KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Saturday, August 11, 2012

KHADIJA YUSUPH:SINA UGOMVI NA MZEE YUSUPH

MWIMBAJI nyota wa muziki wa taarab nchini, Khadija Yussuf ameanika hadharani sababu za kuondoka kwake katika kundi la Jahazi Modern Taarab, linaloongozwa na kaka yake, Mzee Yussuf.
Akizungumza mjini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita, Khadija alisema alijiengua katika kundi hilo kwa sababu ya maslahi duni si vinginevyo.
Khadija alisema si kweli kwamba aliondoka katika kundi hilo kutokana na kushindwa kuelewana na Mzee, hasa katika mambo ya maslahi.
Mwanamama huyo tipwatipwa alijiengua katika kundi la Jahazi mwaka mwishoni mwa mwaka jana na kujiunga na kundi jipya la Five Stars Modern Taarab.
"Sina ugomvi wowote na Mzee, yeye ni kaka yangu, tunaheshimiana sana na tunaelewana sana, lakini nilihama katika kundi lake kutokana na uchache wa maslahi," alisema.
Mwimbaji huyo anayependwa na mashabiki wengi kutokana na sauti yake maridhawa alisema, yupo tayari kufanya maonyesho na kaka yake iwapo atatakiwa kufanya hivyo.
Alisema tangu ajiunge na kundi la Five Stars, linaloongozwa na Ally Jay, mambo yake yamekuwa mazuri na hana matatizo kama alivyokuwa Jahazi.
"Hivi sasa mambo yangu yanakwenda vizuri, tofauti na nilipokuwa Jahazi, namshuruku Mungu malengo yangu yametimia," alisema.
Khadija aliwahi kutamba kwa vibao vyake vitamu kama vile Mkuki kwa Nguruwe, Zilipendwa, Hayanifiki, Hamchoki kusema, Riziki mwanzo wa chuki.
Alikiri kwamba kibao kilichompandisha chati na kumpatia umaarufu mkubwa ni Mkodombwe, alichokiimba wakati akiwa katika kundi la East African Melody.
Khadija alisema kwa sasa anajipanga upya kabla ya kuibuka na kibao chake kipya kitakachojulikana kwa jina la Ukisema cha nini.
"Ninawaahidi mashabiki wangu wakae mkao wa kula kwani niko mbioni kuachia tungo yangu mpya, ambayo bila shaka itakuwa gumzo hapa nchini," alisema.

No comments:

Post a Comment