KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Sunday, August 13, 2017

WASANII WANANE JAHAZI WATIMKIA WAKALI WAO MODERN TALADANCE

THABITI Abdul
KHADIJA Yussuf
AISHA Vuvuzela
JUMANNE Ulaya
RAHMA Machupa

HATIMAYE kikundi cha muziki wa taarab cha Jahazi, kimesambaratika baada ya wasanii wake zaidi ya wanane, kuhama na kujiunga na kikundi cha Wakali Wao Modern Taladance.

Habari kutoka ndani ya Jahazi zimeeleza kuwa, uamuzi wa wasanii hao kuhama, umelenga kuheshimu matakwa ya kiongozi wa zamani wa kundi hilo, Mzee Yussuf, kutaka jina hilo lisiendelee kutumika.

Kwa mujibu wa habari hizo, Mzee Yussuf aliwaeleza wasanii wa kundi hilo kuwa, kuendelea kutumia jina la Jahazi ni sawa na kuendelea kumshirikisha na dhambi wakati alishatangaza kuachana na muziki wa taarab na kumrudia Mungu.

Miongoni mwa wasanii wa Jahazi, waliojiunga na Wakali Wao Modern Taladance ni pamoja na Khadija Yussuf, Rahma Machupa, Aisha Vuvuzela, Mwasiti, Miriam, Mgeni Kisoda, Jumanne Ulaya na Mohamed Ali 'Mtoto Pori'.

Akihojiwa na Uhuru mwishoni mwa wiki, Khadija alikiri kuondoka kwake Jahazi, akiwa amefuatana na wasanii wengine kadhaa.  Alisema wamefikia uamuzi huo kwa sababu kuendelea kwao kuwepo Jahazi ni kuzidi kumpa dhambi kaka yake, Mzee Yussuf.

"Jahazi ilikuwa Mzee Yussuf. Kwa vile ameamua kumrudia Mungu, tuliona ni bora kikundi kivunjwe ili kuepuka kumshirikisha katika dhambi,"alisema.

Aliongeza: "Nimeondoka Jahazi na kijiji changu. Mfalme Mzee Yussuf alikuwa ndiye kila kitu. Ameondoka na sasa hakuna wa kuiongoza."

Khadija alisema hajutii uamuzi wake huo kwa sababu yeye na wenzake wanajiamini kikazi na watashirikiana vyema na wenzao waliowakuta Wakali Wao kuupaisha muziki wa taarab.

"Mashabiki wetu watarajie makubwa kutoka kwetu kwa sababu ukali wetu ni ule ule, hatujatetereka kimuziki,"alisisitiza mwanamama huyo, ambaye amewahi kuimbia vikundi vya East African Melody na Zanzibar Stars.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Wakali Wao Modern Taladance, Thabiti Abdul, alithibitisha kuwepo kwa muungano kati ya vikundi hivyo viwili.

Thabiti alisema awali, uongozi uliokuwa umebaki Jahazi, baada ya Mzee Yussuf kuachana na muziki, ulimfuata na kumuomba ajiunge na kikundi hicho akiwa ndiye mkurugenzi mkuu.

"Lakini baada ya majadiliano ya muda mrefu kati yetu, ikaonekana ni vizuri wasanii waliokuwa Jahazi waje kwangu ili tuwe kitu kimoja kwa kuwa mwenye bendi yake alikuwa hataki jina hilo liendelee kutumika,"alisema.

Thabiti, ambaye ni mmoja wa wapiga kinanda maarufu nchini, akitokea bendi ya Twanga Pepeta International, alisema lengo la muungano wao, ambao wameuita kwa jina la 'Mbili kwa moja', ni kuendeleza muziki wa taarab.

"Niliukubali mpango huu kwa sababu baada ya Mzee Yussuf kujitoa, Jahazi ilikuwa kama imekufa. Japokuwa ilikuwa ikiendelea na maonyesho, haikuwa Jahazi iliyozoeleka,"alisema.

Thabiti alisema mikakati waliyonayo ni kuhakikisha Wakali Wao, kinakuwa kikundi bora na maarufu katika muziki wa taarab nchini kama ilivyokuwa Jahazi enzi za Mzee Yussuf.

"Hakuna kushindwa, tunataka tushinde. Lazima tufike kule ilikokuwa Jahazi,"alisisitiza msanii huyo, ambaye pia ni mtunzi mahiri wa nyimbo za muziki huo.

Kwa mujibu wa Thabiti, katika maonyesho yao, watakuwa wakiimba nyimbo zote za Jahazi, zilizoimbwa na wasanii waliopo kwenye kikundi hicho, akiwemo Khadija Yussuf.

Thabiti alisema kikundi pekee kilichokuwa kikimuumiza kichwa kilikuwa Jahazi, lakini kwa kuwa hakipo, haoni kikundi kingine kitakachomsumbua.

"Mimi na Mzee Yussuf ndio tuliokuwa tukisumbuana. Hata kwenye tuzo za wasanii bora wa muziki wa taarab, tulikuwa tukibadilishana kuzinyakua. Kwa hiyo naweza kusema kuwa, kwa sasa nimebaki peke yangu,"alisema.

Thabiti alisema kwa kuwapata wapiga ala mahiri, kina Mgeni Kisoda, Jumanne na waimbaji kina Khadija, Rahma Machupa, Mwasiti, Miriam na Mtoto Pori, anaamini Wakali Wao itakuwa kwenye matawi ya juu.

