KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Tuesday, December 22, 2015

MABADILIKO YA JINA LA BLOGU



WAPENZI WASOMAJI.

BLOGU YAKO PENDWA YA CCMNUMBERONE, ILIYOKUWA MAALUMU KWA KURIPOTI HABARI ZA UCHAGUZI MKUU WA MWAKA 2015, SASA IMEBADILISHWA JINA NA ITAJULIKANA KWA JINA LA TANZANIAKWANZADAIMA. ITAKUWA MAALUMU KWA KURIPOTI HABARI ZA KISIASA, KIUCHUMI, BIASHARA, ELIMU NA MAMBO MENGINE YA KIJAMII.

INAPATIKANA KWA ANWANI IFUATAYO:

www.tanzaniakwanzadaima.blogspot.com



KARIBUNI TUENDELEZE LIBENEKE.

Saturday, December 12, 2015

ZUHURA SHAABAN AANGUO KILIO, ASEMA TAARAB SASA BASI


Na Rashid Zahor

MWIMBAJI nyota na machachari wa muziki wa taarab nchini, Zuhura Shaaban, amejikuta akibubujikwa na machozi na kuapa kwamba, kamwe hatawasamehe watu wanaomzushia maneno ya uongo kwamba anajihusisha na mapenzi ya jinsia moja.

Zuhura amesema japokuwa vitabu vya dini vinasisitiza umuhimu wa binadamu kusameheana pale wanapotendeana makosa, kwake katu hawezi kuwasamehe watu hao.

Huku akitokwa na machozi kwa uchungu, Zuhura amesema kamwe katika maisha yake hajawahi kujihusisha na vitendo vya aina hiyo na roho huwa ikimuuma pale anapowasikia ama kuwaona watu wakizungumzia jambo hilo kuhusu yeye.

"Watu wananisema vibaya. Wananiweka kwenye mstari ambao mimi sipo. Roho inaniuma sana kwa sababu tangu nilipozaliwa kutoka tumboni kwa mama yangu hadi leo hii nina umri wa miaka 49, sijawahi kujihusisha na vitendo hivyo,"amesema Zuhura huku akishindwa kuyazuia machozi yaliyokuwa yakimchuruzika.

Zuhura alijikuta akiwa katika hali hiyo wiki hii, alipokuwa akihojiwa na mtangazaji Mariam wa Migomba, katika kipindi cha Muziki wa Mwambao, kilichorushwa hewani na kituo
cha televisheni cha TBC 1.

"Kama kuna mtu niliyewahi kumtamkia kuhusu kufanya naye kitendo  hicho ama niliwahi kufanya naye, ajitokeze hadharani aseme," alisema Zuhura, mwimbaji mwenye sauti yenye mvuto na macho ya kuvutia.

Aliongeza kuwa kutokana na uvumi huo, kila anapokwenda kwenye shughuli za kijamii, akiwa ameongozana na mwanamke mwenzake, baadhi ya watu humnyooshea vidole ama kukonyezana na kuanza kumzungumzia vibaya.

"Siwezi kumsamehe mtu wa aina hiyo. Sitamsamehe japo dini inatufundisha kusameheana,"alisema Zuhura, mwimbaji asiyependa makeke anapokuwa jukwaani, zaidi ya kuutikisa mwili wake taratibu kwa namna ya kuvutia.

Licha ya umaarufu alionao katika muziki wa taarab kutokana na uimbaji wake mwanana na sauti ya kuvutia, Zuhura kwa sasa ameamua kujiweka kando na muziki huo.

Moja ya sababu anazozitaja ni umri kumtupa mkono, licha ya ukweli kwamba wapo baadhi ya waimbaji nyota wa kike wenye umri mkubwa kuliko wake, kama vile Mwanahawa Ally, Khadija Kopa na Rukia Juma, ambao bado wanajihusisha na muziki huo.

"Wakati umekwenda. Katika maisha, lazima hufika wakati wewe mwenyewe unaamua hiki nitafanya, hiki sifanyi.

