sijulikani. Waliokuwa wananijua ni familia yangu na marafiki zangu na ndugu zangu. Nilipokuja kuolewa mara ya pili, nilikuwa najulikana, lakini kutokana na hitilafu zangu mimi na yeye, hatukuweza kudumu kwa muda mrefu.
Si kwamba niliachika kwa sababu ya umaarufu, la hasha au ukiwa maarufu unakuwa na wapenzi wengi, hapana. Naweza kukwambia kwa sasa nina mpenzi mmoja, huwezi kuamini, lakini ni ukweli kutoka moyoni mwangu. Nampenda ananipenda, namjali ananijali.
Wapo wanaosumbua kwa sababu wapo wanaokuja kwa nia nzuri, anaomba namba yako ya simu, anasema oooh, nitakuhitaji, lakini mwisho wa siku anakusumbua, oooh nakupenda, ooh kila ninapokuona kwenye TV, napenda kukuona vile kama unavyocheza, lakini tuwe wawili tu.
Lakini hayo yote yanategemea na wewe mwenyewe, ukiwa na tamaa, ukiona ana chapaa, unajikuta unakwenda, lakini kwa mtu kama mimi sidhani kama ninayo tamaa ya pesa kwa sababu mimi mwenyewe najua kutafuta.
SWALI: Kuna mtazamo kwamba mwanamke anapomiliki bendi, lazima kunakuwa na mwanaume nyuma yake, ambaye ndiye anayemuunga mkono. Kuna ukweli wowote kuhusu msemo huu?
JIBU: Hicho kitu sikikatai, inawezekana kabisa kipo kwa sababu haiwezekani mtu kuja kuwekeza kwako bila sababu maalumu, inawezekana kabisa mtu akaja kuwekeza kwako kwa sababu maalumu, akijua kuna kitu ambacho atakipata.
SWALI: Hivi asili yako hasa ni wapi kwa sababu ulivyo, unaonekana kuwa ni mtanzania, lakini umechanganya marashi fulani. Hebu tueleze kwenu hasa ni wapi?
JIBU: Mimi na taarabu ni vitu viwili tofauti, lakini yote haya ni kwa sababu ya kutafuta maisha. Mimi hasa chimbuko langu kwa wazazi wangu, hasa upande wa baba, wametokea Burundi. Kwa hiyo mimi jina langu halisi, ambalo linatambulika katika ukoo, naitwa Mlundi.
Kwa hiyo baada ya wazazi wetu kutoka kule Burundi, wakawa wanaishi Tanzania. Ndio sababu najiita mkuria wa kwanza kuimba taarabu. Kwa hiyo Musoma ndiko hasa nilikokulia, lakini kiasili hasa, mimi siyo mtu wa Musoma, asili ya wazazi wangu ni Burundi.
Baada ya hapo, wazazi wangu wakaamua kuhamishia maisha yao Dar es Salaam. Ni kuanzia hapo, nilisoma Dar es Salaam na kukulia Dar es Salaam. Kwa hiyo hata kuolewa, niliolewa Dar na walionilea, baadhi yao ni watu wa Pemba.
Mama yangu alikuwa msanii, kwa hiyo kila alipokuwa akitoka, tuseme saa mbili usiku, alikuwa akiniacha kwa majirani zetu, ambao wengi walikuwa Wapemba, ndio sababu na mimi nilikuwa naitwa Mpemba kwa sababu hata lafudhi yangu ilikuwa kama ya kwao, lakini mimi si mpemba hata kidogo, sihusiki nao kwa lolote.
SWALI: Kwa hiyo ile stori kwamba wewe na Mzee Yusuph ni ndugu haina ukweli wowote?
JIBU: Hapana, mimi na Mzee Yusuph hatuna undugu wowote.
SWALI: Kwa nini muziki wa taarab unaitwa mipasho?
JIBU: Ni kwa sababu tunaimba vitu, ambavyo ni vya kweli, ndio maana wakaita mipasho, ingawaje mtu akisikia wimbo ukiimbwa, anadhani kaambiwa yeye, ndio sababu wanasema anayejishuku, hajiamini.
SWALI: Kwa nini unaitwa Mashauzi? Una dharau sana?
JIBU: Mimi nasema anayenizungumzia, mara nyingi anakuwa hanitambui. Mimi ni mtu ambaye napenda sana kucheka na watu, napenda kutaniana na watu, naweza nikafika sehemu, watu wasiponiona, labda siku mbili au tatu, wanaweza kunipigia simu wakaniuliza, inakuwaje mbona hatukuona? Isha tumekumiss sana, hebu njoo mahali fulani. Kwa hiyo mtu anayenizungumzia kwa mwelekeo huo, hanijui kiundani.
