KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Monday, August 20, 2012

MAALIM SEIF AMTEMBELEA BI KIDUDE

Na Khamis Haji, OMKR
MSANII mkongwe hapa nchini Fatma Baraka Khamis ‘Bi Kidude’, amewajia juu baadhi ya watu walioeneza uvumi kwamba amefariki dunia.
Bi. Kidude amesema anasikitishwa sana na kitendo hicho cha kuzushiwa kifo wakati bado ni mzima na anafanya shughuli zake kama kawaida.
Msanii huyo alitoa ya moyoni jana, wakati akizungumza na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad, wakati alipomtembelea nyumbani kwa mwanawe huko Kihinani, Wilaya ya Magharibi, ikiwa ni katika ziara zake za kuwatembelea wazee mbalimbali wanaosumbuliwa na maradhi.
Alisema kuwa, kitendo cha watu hao licha ya kumsikitisha yeye binafsi, pia kimesababisha usumbufu na hofu kubwa miongoni mwa jamii na baadhi ya watu ambao walilazimika kufunga safari kuja Zanzibar kutoka nchi mbalimbali.
“Kuna watu wameeneza taarifa za uongo kwamba nimekufa, wapo watu waliofunga safari kutoka nchi tafauti kuja Zanzibar, lakini walipofika walishangaa kuniona nipo hai”, alisema msanii huyo maarufu wa muziki wa taarab hapa Zanzibar na Afrika Mashariki.
Bi. Kidude alieleza kuwa anasumbuliwa na maradhi ya miguu, lakini amekuwa akifanya shughuli zake nyingi za kawaida.
Katika ziara yake ya kuwatembelea wagonjwa na watu wazima iliyoanza juzi, pia aliwafariji, mzee Khamis Makungu wa kijiji cha Ndijani, mzee Abdulrazak Mukri wa Mkunazini, mzee Ali Haji Pandu wa Mpendae na Sheikh Habib Ali Kombo wa Kiembesamaki.

No comments:

Post a Comment