Naye Mtoto Pori alisema yeye na wasanii wengine wote kutoka Jahazi, waliojiunga na Wakali Wao, wamefanya hivyo kwa moyo safi, bila kushawishiwa na mtu.

"Tuliona kwa kuwa mwanzilishi wa kikundi hataki jina lake liendelee kutumika, tusiendelee kumbebesha dhambi. Tuliangalia upepo, tukaona ni bora tuondoke,"alisema mwimbaji huyo machachari.

Aliongeza: "Pia, tuliona hakuna anayependa kuwa masikini kwa sababu ni kitu kibaya. Unaamka asubuhi, hujui wapo pa kwenda."

Utambulisho wa wasanii hao wapya ndani ya Wakali Wao Modern Taladance, umepangwa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu, kwenye ukumbi utakaotangazwa baadaye.


 

Sunday, June 25, 2017

EID MUBARAKA WASOMAJI WANGU WAPENZI WA BLOGU YA RUSHAROHO


EID MUBARAK



Mikono tupeane
Rehema tutakiane
Upendo tushikamane
Toba tuhimizane
Makosa tusameheane
Yarabi tupe baraka zako
Utukubalie swaumu zetu
Amina yarabi Amina

KHADIJA: SIKUKATAA KUMPA MKONO LEILA WAKATI WA MSIBA. ASEMA HUO NI UZUSHI, MZEE YUSSUF ASIMULIA KILICHOTOKEA



MWIMBAJI  nyota wa muziki wa taarab nchini, Khadija Yussuph, amekanusha madai kuwa alikataa kupeana mkono na mke mkubwa wa kaka yake, Leila Rashid wakati wa msiba wa mke mdogo, Chiku.

Khadija amesema madai hayo hayana msingi wowote kwa sababu asingeweza kufanya kitu kama hicho kwenye msiba na kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Akihojiwa katika kipindi cha Ng'aring'ri, cha Clouds TV leo, Khadija alisema kifo cha wifi yake, Chiku, ambaye ni mke mdogo wa kaka yake, Mzee Yussuph kilimchanganya na kumpa uchungu mkubwa.

"Kumbuka kulikuwa na watu wengi na ulikuwa msiba, nisingeweza kukataa kupeana naye mkono. Ingekuwa kwenye harusi labda ingeweza kutokea, lakini sio kwenye msiba.

"Na mimi nilikuwa nimechanganyikiwa sana. Nakumbuka nilimuona kwa mbali wakati anafika, lakini sikumbuki kama alinifuata na kunipa mkono, sio kweli hata kidogo,"amesema Khadija, ambaye alikuwa akiimba kundi moja na kaka yake, Mzee Yussuph na wifi yake, Leila.

Khadija amewataka mashabiki wake wapuuze madai hayo kwa kuwa yamelenga kumchafua kwa vile bado anamtambua Leila kuwa ni mke halali wa kaka yake, ikiwa ni pamoja na kuzaa naye watoto wawili.

Aidha, amewataka mashabiki wa muziki huo kumuombea Mzee Yussuph awe na moyo wa subira katika kipindi hiki kigumu, ambacho mkewe amemuachia watoto wadogo wawili.

Chiku alifariki dunia wiki iliyopita baada ya kufanyiwa operesheni ya uzazi kwenye Hospitali ya Amana, Dar es Salaam. Mazishi yake yalifanyika kwenye makaburi ya Kisutu, Dar es Salaam.

Akizungumzia uamuzi wa Mzee Yussuph kuachana na muziki wa taarab na kumrudia Mungu, ikiwa ni pamoja na kwenda kuhiji Makka, Khadija alikiri kuwa anajisikia kupwaya kwa vile alizoea kuimba naye pamoja.

Alisema uamuzi huo wa Mzee Yussuph umemfanya ajihisi upweke kila anapojihusisha na muziki huo stejini kwa vile alimzoea kama kaka, kiongozi na msanii mwenzake.

Kwa upande wake, Mzee Yussuph alisema hana hakika iwapo Khadija alikataa kupeana mkono na Leila wakati wa msiba wa mkewe mdogo, Chiku.

Alisema kama ni kweli Khadija alifanya kitendo hicho ni kosa kubwa mbele ya Mungu, hivyo anamuombea msamaha kwake na kwa mashabiki wa muziki huo.

Hata hivyo, alisema katika siku za hivi karibuni, Khadija alikuwa na uhusiano mzuri na Leila, ikiwa ni pamoja na kuchati ama kuzungumza kwa simu, tofauti na miaka kadhaa iliyopita, ambapo hawakuwa wakielewana.

Kuhusu msiba wa mkewe mdogo Chiku, msanii huyo nyota wa zamani wa taarab alisema baada ya kupata taarifa za kifo chake, alichanganyikiwa kwa kuwa hakutarajia.

Alisema mara baada ya kupata taarifa hizo, alimpigia simu mkewe mkubwa, Leila ambaye naye alichanganyikiwa na kumuuliza iwapo anaruhusiwa kuhudhuria kwenye msiba.

Amesema maneno ambayo hawezi kuyasahau kutoka kwa Leila ni pale alipompa pole na kisha kutuma ujumbe mfupi kwenye simu ya mkononi ukisema 'Jamani Chiku, mbona mapema hivi.'

Sunday, June 18, 2017

MKE WA PILI WA MZEE YUSSUPH AFARIKI KWA UZAZI AMANA




Aliyekuwa mfalme wa muziki wa Taarab Alhaj Mzee Yusuf, amefiwa na mke wake wa pili, Chiku Khamis Tumbo.