SWALI: Hivi wewe huwa unaandika maishairi ya muziki?
JIBU: Unajua unaweza kukaa na mtu mahali, lakini huwezi ukajua hisia zake zikoje. Wewe unaweza kuzungumza kitu, lakini hujui kwamba hicho kitu mimi kimenigusa. Kwa hiyo ninapoona hivyo, namtumia ujumbe mkurugenzi wangu, ambaye ni Thabiti Abdul na kumweleza kwamba kuna mtu amezungumza kitu hiki na kile kimenigusa sana, naomba unitungie mashairi na yeye atafanya hivyo.
Kwa mfano, kuna wakati tulipokuwa tumekaa pale nje, kuna mtu alisema neno kuhusu mimi, nikamwambia kama nimekukera, hama mji. Inapokuwa hivyo, namweleza mkurugenzi wangu kwamba kuna hiki na kile na yeye anaandika, anaweka muziki na sauti, nyimbo inakuwa imekamilika. Baadaye ananifuata na kuniambia wimbo umekamilika kwa hiyo kazi yangu inakuwa ni kuweka vikorombwezo vya chini. Mara nyingi hivyo huwa vinatoka kichwani.
SWALI: Taarabu ina mashabiki wengi sana, lakini mara nyingi wanakuwa wale, ambao mwonekano wao ni tofauti na wengine na kwa wanawake, inakuwa ni wale, ambao wameshindikana katika familia zao. Kwa nini inakuwa hivyo?
JIBU: Hakuna uhusiano isipokuwa vile vitu vinavyoimbwa, wao ndio wanakuwa wanapenda. Wanakuwa wanapenda kupashana, kuchambana, labda niseme hivyo.
Lakini nikirudi kwenye swali la awali, si watu wote wanaopenda taarabu wanakuwa ni watu walioshindikana. Sasa hivi naweza kusema kwamba taarabu inapendwa hata na akina baba, ambao ni marijali, wanapenda watoto, wanapenda wasichana, utakuta mtu anakwenda klabu huku akiwa anamjua mwimbaji taarabu.
Zamani wanaume walikuwa wanahisi kwamba mwanamke akipenda taarabu, huenda ni shangingi na vivyo hivyo mwanaume akipenda taarabu, alikuwa akionekana namna gani vipi.
SWALI: Hivi inakuwake mwanaume, ambaye namna gani vipi anaweza kuwachukua shoga zake wa kike wanne au hata watano, akajiweka katikati yao na kucheza kama vile naye ni mwanamke ama shughuli ni ya kwake. Inakuwaje kitu kama hicho kinatokea?
JIBU: Niseme tu kwamba, awali ya yote namshukuru Mungu kwamba sisi wanawake bado tunaendelea kuzaa. Lakini huwa nasikia uchungu sana ninapoona kitu kama kile, lakini huwezi kusikia uchungu, ukamfuata mtu na kumweleza acha maana jibu atakalokupa, ukirudi nyumbani unaweza kutafuta maji ili ushushie.
Wale ni watu ambao wanakuwa wameshaamua kuishi maisha ya aina fulani. Kuna wengine ukionyeshwa na kuambiwa huyu ni dizaini fulani, unaweza kukataa.
SWALI: Mara ya mwisho kulia ilikuwa lini?
JIBU: Siku kama nne hivi zilizopita.
SWALI: Nini hasa kilitokea?
JIBU: Naweza kusema ni sababu ya mapenzi.
SWALI: Unataka kusema ni maumivu? Ulilizwa?
JIBU: Hapana hapana, unajua wakati mwingine furaha nayo inaweza kuleta kilio. Lakini sikulia kwa kuumizwa, nililia kwa kujiumiza kwa maana kwamba nilipatwa na kitu kama wivu fulani hivi.
SWALI: Kuna wasanii fulani wa kundi la taarab la Five Stars walipata ajali ya barabarani kule Morogoro mwaka jana. Ulijisikiaje baada ya kupata taarifa hizo?
JIBU: Ukweli ni kwamba kila chenye roho lazima kitaonja mauti, lakini mauti yanapomfika mtu wa karibu yako, huwa yanaumiza sana, na hasa ukikumbuka ajali yenyewe jinsi ilivyotokea, ni kitu ambacho tunapaswa kumshukuru Mwenyezi Mungu.
Binafsi siwezi kusema kwamba nilishuhudia, lakini nilikuwa mmoja kati ya watu wa mwanzo kupata taarifa za ajali ile kuliko watu wengine. Ah, inasikitisha sana.