"Wakati ule nilikuwa mdogo, nilikuwa naweza kufanya chochote ninachokitaka, lakini kwa sasa nimeshakuwa mtu mzima, nina watoto. Baadhi ya wakati huwa wananiambia mama hilo hapana,"alisema Zuhura, mwimbaji mwenye sauti inayopanda na kushuka mithili ya mawimbi baharini.

Mwanamama huyo mwenye wajihi unaovutia na sura ya mchongo wa dafu, amesema kwa sasa ameamua kujihusisha na biashara kwa ajili ya kuendesha maisha yake na familia yake, akiwa anamiliki duka la nguo.

Amesema kwenye duka hilo lililoko visiwani Zanzibar katika kisiwa cha Unguja, anauza nguo za kinamama, vipodozi na vikolombwezo vya aina mbalimbali vinavyowahusu wanawake.

"Nimeamua kuingia kwenye biashara. Nauza nguo na vitu vya kike. Naendesha maisha yangu na watoto kwa njia hiyo,"amesema Zuhura.

Akizungumzia maendeleo ya muziki wa taarab kwa sasa, Zuhura alisema umepoteza maana na mvuto kutokana na kutoka nje ya mipaka na kuwa muziki wenye kelele nyingi.

Alisema wakati ulipoanzishwa mtindo wa modern taarab, akiwa na kikundi cha East African Melody, hawakutokana moja kwa moja nje ya muziki wa taarab kama ilivyo sasa.

"Vikundi vya sasa hivi vimetoka nje kabisa ya taarab, kuanzia kwenye ushairi na mipigo ya nyimbo,"amesema mwanamama huyo.

Amewataka wasanii wakongwe wa muziki huo, ambao bado wanaendelea kujihusisha na taarab, wakae chini na kutafakari wapi walikotoka, walipo na wanakokwenda.

Alisema kama miaka ya nyuma waliweza kupiga muziki wa kiasili wa taarab na kuongeza madoido kidogo, haoni kwa nini wasiendelee kufanya hivyo kwa sasa ili wasipoteze asili ya taarab.

"Siku hizi waimbaji wa taarab hawaimbi, wanapiga kelele,"alisema.

Kwa mujibu wa Zuhura, wapo waimbaji wengi wazuri hivi sasa kuliko hata enzi zao, lakini wanakosa miongozo mizuri ya kuimba nyimbo za muziki huo kwa namna ya kuvutia.

Ameutaja wimbo ambao anaamini aliutendea haki katika kuuimba na hadi leo bado unamvutia kuwa ni 'Siadhiriki', aliourekodi wakati akiwa katika kikundi cha East African Melody.

Katika maisha yake ya usanii, Zuhura hajawahi kutunga wimbo wa taarab zaidi ya kutungiwa na watunzi mahiri wa nyimbo hizo. Anasema hiyo ni kwa sababu hana kipaji cha utunzi.

"Katika kipindi chote nilichokuwa nikiimba taarab kwenye vikundi mbalimbali, sikuwa natilia maanani na kuuweka rohoni muziki huo. Kuna watu waliogundua kwamba nina kipaji na ndio waliokuwa wakinihamasisha kuimba,"alisema.

Amesema vivyo hivyo hakuwahi kumfundisha kuimba msanii yoyote wa kike kwa kuwa hata naye hakuwahi kufundishwa kufanya hivyo.

Mbali na kikundi cha East African Melody, Zuhura amewahi kuimbia vikundi vya Zanzibar Stars na Zanzibar One. Kwa sasa anaimba muziki wa kwenye sherehe tu, hasa za harusi visiwani Zanzibar.

Wednesday, November 25, 2015

ISHA MASHAUZI SASA AJA NA KISMET



Isha Mashauzi “Queen of the Best Melodies” au malkia wa masauti ukipenda, ameingia studio kurekodi wimbo wake mpya kabisa unaokwenda kwa jina la “Kismet”. 

Isha akiwa na kundi zima la Mashauzi Classic, amerekodi wimbo huo katika studio za Sofia Records chini ya producer Ababuu Mwana Zanzibar. 