Mzee Yusuf amenukuliwa katika moja ya vyombo vya habari leo akisema kuwa, mkewe alifariki jana kwenye Hospitali ya Amana, Dar es Salaam.

Mkurugenzi huyo wa zamani wa kundi la Jahazi, alisema alimpeleka mkewe Amana, jana saa 10 alasiri, kwa ajili ya kujifungua na kwa bahati mbaya opereshini (upasuaji) iliyofanywa jioni, haikwenda salama na ikampoteza mkewe na mtoto aliyezaliwa.

Mazishi ya Chiku yanatarajiwa kufanyika leo jioni kwenye makaburi ya Kisutu, Dar es Salaam. Marehemu Chiku ameacha watoto wawili.

Wednesday, May 10, 2017

ALLY J AITOSA FIVE STARS NA KUREJEA JAHAZI MODERN TAARAB




KIONGOZI wa kundi la muziki wa taarab la Five Stars, Ally J, ameamua kuliacha kundi hilo na kujiunga na kundi lake la zamani la Jahazi.

Ally J, ambaye ni mmoja wa wapapasaji mahiri wa kinanda nchini, amesema uamuzi wake huo umelenga kukuza na kuendeleza fani ya taarab, ambayo imeanza kupwaya.

Msanii huyo alisema ni kweli kwamba, aliwahi kuapa huko nyuma kuwa hatarudi tena kwenye kundi la Jahazi, lakini kuwa na mkataba wa kufanya hivyo.

Alikiri kuwa uamuzi wa kiongozi wa zamani wa Jahazi, Mzee Yussuf, kuachana na taarab baada ya kurejea kutoka Hijja, Makka, umeudhoofisha muziki huo.

"Kwamba sitarajii kurudi Jahazi, yalikuwa maneno tu. Nilipoona wanahitaji mtu wa aina yangu na baada ya kunifuata, nilizungumza nao tukakubaliana,"alisema Ally J, ambaye pia ni mmoja wa watunzi mahiri wa muziki wa taarab nchini.

Mpiga kinanda huyo alisema yeye si mgeni katika kundi la Jahazi kwa vile aliwahi kulitumikia miaka ya nyuma, likiwa chini ya Mzee Yussuf na kwamba aliondoka kwa hiari yake bila kugombana na mtu yeyote.

Ally J alisema anamshukuru Mungu kwamba alipokelewa vizuri Jahazi na kwamba, kurejea kwake hakumaanisha kwamba kundi hilo halina wasanii wengine wazuri wa kiwango chake.

"Si kwamba Jahazi haina wapigaji wazuri, isipokuwa walitaka mtu anayeifahamu vyema mipigo ya Jahazi,"alisema Ally J.

Aliongeza kuwa binafsi anazo njia zake za kimuziki kama ilivyo kwa Jahazi na vikundi vingine vya taarab, lakini hilo haliwezi kumfanya ashindwe kwenda sambamba na kundi hilo kwa wakati huu.

Alisema iwapo ataamua kubadilisha mipigo ya kimuziki ya Jahazi na kuanzisha mipigo ya Five Stars Modern Taarab, atakuwa ameiondoa kwenye reli na kufanya kitu tofauti na kile walichokizoea.

"Mimi na wenzangu kina Jumanne Ulaya na wengine niliowakuta Jahazi, tutakaa na kuona tufanye nini ili kuliendeleza kundi hili kimuziki,"alisema Ally J.

Mtaalamu huyo wa kupapasa kinanda alisema, karibu nyimbo zote alizoshiriki kupiga ala hiyo alipokuwa Jahazi ni nzuri hivyo anaamini ataendelea kutumia ujuzi wake kufanya vizuri zaidi.

Hata hivyo, Ally J amekiri kuwa uamuzi wake wa kurejea Jahazi haukuwafurahisha wasanii na mashabiki wengi wa muziki huo kwa vile kila mmoja ana mtazamo wake.

"Jambo la muhimu ni kwamba nahitaji kufikiria, sio kufikiriwa. Haya ni maisha na maamuzi yangu. Hakuna mdau yeyote wa taarab aliyewahi kunisaidia matatizo yangu ya kimaisha. Tuache maneno maneno, tupige muziki. Tutengeneze nyimbo nzuri,"alisema.

Alisema tayari ameshatunga nyimbo mbili mpya ndani ya kundi la Jahazi, ambazo ni Nataka Jibu na Jicho la Mungu, zilizoimbwa na Mwasiti na Mosi Suleiman.

Alikiri kuwa amekuwa akikumbana na changamoto nyingi katika muziki huo, lakini amekuwa akijitahidi kukabiliana nazo kadri ya uwezo wake.

"Ninachokifanya kwa sasa ni kufikiria nitoe kitu gani kitakachokubalika kwa mashabiki. Hii ni kwa sababu Jahazi imeshatoa nyimbo nyingi nzuri, hivyo mashabiki kwa sasa wanatarajia kuona mambo mapya sio yale yale waliyoyazoea,"alisisitiza msanii huyo.

Pamoja na kujiengua katika kundi la Five Stars Modern Taarab, Ally J alisema kundi hilo bado lipo na litaendelea kufanya maonyesho yake kama ilivyokuwa zamani, japokuwa kwa sasa halina wasanii wa kudumu.

Alisema Five Stars badi ipo na itaendelea kuwepo, isipokuwa yeye ndiye hayupo. Alisema binafsi itakapotokea kundi hilo kupata mwaliko wa kufanya maonyesho, atakuwa akishiriki iwapo kundi lake la Jahazi halitakuwa na kazi siku hiyo.