SWALI: Kuna taarifa kwamba matiti yako yametengenezwa na wachina na wewe ulikuwa mtu wa mwanzo kuyatengeneza. Je, kuna ukweli wowote kuhusu taarifa hizo?
JIBU: Asante sana kwa swali lako. Naweza kusema kwamba, huyo mchina mwenyewe mimi huwa nakutana naye barabarani. Mimi nilivyo ndivyo jinsi nilivyoumbwa na Mungu. Kama nimejaaliwa au vinginevyo, siwezi kujua. Lakini sijawahi kwenda mahali popote kuomba ama kutaka umbo langu liboreshwe.
Sijui huyo aliyeandika kwenye gazeti kwamba aliniona au vipi au aliamua tu kufanya hivyo ili auze gazeti lake, lakini sijawahi kufanya kitu kama hicho kwa sababu mimi ni mtoto wa kiislamu na dini yetu inazuia kufanya kitu kama hicho.
SWALI: Unazungumziaje kuhusu masuala ya dini na muziki? Unadhani dini yako inaruhusu wewe kujishughulisha na muziki?
JIBU: Kazi ya muziki ni kazi kama zilivyo kazi zingine, lakini si mbaya mtu kama mimi nikipata muda wakati mwingine kujihusisha na muziki kwa sababu siku zote, kabla sijapanda jukwaani, huwa namuomba Mungu kwa maana hiyo, ukimkumkuka Mungu, siku sote ndivyo atakavyozidi kukujalia na kukuwezesha kufanikiwa katika mambo yako.
SWALI: Hivi jina la Mashauzi limetokea wapi?
JIBU: Jina hilo limetokana na mashabiki. Zamani nilikuwa najulikana zaidi kwa jina la Mama Afrika kwa sababu nilikuwa napenda sana kuvaa kiafrika. Nilipokuwa nikienda kwenye kitchen part, nilikuwa najulikana zaidi kwa jina hilo kwa sababu wakati huo nilikuwa nafanyakazi kama MC.
SWALI: Kwa maana hiyo, kabla hujaanza kuimba ulikuwa MC?
JIBU: Ni kweli kabisa kwamba kabla ya kuanza kuimba taarabu nilikuwa MC. Ilikuwa miaka hiyo kabla sijaanza kuganga njaa.
SWALI: Kila mtu anajijua thamani yake, wewe binafsi unaijua thamani yako?
JIBU: Ni kweli, kwa sasa naijua thamani yangu kwa sababu nilivyokuwa huko nyuma sio sawa na nilivyo hivi sasa.
SWALI: Kwa hiyo thamani yako huwa unaiona?
JIBU: Thamani naiona kwa sababu bila ya wewe mwenyewe kuiona thamani yako, hakuna mtu mwingine anayeweza kuiona.
SWALI: Bangi vipi? Nasikia ndio zako hizo (kuvuta)?
JIBU: Hicho kitu mimi situmii kabisa. Katika vitu ambavyo sijawahi kukifanya ni kuvuta bangi. Muziki mimi upo kwenye damu kwa hiyo siwezi kuunogesha kwa kitu chochote zaidi ya kusema naanza kwa kutaja jina la Mwenyezi Mungu na sasa nakwenda kazini.
SWALI: Gari lako la kwanza kumiliki lilikuwa la aina gani?
JIBU: Gari langu la kwanza lilikuwa Lexas. Ukweli hiyo ni ndoto kubwa niliyokuwa nayo kwa sababu mimi huwa sipendi kitu cha kununuliwa kwa sababu mtu anaweza kukufanyia hivyo, baadaye akaja na kukueleza kitu kingine.
Sasa ikitokea mtaani watu wameshazoea kukuona na kitu fulani, halafu baadaye hicho kitu huna, utakuwa huna mahali pa kuuweka uso wako.Nilikaa na gari hiyo kwa muda wa kama mwaka mmoja na miezi mitatu hivi.
SWALI: Ni kweli kwamba wasanii wa taarab, hasa wa kike wana tabia ya kutembea na waume za watu?
JIBU: Unajua mapenzi ni kitu, ambacho hakiingiliwi. Na mapenzi ni siri, ingawaje sasa hivi imekuwa dhahiri na ndio sababu baadhi yetu tumekuwa tukishutumiwa kwamba unatembea na mume wa mtu, lakini kama tungekuwa tunafanya siri, sidhani kama kuna mtu angekuja kugundua hicho kitu. Kila mtu anataka ajionyeshe kwamba mimi nilikuwa natembea na fulani.
