KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Saturday, August 11, 2012

MARIAM KHAMIS: SIJAPOTEA NJIA KUJIUNGA NA TOT

MWIMBAJI nyota wa taarab nchini, Mariam Khamis amesema hajapotea njia kutokana na uamuzi wake wa kujiengua kutoka katika kundi la Five Stars Modern Taarab na kujiunga na kundi la Tanzania One Theatre (TOT).
Mariam alisema mjini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita kuwa, uamuzi wake huo umelenga kutafuta maslahi bora zaidi na pia kujiandaa kwa maisha yake ya baadaye.
Alisema hakuondoka Five Stars kwa kufukuzwa bali alifanya hivyo kwa hiari yake mwenyewe kwa vile maisha ni kutafuta na ahangaikaye siye sawa na mkaa bure.
“Unajua linapotokea jambo, huwa yanasemwa mengi, lakini huo ndio ukweli wenyewe,”alisema.
Mariam, ambaye aliwahi kutamba kwa kibao chake cha ‘Paka mapepe’ alisema, ameamua kujiunga na TOT kwa sababu ajira yake ni ya uhakika tofauti na vikundi vingine.
Alisema wasanii wote wanaounda kundi la TOT hawategemei mapato ya milangoni kulipana mishahara na hata wasipofanya maonyesho, malipo yao kwa mwezi yapo palepale.
Tayari mwimbaji huyo mwenye sauti maridhawa, ameshatungiwa wimbo unaojulikana kwa jina la ‘Sidhuriki kwa lawama’, na unatarajiwa kuanza kusikika hewani hivi karibuni.
“Nawaomba mashabiki wangu wasichukie kwa sababu maisha ni kutafuta, wakubali matokeo,”alisema.
Mwimbaji huyo mwenye sura yenye mvuto alikiri kuwa, tangu alipojiunga na TOT, yamesemwa mengi juu yake, lakini hajali na anayachukulia kama changamoto katika maisha yake.
“Wengine wanasema nimekwenda TOT kujimaliza kiusanii, wengine wanasema nitakufa, lakini mimi sijali. Tangu nilipozaliwa, nilishatia saini mbele ya Mungu kwamba nitakufa siku fulani,”alisema.
Alisisitiza kuwa, ili msanii aweze kukomaa kiusanii, anapaswa kutembea katika vikundi mbalimbali kama ilivyo kwa waimbaji nyota wa muziki huo, Khadija Omar ‘Kopa’, Sabah Salum na wengineo.
“Hata mimi utafika wakati nitakuwa hivyo na kuamua kutulia kama wakongwe hao,”alisisitiza.
Mbali na kuimbia kundi la Five Stars, Mariam pia aliwahi kung’ara alipokuwa katika vikundi vya East African Melody na Zanzibar Stars.Baadhi ya vibao alivyotamba navyo katika vikundi hivyo ni pamoja na ‘Huliwezi bifu’, ‘Raha ya mapenzi’ na ‘Ndo basi tena’.

No comments:

Post a Comment