Thursday, January 5, 2017

LEYLA: SIPENDI KUZUNGUMZA MAMBO YANAYOMUHUSU KHADIJA YUSSUF

MWIMBAJI nyota wa taarab wa kundi la Jahazi, Leyla Rashid, amesema kamwe katika maisha yake hapendi kuzungumza mambo yanayomuhusu Khadija Yussuf.

Leila, mke wa kiongozi wa zamani wa kundi hilo, Mzee Yussuf, amesema anashangazwa na kauli mbalimbali zinazotolewa na Khadija kuhusu ndoa yake.

Mwanamama huyo amesema mumewe hajawahi kumkataza kuimba taarab ama kumtishia kumuacha kama inavyodaiwa na Khadija.

Akizungumzia wimbo mpya wa Khadija, ambao unazungumzia ndoa yake na Mzee, Leyla alisema ameusikia lakini hawezi kuuzungumzia.

"Sina mpango wa kumpa mtu kiki (kumpa ujiko) na wala sifikirii. Najali mambo yangu,"amesema Leyla.

"Ninayemjua katika maisha yangu ni Mzee, sina haja na Khadija,"aliongeza.

Leyla alisema maelewano kati yake na mumewe yanaendelea vizuri na ndoa yao imezidi kuimarika kuliko ilivyokuwa awali.

Aidha, alisema suala la talaka siyo la ajabu kwa watu wenye ndoa na kwamba linaweza kumkuta mtu yeyote.

Tuesday, December 20, 2016

SIJAWAHI KUOMBA TALAKA KWA MUME WANGU-LEYLA


MWIMBAJI nyota wa muziki wa taarab nchini, Leyla Rashid amesema kamwe hajawahi kuomba talaka kutoka kwa mumewe, Mzee Yusuph.

Aidha, Leyla amesema anajisikia upweke kuendelea kuimba nyimbo za muziki huo bila kuwa karibu na Mzee.

Leyla alisema hayo hivi karibuni, baada ya kudaiwa kuwepo na shinikizo la kumtaka aachane na muziki huo na kuungana na mumewe, ambaye kwa sasa ameacha kuimba taarab na kuwa alhaji.

Hivi karibuni, dada wa Mzee Yusuph, Khadija Yusuph, alikaririwa akisema kuwa, Layla anafanya makosa kuendelea kuimba taarab wakati mumewe ameachana na muziki huo.

Khadija alisema kwa mujibu wa sheria za dini ya kiislamu, mke anapaswa kufuata maelekezo ya mumewe iwapo amemtaka kuachana na fani ambayo yeye ameshaiacha.

Akijibu tuhuma hizo, Leyla alisema ni kweli amewahi kugombana na mumewe mara kadhaa, lakini kamwe hakuwahi kuomba talaka.

Pia, alisema sio kweli kwamba Mzee aliwahi kumtishia kwamba atampa talaka iwapo hataacha kuendelea kujihusisha na muziki huo.

"Hajaniambia acha, isipokuwa mimi mwenyewe najihisi kupungukiwa na kitu fulani.Nilizoea tunakuwa pamoja stejini, lakini sasa hayupo tena,"alisema Leyla.

Mwanamama huyo alisema hadi sasa hajaamua nini la kufanya, bali anamuachia Mungu na kusisitiza kuwa, ni kawaida kwa binadamu kutokosa la kusema, lakini hababaishwi na maneno yao.

"Kama mtu anasema, mwache aseme, mdomo ni mali yake," alisema mwanamama huyo mwenye watoto wawili na kusisitiza kuwa, muda wa kuachana na muziki huo ukifika, atafanya hivyo.

Leyla alisema mumewe hadi sasa hajaonyesha shaka yoyote kwake kwa uamuzi wake wa kuendelea na muziki huo, zaidi ya kumtia moyo na kufuatilia maendeleo yake kila anaposafiri mikoani kwa maonyesho mbalimbali.

TMK MODERN TAARAB YAZINDULIWA KWA KISHINDO




KIKUNDI kipya cha taarab cha TMK Modern, mwishoni mwa wiki kilifanya onyesho kabambe la uzinduzi, lililofanyika kwenye ukumbi wa Dar Live, Mbagala, Dar es Salaam na kuhudhuriwa na mashabiki lukuki.

Katika onyesho hilo, kundi hilo lilisindikizwa na bendi ya Twanga Pepeta, Madada sita na mwimbaji nyota wa muziki huo, Leila Rashid kutoka Jahazi.

Wakiongozwa na waimbaji nyota na wakongwe, Mwanahawa Ali, Omar Tego na Maua Tego, kundi hilo liliwafanya mashabiki wafurike kwa wingi stejini kucheza muda wote wa onyesho.

Wakati huo huo, uongozi wa kundi jipya la muziki wa taarab nchini, 'Yah TMK Modern Taarab', umewataka wapenzi wa muziki huo, kuipokea bendi yao ambayo inaanza rasmi maonyesho yake ya katika kumbi mbalimbali hapa nchini.

Mkurugenzi wa kundi hilo, Said Fella amesema baada ya kufanya utambulisho wa kundi hilo mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye ukumbi wa Dar Live, sasa wanaanza rasmi maonyesho katika kumbi mbalimbali za burudani hapa nchini.

Fella alisema kundi hilo litaanza onyesho lake la kwanza Desemba 23, mwaka huu, kwenye ukumbi wa CCM Kigamboni, wakati siku ya mkesha wa Krismas watakuwa kwenye ukumbi wa Mpo Africa, ulioko
Tandika.