SWALI: Kuna kipindi ulishutumiwa kwa kutimua wasanii wote wa kike kwenye kikundi chako na stori iliyozagaa mjini ni kwamba ulikuwa na uhusiano wa kimapenzi na Thabiti Abdul. Hebu tueleze mahusiano yako na Thabiti, kuna ukweli wowote kuhusu hilo?
JIBU: Usinione nacheka, nafanya hivyo kwa sababu umeniambia nifunguke. Mimi Thabiti sina mahusiano naye yoyote zaidi ya kazi. Nimemtambua Thabiti miaka mingi iliyopita. Alianza kazi ya sanaa siku nyingi, tangu mimi nikiwa mdogo. Mimi ni mdogo sana kwa Thabiti. Nilikuwa nikimuona akifanyakazi na mama yangu na sehemu nyingine.
Mwaka 2009 wakati nikiwa Jahazi, baada ya kuona mambo yanakwenda longo longo ama mrama, nikaamua kutengeneza albamu yangu mimi kama mimi. Nilianza kushirikiana na watu kama akina Ally J, Fikirini pamoja na Mussa, lakini baadaye nikasema hata, wacha nimshirikishe na huyu mtu ili niweze kupata kitu kizuri zaidi. Ndipo hapo nilipoanza mahusiano ya kikazi na Thabiti Abdul.
Ikaenda hivyo kwa muda mrefu, lakini waswahili wanasema kila mtu na mtuwe ama kila shetani na mbuyu wake. Jinsi tulivyokuwa tumeshibana kikazi, ndivyo watu walivyoanza kututafsiri kivingine. Unajuwa hakuna kitu kizuri kama unapomuelekeza mtu kitu, akaweza kukifanya vile unavyotaka ama kufundisha mtu, lakini akawa haelewi. Kila alichokuwa akikifanya, mimi nilikuwa naelewa. Vile vitu vikamfanya anielewe ndipo tukashikana mpaka kumaliza albamu yangu ya kwanza.
Kamwe hatujawahi kuunganisha viungo vyetu vya uzazi kwa sababu kila mmoja anaye wa kuunganisha naye. Lakini ndio hivyo tena, stori zimeshaenea mjini, lakini nilishawahi kusema kwamba, hakuna kitu chochote kinachoendelea kati yangu mimi na Thabiti.
SWALI: Huko nyuma ulikuwa katika kikundi cha Jahazi kinachoongozwa na Mzee Yusuph, lakini baada ya kutokea purukushani, ukaamua kuanzisha bendi yako na sasa upo na Thabiti, mnafanya kazi kama wakurugenzi. Kitu gani kilitokea kati yako na Mzee Yusuph?
JIBU: Hakuna kitu chochote kibaya kilichotokea kati yangu na Mzee Yusuph. Wakati naanza kufanya zing zong, nilimwambia nahitaji kufanya kitu fulani kutokana na majukumu yaliyonibana na akaniambia sawa. Nikaanza kutengeneza albamu zangu.
Nilipoanza kutengeneza albamu ya pili, ndipo nilipoanza kuona utamu wa vimeo. Ilikuwa kila nikipita huku na kule, naulizwa wewe ndiye Isha Ramadhani, tunakuomba siku fulani tuna kitchen party, uje kutumbuiza. Tunataka ile mama nipe radhi, na nikienda huko naulizwa tukupe shilingi ngapi, wakati mwingine nilipotaka kiasi kidogo cha pesa, waliniongeza, oooh tutakupa shilingi laki mbili.
Kwa hiyo ikafika kipindi nikasema hebu wacha nijaribu, lakini nikaona kwa nini nijaribu, bora nithubutu, kwa kweli nikaweza na sasa nasonga mbele.
SWALI: Kwa hiyo wewe na Mzee Yusuph hamna uhusiano wowote wa kimapenzi?
JIBU: Kusema ule ukweli, Mzee Yusuph ni kama baba yangu, ingawaje kuna watu huwa wanapenda kutuona tukigombana, lakini mimi siwezi kuwa mjinga kiasi hicho. Namshukuru hata yeye mwenyewe ananielewa mimi ni nani na ninataka kufanya nini.
SWALI: Kitu gani kinachokufurahisha katika maisha yako? Dhahabu, maisha mazuri, matiti yako kusimama vizuri kifuani au nywele? Ni kipi kinachokufanya uwe na furaha?
JIBU: Kitu kinachonifurahisha katika maisha yangu ni kuwa na furaha na yule ninayempenda na pia niwe na furaha na familia yangu, nisiwaudhi wazazi wangu wote wawili, bila wao mimi nisingekuwepo, wangeweza kuninyonga miaka mingi iliyopita. Napenda sana kuwa na furaha kila wakati ndio maana huwa sipendi kujiudhi.

No comments:

Post a Comment