KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Saturday, August 11, 2012

LEILA: SIONI TATIZO KUFANYAKAZI NA MUME WANGU


“NILIANZA kumfahamu Mzee Yusuf katika ukumbi wa Equator Grill uliopo Mtoni kwa Azizi Ally, Temeke, Dar es Salaam. Nilipenda sana jinsi alivyokuwa anapiga kinanda wakati huo, ” anasema mwimbaji nyota wa taarab wa kundi la Jahazi, Leila Rashid.
Anasema kipindi hicho alikuwa akihudhuria maonyesho mbalimbali yaliyokuwa yakifanywa na kikundi cha taarab cha Zanzibar Stars, ambacho Yusuf alikuwa mmoja wa wasanii wake, akiwa anapiga kinanda.
Leila, ambaye alikuwa na ndoto ya kuwa mwimbaji tangu akiwa mdogo anasema, alikuwa na kawaida ya kwenda kwenye ukumbi huo kila Zanzibar Stars ilipokuwa ikifanya onyesho.
“Nilikuwa na ndoto ya kuimba taarab tangu nilipokuwa mdogo na nilikuwa nikivutiwa sana na uimbaji wa Sabah Salum ‘Muchacho’ kutokana na uimbaji wake mzuri,” anasema.
Leila anasema alikuwa akitumia muda mwingi akiwa nyumbani kwao kuimba nyimbo mbalimbali za waimbaji nyota wa muziki huo kwa lengo la kupima uwezo wake kama anaiweza fani hiyo.
Mwimbaji huyo mwenye sura na umbo la kuvutia, ambaye wajihi wake unashabihiana na mwanamke wa kisomali, anasema siku ya kwanza kuanza kufahamiana na Yusuf, alijihisi mwenye furaha kubwa.
“Kwa kweli siku ya kwanza kufahamamiana na Yusuf nilijihisi mwenye furaha sana na niliamini ataweza kunisadia kukuza kipaji changu cha uimbaji nilichokuwa nacho,” anasema.
Baada ya kufahamiana na kuwa karibu na Yusuf, Leila anasema mwimbaji huyo gwiji wa taarab alimshawishi ajiunge na kikundi cha Zanzibar Stars, ambacho kilikuwa kikiwika wakati huo.
Leila, ambaye kwa sasa anasikika kila kona ya nchi kutokana na uimbaji wake mzuri, anasema ushauri aliopewa na Yusuf aliusikiliza na kuufanyia kazi.
Anasema alijiunga na Zanzibar Stars miaka tisa iliyopita na wimbo wake wa kwanza ndani ya kikundi hicho unajulikana kwa jina la ‘Riziki atoae Mola’.
Mwimbaji huyo mwenye bashasha anasema, baada ya kurekodi wimbo huo, hakufanikiwa kutoa wimbo mwingine kutokana na ubinafsi uliokuwepo katika kundi hilo.
Anasema mara yake ya kwanza kupanda kwenye steji alikuwa na hofu, lakini alifanikiwa kuimba vizuri na kushangiliwa na mashabiki wengi.
Leila, mwimbaji mwenye sauti nyororo na macho ya kuvutia anasema, aliamua kuondoka Zanzibar Stars kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo ubinafsi na uchache wa maslahi.
Anasema licha ya kwamba kipindi hicho Zanzibar Stars ilikuwa inatamba kwa nyimbo za taarab, maslahi yalikuwa madogo, hali iliyosababisha waimbaji wengi mahiri kuhama.
Mwimbaji huyo anasema, mwaka 2006 alijiunga na kundi jipya la Jahazi Morden Taarab ‘Wana wa nakshinakshi’ chini ya Mkurugenzi wake Mzee Yusuf.
Anasema kuanzishwa kwa kundi hilo, ambalo linaongozwa na mume wake, Yusuf kulimfanya afahamike ndani na nje ya nchi hii.
“Jahazi ndiyo imenifanya nifahamike kila kona ya nchi hii, nadhani kama si kundi hili, hadi sasa ningekuwa sifahamiki,” anasema.
Leila anasema wimbo wa ‘Maneno ya mkosaji’, ambao ulikuwa wa kwanza kuimba katika kundi hilo, ulimpandisha chati na kumpa umaarufu mkubwa na kusisitiza kuwa, kwa sasa anajiona yupo kwenye chati ya juu.
“Sidhani kama kuna mwimbaji anayeweza kujaribu kusimama na mimi kwa sasa, niko juu na nimeiva kila idara,” anajigamba mwimbaji huyo.
Akizungumzia maendeleo ya muziki wa taarab nchini, Leila anasema upo juu na unazidi kukua kadri siku zinavyosonga mbele kutokana na kuwa na mashabiki wengi zaidi.
Mwimbaji huyo, ambaye ni mama wa watoto wawili anasema, haoni tatizo kufanyakazi katika kundi moja na mumewe kwa sababu ameshaizoea tabia ya mumewe.
Leila anasema ataendelea kuheshimiana na mume wake kwa kipindi chote watakachoendelea kuwa pamoja huku akisisitiza kuwa, hakuna anayeweza kuwatenganisha kwa vile anampenda kuliko kitu kingine chochote.
“Nampenda sana mume wangu ndio maana hata anapotaka kuoa mke mwengine, huwa nampa ruksa kwani najua kufanya hivyo ni sheria kwa mujibu wa dini yetu,” anasema.
Hata hivyo, mwimbaji huyo anayependa kutabasamu muda wote anasema, hafurahishwi kuona Yusuf na mdogo wake Khadija, ambaye ni mwimbaji wa kundi la Five Stars Modern Taarab wametofautiana.
Anasema ni vyema wanandugu hao wawili waishi kama awali na waendelee kufanyakazi katika kundi moja kwa vile kugombana kwao hakutoi sura nzuri mbele ya jamii.
Leilah, ambaye kwa sasa anatamba na wimbo wa ‘Ubinadamu kazi’, anasema kupitia fani hiyo, ameweza kusafiri katika mikoa mingi nchini na pia nje ya nchi. Alizitaja baadhi ya nchi alizowahi kutembelea kuwa ni Uingereza, Oman, Dubai, Nairobi na Burundi.
Mwimbaji huyo amekitaja kibao cha ‘Kwa hilo hujanikomoa’ kuwa ndicho kilichomfanya apendwe zaidi na mashabiki kutokana na kukiimba kwa umahiri mkubwa.
Ametoa mwito kwa serikali kuwasaidia waimbaji wachanga ili waweze kuonyesha vipaji vyao. Pia amewataka wasanii wenzake wa muziki huo, kuwa na upendo na kuacha majungu miongoni mwao.

No comments:

Post a Comment