Alisema Desemba 25, kundi hilo litakuwa ndani ya ukumbi wa Lekam ulioko Buguruni na Desemba 26, litakuwa kwenye ukumbi wa Lanch Time, Mazense.

Fella alisema kuwa kundi hilo limejipanga kutoa burudani ya aina yake na kudhihirisha kuwa, kwa sasa ndilo moto wa kuotea mbali.

"Lengo letu ni kutoa burudani, tumejipanga kutoa burudani ya aina yake, wanamuziki wapo vizuri na kila mtu anajisikia kufanya kazi yake vizuri kabisa," alisema Fella.

Kundi hilo linaundwa na wasanii mbalimbali nguli, akiwepo Mwanahawa Ali, Fatma Mcharuko, Aisha Vuvuzela, Omar Tego, Maua Tego na wapiga vyombo kina Mohamed Mauji, Mussa Mipango, Chid Boy (kinanda) na Babu Ally Kichupa.

Tuesday, December 13, 2016

ISHA MASHAUZI KUFUNGA NA KUFUNGUA MWAKA NA "KISS ME"

Mwanamuziki maarufu wa muziki wa taarabu hapa nchini Aisha Ramadhani a.k.a Isha Mashauzi (pichani)  anataraji kuachia kibao kipya cha kufunga na kufungua mwaka kitachokwenda kwa jina la "Kiss Me".

Akizungumza na Globu ya Jamii jijini Dar es salaam leo Isha Msahauzi amesema kuwa amekuwa kimya kwa kipindi kirefu hivyo kibao hicho kitaweza kuwarudisha mashabiki wake katika mstari.

“Hii ni zawadi ya kufunga na kufungua mwaka kwa mashabiki wangu. Hivyo mashabiki wangu wapendwa wajue kuwa nyimbo hiyo ambayo ipo katika viwango vya hali ya juu itakonga nyoyo zao",   amesema Isha Mashauzi, akiongezea kuwa imefanywa katika studio za Sophia Records  zilizopo kinondoni”

Ameongeza: "Waliniona  nimekuwa kimya katika taarabu sasa nimerudi tena na hiki kibao ambacho watafurahi wenyewe...."

Tuesday, December 6, 2016

TMK TAARAB KUTAMBULISHWA RASMI KWA MASHABIKI DESEMBA 17



NA VICTOR MKUMBO

TANZANIA ni miongoni mwa nchi za Ukanda wa Pwani, ambazo zina bendi nyingi za muziki wa taarabu.

Muziki wa taarabu umekuwa ukipandachati kila kukicha na wasanii mbalimbali wanaibuka na kufanya vyema.

Hata hivyo,kuna aadhi ya bendi zimekuwa zikianzishwa mara kwa mara na kufanya vizuri, lakini zingine zikifa kutokana na sababu mbalimbali.

Pia,uongozi mbovu unachangia wasanii wengi kuhama bendi moja hadi nyingine kutokana na maslahi duni, tofauti na zamani, ambapo walifanyakazi kwa moyo hata kama hawapati kiwango cha fedha cha kuridhisha.

Kwa sasa, kuna ushindani mkubwa ndani ya muziki huo huku wasanii wakongwe wakitamani kutoka kwenye bendi kubwa na kuhamia katika bendi zisizokuwa na majina makubwa ili kufuata neema.

Bendi mpya ya taarabu ya TMK Modern, imeanzishwa kwa mara ya kwanza waka huu, ikiwa imesheheni wasanii wakongwe, ambao kwa namna moja au nyingine wanaweza kuipa mafanikio kutokana na umahiri wao.

Wasanii, wakongwe waliojiunga na bendi hiyo, wametoka katika bendi za muziki wataarabu ambazo zinatamba kwa sasa kwa ajili ya kuongeza upinzani ndani ya tasnia hiyo.

Kutokana na jinsi uongozi waTMK Modern Taarab, kujipanga vyema, huenda ikawa moja ya bendi ambazo zitatikisa kwenye muziki huo na watu wanasubiri kwa hamu kuona vitu vipya.

Bendi hiyo inaongozwa na Mkurugenzi, Said Fella, mbaye ni mmoja wa watu waliodumu kwenye tasnia ya muziki kwa muda mrefu.

Wasanii ambao wapo chini ya Fella wamekuwa akifanikiwa zaidi kila kukicha na kufanya matamasha ndani na nje ya nchi.

Fella anamiliki kituo cha wasanii cha kubwa na Wanawe, ambapo ndani yake kuna wasanii wa kila sanaa.

Kituo hicho kimetambulika kwa kuwatoa wasanii wachanga na kufanya vyema kwenye tasnia ya muziki, tofauti na jinsi ilivyokuwa inatarajiwa na wengi.

Wapo wasanii ambao wametokea kwa Fella na kwa sasa wanafanya vizuri na nyimbo zao haziishi kusikilizwa na kutazamwa na mashabiki wa muziki katika ukanda wa AfrikaMashariki.

Kundi la TMK Modern Taarab, linaundwa na wasanii nguli kina Mwanahawa Ally, FatmaMcharuko, Aisha Vuvuzela, Maua Tego na OmaryTego.

Wasanii waliotoka Mkubwa na Wanawe ni Amina Mnyalu, Jeza Adam, Hassan Saleh na Ibrahim Said.

Wapiga ala ni Mussa Mipango, Father Mauji, Chid Boy na Babu Ally ambao wamejikitika katika upande wa kupiga gita na kinanda.

Akizungumzia kundi hilo hivi karibuni, Mkurugenzi Mtendaji, OmaryTego, alisema wameanzisha bendi hiyo mwaka huu ili kuhakikisha wanaleta mapinduzi katika muziki wa taarab nchini.

Alisema kwa kiasi kikubwa wamejipanga, hivyo wana imani kubwa yakuufikisha mbali muziki wa taarab.

Alisema bendi hiyo inaundwa na wasanii wakongwe waliopitia katikabendi mbalimbali za muziki wa aarab ili kuhakikisha wanasimama vyema.

Alisema kuna changamoto mbalimbali wasanii wanaounda kundi hilo,
ambazo wamepitia awali na hivyo kuamua kuunda kundi la pamoja na kurudi upya katika muziki huo.

“Wasanii wanaounda kundi la TMK Modern Taarab, wametokea atika bendi mbalimbali, ili kuhakikisha tunafikia malengo kwani pia wamepitia kwenye changamoto nyingi hadi kufika hapa walipo sasa,” amesema.

Anasema kuwa adi sasa wameshakamilisha kurekodi jumla ya nyimbo saba ambazo zitakuwepo kwenye albamu zao mpya zitakazotoka mwakani.

Amesema kuwa baadhi ya nyimbo zimeshaanza kusikika katika vituo mbalimbali vya redio na kufanya vizuri.

Nyimbo zilizoanza kusikika ni pamoja na Figisufigisu zimekwisha, mtunzi akiwa Tego, Sina pupa Mungu atanipa, iliyoimbwa na Manahawa, Kibaya kina mwenyewe ya Aisha Vuvuzela na Ndoa, iliyoimbwa na Jeza Adam.
 “Nyimbo ambazo zimeshakamilika zimetungwa kwa ustadi mkubwa na hivyo msikilizaji hatachoka kupata burudani safi, ikiwa ni pamoja na ujumbe uliopo,” amesema.

Mkurugenzi huyo anasema kuwa bado wapo katika mikakati ya kuboresha kundi lao ili kuhakikisha linaimarika zaidi.

Amesema kuwa apo wasanii wakubwa kutoka kwenye bendi kongwe, ambao wanatarajiwa kujiunga nao hivi karibuni.

“Tumejipanga vyema kuhakikisha tunafanya mapinduzi kwenye muziki wa taarab kwani pia bado tupo kwenye mikakati ya kuimarisha kundi letu. Kuna baadhi ya wasanii ambao watajiunga na sisi hivi karibuni na wanatoka kwenye bendi kongwe,” amesema.

Ameongeza uwa wanatarajia kufanya uzinduzi wa kuitambulisha rasmi bendi hiyo Desemba 17, mwaka huu, katika onyesho la kwanza litakalofanyika kwenye ukumbi wa Dar Live.

Amesema uwa uzinduzi huo unatarajiwa kuwa wa aina yake kutokana na maandalizi ya muda mrefu waliyoyafanya.

Katika uzinduzi huo, watasindikizwa na wasanii mbalimbali, wakiwemo  Amani Temba na Said Chege, Dullah Makabila, Madada sita kutoka Mkubwa na Wanawe na kundi zima la The African Stars ‘TwangaPepeta’.

Baada ya uzinduzi huo, wataendelea kufanya maandaliziyaalbamu zao mbili, ambazo zitatoka kwa mpigo.

Monday, October 31, 2016

KUNDI JIYA LA TAARAB LA TMK LAIBOMOA JAHAZI, COAST MODERN TAARAB


Ule usemi unaosemwa na baadhi ya wadau wa taarab ya kuwa "Jahazi Modern Taarab bila ya Mzee Yussuf linasuasua" unaonekana kama unakubalika kwa asilimia fulani baada ya bendi hiyo kupoteza waimbaji muhimu pamoja na wapiga vinanda.

Majina ya Fatma Nyoro, Chidi Boy, Moh'd Mauji, Mussa Mipango, Kichupa kwa sasa hayatosikika kwenye maonesho ya Jahazi.

Pia kuna tetesi kuwa Khadija Yussuf ameenda Wakaliwao kwa Thabit Abdul.

Bendi ya TMK pia imeibomoa Coast Modern Taarab kwa kumpa shavu Omary Teggo na dada yake.
Pia Bi Mwanahawa Ali (JEMBE GUMU) ametilishiwa saini katika bendi hiyo huku akipewa wimbo wa "SINA PUPA MUNGU ATANIPA".

Thursday, October 20, 2016

ISHA MASHAUZI, LEYLA RASHID NANI ZAIDI KUONYESHANA KAZI KESHOKUTWA DAR




NI vita ya “Sura Surambi” na “Nina Moyo Sio Jiwe”.  Ndiyo unavyoweza kusema kuelekea mpambano wa waimbaji nyota wa taarab malkia Leyla Rashid na Isha Mashauzi.

Onyesho hilo linasosubiriwa kwa hamu kubwa litafanyika Jumamosi ya tarehe 22 mwezi huu ndani ya ukumbi wa Dar Live Mbagala, jijini Dar es Saalam.

Bendi mbili kubwa za taarab, Jahazi Modern Taarab na Mashauzi Classic ndiyo zitakazosindikiza mpambano wa mahasimu hao wawili.

“Sura Surambi” ni moja ya nyimbo ambazo piga ua lazima iwe kweye ratiba ya Isha Mashauzi wakati iwe isiwe Leyla naye lazima aidumbukize ngoma yake ya “Nina Moyo Sio Jiwe” katika orodha ya nyimbo atakazotumbuiza.

Tangu onyesho hilo litangazwe, waimbaji hao wameingia kwenye vita vikubwa vya maneno ambapo kila mmoja amejinasibu kuibuka na ushindi.

Tuesday, September 27, 2016

DK SHEIN AONGOZA HARAMBEE YA KUCHANGIA UJENZI WA TAASISI YA SITI BINTI SAAD

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akimkabidhi picha ya kuchora Mmiliki na Mkurugenzi wa Kampuni ya Pennyroyal inayojenga Hoteli Kubwa ya Kimataifa huko Matemwe Kaskazini Unguja Bw.Brian Thomson (kulia) iliyonadishwa na kuinunua kwa Shilingi za Kitanzania Milioni nane(8) pia  akiwa amechangia Shilingi Miliion Ishirini na tano katika  Harambee ya kuchangia ujenzi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Sadi,hafla ilifanyika jana katika Ukumbi wa Hayat Hotel Mjini Unguja,wakati huohuo ameahidi kuanzisha Chuo cha Muziki Academy katika Mkoa wa Kaskazini,ambapo mradi huo utagharimu shilingi za kitanzania Miliioni mia sita, wakiwemo  na walimu pamoja na zana  zote

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akimkabidhi picha ya kuchora Mmiliki na Mkurugenzi wa Kampuni ya Pennyroyal inayojenga Hoteli Kubwa ya Kimataifa huko Matemwe Kaskazini Unguja Bw.Brian Thomson (kulia) iliyonadishwa na kuinunua kwa Shilingi za Kitanzania Milioni nane(8) pia  akiwa amechangia Shilingi Miliion Ishirini na tano katika  Harambee ya kuchangia ujenzi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Sadi,hafla ilifanyika jana katika Ukumbi wa Hayat Hotel Mjini Unguja,wakati huohuo ameahidi kuanzisha Chuo cha Muziki Academy katika Mkoa wa Kaskazini,ambapo mradi huo utagharimu shilingi za kitanzania Miliioni mia sita

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein,(kushoto) na Mtoto wa Mwanahamis Ali 9years mkaazi wa Shaurimoyo Mjini Unguja akichora kaburi alilozikwa Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad (katika picha ya kuchora chini) baada ya kukabidhiwa picha hiyo Rais, wakati wa harambee ya Ujenzi wa Ofisi ya taasisi hiyo  iliyofanyika jana katika ukumbi wa Hayyat Hotel Mjini Unguja

Baadhi ya Mawaziri wakiwa katika hafla ya harambee ya Ujenzi wa Ofisi ya taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad inayotarajiwa kujengwa Fumba Mkoa wa Magharibi Unguja,wakiwa katika hafla iliyofanyika jana katika ukumbi wa Hayyat Hotel

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein,(katikati) Rais Mstaafu wa Jamhuri ya muungano Mzee Mwinyi(kushoto)  pia Mlezi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad na Mwenyekiti wa taasisi hiyo Bi Nasra Mohamed Hilal (wa pili kuli) wakimuangalia Mtoto wa Mwanahamis Ali 9years mkaazi wa Shaurimoyo Mjini Unguja akichora kaburi alilozikwa Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad wakati wa harambee ya Ujenzi wa Ofisi ya taasisi hiyo inayotarajiwa kujengwa Fumba Mkoa wa Magharibi Unguja,katika hafla iliyofanyika jana katika ukumbi wa Hayyat Hotel

Kikundi cha Muziki cha Rahatul Zamani kikitumbuiza  wakati wa Harambee ya kuchangia   ujenzi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad hafla iliyofanyika jana katika Ukumbi wa Hayatt Hotel Mjini Unguja,mgeni rasmi akiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein

Mmiliki na Mkurugenzi wa Kampuni ya Pennyroyal inayojenga Hoteli Kubwa ya Kimataifa huko Matemwe Kaskazini Unguja Bw.Brian Thomson (wa pili kushoto) akiwa na msaidizi wa kampuni ya ujenzi ya Pennyroyal inayojenga Hoteli Kubwa ya Kimataifa huko Matemwe Kaskazini Unguja Bw.David Haycok (kushoto)pamoja na Wasaidi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein,(kutoka kulia) Mzee Burhani Saadat Haji na Chimbeni Kheir wakiwa katika Harambee ya kuchangia   ujenzi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad iliyofanyika jana katika Ukumbi wa Hayatt Hotel Mjini Unguja

Baadhi ya Viongozi na Wafanyabishara wa makampuni mbali mbali wakiwa katika Harambee ya kuchangia   ujenzi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad iliyofanyika jana katika Ukumbi wa Hayatt Hotel Mjini Unguja

Baadhi ya Viongozi na Wafanyabishara wa makampuni mbali mbali wakiwa katika Harambee ya kuchangia   ujenzi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad iliyofanyika jana katika Ukumbi wa Hayatt Hotel Mjini Unguja

Baadhi ya Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakijaza fomu maalum za kuchangia fedha kwa ajili ya ujenzi wakati wa harambee ya Ujenzi wa Ofisi ya taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad inayotarajiwa kujengwa Fumba Mkoa wa Magharibi Unguja, katika hafla iliyofanyika jana ukumbi wa Hayyat Hotel

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akimkabidhi picha ya kuchora ya Marehemu Bibi Siti Binti Saad Mkurugenzi wa Kampuni ya Azam Marine Fasty Ferry Huseein Mohamed wakati wa harambee ya Ujenzi wa Ofisi ya taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Binti Saad inayotarajiwa kujengwa Fumba Mkoa wa Magharibi Unguja, katika hafla iliyofanyika jana ukumbi wa Hayyat Hotel Mjini Zanzibar,[Picha na Ikulu.]

Sunday, August 21, 2016

JK, MAKAMU WA RAIS SAMIA WAONGOZA MAZISHI YA MAREHEMU SHAKILA SAIDI

HII ni picha aliyopiga kwa mara ya mwisho marehemu Bi Shakila Saidi alipohudhuria mkutano mkuu maalumu wa CCM uliofanyika Julai 23, mwaka huu mjini Dodoma
Rais mstaafu Jakaya Kikwete akitia saini kitabu cha maombolezo baada ya kuwasili nyumbani kwa marehemu Bi Shakila Saidi, Mbagala Charambe, Dar es Salaam jana.
MAKAMU wa Rais Samia Suluhu Hassan akitia saini kitabu cha maombolezo baada ya kuwasili nyumbani kwa marehemu Bi Shakila Saidi
MKE wa Rais mstaafu Jakaya Kikwete, Mama Salma Kikwete akitia saini kitabu cha maombolezo nyumbani kwa marehemu
WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Michezo na Sanaa, Nape Nnauye akimkaribisha Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan nyumbani kwa marehemu Bi Shakila Saidi
Makamu wa Rais akiwafariji baadhi ya ndugu wa marehemu
WAZIRI Nape akiteta jambo na mmiliki wa blogu ya Michuzi, Ankal Muhidin Issa Michuzi. Katikati ni Mwenyekiti wa Chama Cha Muziki wa Dansi, Athumani Msumari
BAADHI ya waumini wa dini ya kiislamu wakijiandaa kuuswalia mwili wa marehemu Bi Shakila
MAKAMU wa Rais akishiriki kwenye dua ya kumuombea marehemu Shakila
JENEZA lenye mwili wa Bi Shakila likipelekwa makaburini. PICHA KWA HISANI YA BLOGU YA MICHUZI NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS

Saturday, August 20, 2016

MKONGWE WA TAARAB NCHINI BI SHAKILA SAIDI AFARIKI DUNIA



Bi Shakila Tatu Said Msengi muimbaji maarufu wa Taarab, hatunae tena. Jioni leo ameanguka ghafla na alipokimbizwa hospitali moja jirani na kwake Mbagala Charambe alipofika huko Bi Shakila alikata roho.

Bi Shakila alikuwa mzaliwa wa peke yake kwa baba na mama yake, alizaliwa tarehe 14 June 1947, tarehe moja na mwanamuziki mwingine mkongwe Mabruk Khamis wa Kilimanjaro Band anaejulikana kwa jina la Babu Njenje.

Mama yake Babu Njenje alikuwa na tatizo la kutoa maziwa hivyo Babu Njenje alianza kwa kunyonyeshwa na mama yake wa Bi Shakila.

Kwa kadri ya maelezo yake mwenyewe Bi Shakila alianza muziki akiwa na miaka 6, alipokuwa na umri wa miaka 12, aliteuliwa kumuimbia Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alipotembelea Pangani, wakati wa kutafuta Uhuru.

Na ni baada ya hapa ambapo aliweza kusikika na Bwana Khatibu ambaye aliweza kumshawishi kujiunga na kundi la Taarab lililokuwa pale Pangani lililoitwa Taarab Kijamvi, hakukaa sana katika kundi hilo akalazimika kuhamia Tanga kumfuata Bwana Khatib ambaye walibahatika kuzaa watoto watano.

Huko Tanga alijiunga na kundi la Shaabab Al Watan. Katika kundi hili hakupata nafasi ya kuimba katika kadamnasi, hivyo baada ya muda si mrefu Bi Shakila akiambatana ma mumewe walihamia kundi lililokuwa likimilikiwa na Mzee Kiroboto lililoitwa Young Noverty.
Pamoja na Bi Shakila kupata uzoefu mkubwa wa kuimba mbele za watu kundi hili lilikuwa ni kutumbuiza bure katika vikao vya kahawa.

Hatimae kundi hili lilikufa na zaidi ya nusus ya wasanii kujiunga na kundi la Black Star lililokuwa la mwarabu mmoja aliyekuwa anafanya kazi bandarini aliyeitwa Hassan Awadh na hapo ndipo Bi Shakila alipoanza kufahamika, na akapewa nyimbo kama Jongoo Acha Makuu, Mpenzi Amini, Majuto Yamenipata.

Sifa zake zikaanza kuenea Afrika Mashariki. Mwaka 1972 tajiri mwingine Mwarabu aliyeitwa Sudi Said akanunua vyombo vipya vizuri na kuanzisha kundi la Lucky Star Musical Club, hapo Bi Shakila na wenzie tisa walihama Black Star na kuhamia Lucky Star.

Kwa kuwa kundi lilianzishwa wakati Bi Shakila alikuwa mja mzito, mtoto aliyezaliwa alimuita Lucky kwa ajili ya tukio hilo. Nyimbo nyingi zinazofahamika hadi leo za Bi Shakila zilirekodiwa wakati yuko kundi hili.

Mapenzi Yamepungua, Kifo cha Mahaba. Macho Yanacheka. Bi Shakila aliendelea na kundi hili hadi mwaka 1984, Baada ya kifo cha mumewe alipumzika kwa muda kasha akahamia Dar es salaam ambapo alijiunga na kundi la JKT alilodumu nalo mpaka alipostaafu.
CHANZO CHA HABARI: BLOGU YA KITIME