Huo ni wimbo utakaopatikana katika albam ijayo ya Mashauzi Classic Modern Taarab, ukiachana na “Sura Surambi” inayozinduliwa Alhamisi hii Mango Garden Kinondoni. 

“Hakuna kulala, mwisho albam moja ndiyo mwanzo wa albam ijayo”, alisema Isha Mashauzi katika maongezi yake na Saluti5. 

“Huu ni utaratibu wangu wa siku zote, kuisindikiza albam inayozinduliwa kwa kigongo kitachopatikana albam ijayo,” anafafanua Isha. 

“Kismet” ni utunzi wake Isha Mashauzi ambapo ndani ya wimbo huo, mwimbaji huyo anasema anawawakilisha wale wote ambao wako ndani dimbwi la mapenzi yaliyokolea raha, mapenzi yasiyo na kokoro wala chembe ya maudhi. 

Isha ameiambia Saluti5 kuwa “Kismet” ambayo tayari inatingisha kwenye kumbi za burudani wanazopiga Mashauzi Classic, inaingia hewani wiki hii.
IMETOLEWA KUTOKA BLOGU YA SALUTE 5

Saturday, November 21, 2015

PICHA YA KIHISTORIA KWA WATANZANIA, HAIJAWAHI KUTOKEA NA PENGINE HAITAKUJA KUTOKEA AFRIKA

RAIS John Magufuli akiwa katika picha ya pamoja na marais wastaafu, wa awamu ya pili, Ali Hassan Mwinyi, wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa na wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete baada ya kulihutubia na kulizindua jana mjini Dodoma.

Monday, August 10, 2015

HAMMER Q AJA NA VIJUMBA JUMBA



Ni Mr & Mrs Hammer Q katika nyimbo Mpya waliyoipa jina la "Vijumba Jumba".

Ni nyimbo Tamu, Nyimbo nzuri iliyo tofauti kabisa na Miondoko ya Taarabu za hivi sasa, ni Taarabu asilia iliyoimbwa na watu wawili Mr & Mrs, wakiimba kwa kupokezana, utaipenda.

Hammer Q ameongea na blog hii ya taarabuzetu.blogspot.com na kusema yupo katika mkakati kabambe wa kurudisha Taarabu asilia ile Taarabu ya kipindi kileee...!!

Ni nyimbo nzuri kusikiliza na Familia yako, Sherehe na Popote pale unaisikiliza kwa raha zako.

IMETOLEWA KUTOKA BLOGU YA TAARABUZETU

Monday, May 11, 2015

HIVI NDIVYO VIBAO VIPYA VYA OGOPA KOPA


DAR MODERN TAARAB KUFANYA ZIARA MIKOA SITA


KIKUNDI cha taarab cha Dar Modern, kinatarajia kufana ziara katika mikoa sita nchini kwa lengo la kutambulisha ujio wake mpya katika muziki huo.

Ziara hiyo, iliyopewa jina la Modenika na Dar Modern,  italifikisha kundi hilo katika mikoa ya Rukwa, Katavi, Dodoma, Morogoro na Dar.

Mratibu wa ziara hiyo, Emmanuel Simon, alisema wiki hii kuwa, ziara hiyo itaanzia mkoani Mbeya, ambako kundi hilo litafanyika onyesho lake la kwanza Mei 20 mwaka huu katika mji mdogo wa Kyela.

Mei 22, mwaka huu, kundi hilo litafanya onyesho lingine katika mji mdogo wa Mpanda ulioko mkoani Katavi, wakati siku inayofuata, litahanikiza maraha katika mji wa Sumbawanga ulioko mkoani Rukwa.

Kwa mujibu wa Emmauel, baada ya maonyesho hayo, kundi hilo litarejea Dar es Salaam, ambako Mei 29, litafanya onyesho kwenye ukumbi wa Travertine ulioko Magomeni.

Mei 30, kundi hilo litakuwa kwenye ukumbi wa Royal Village ulioko mjini Dodoma na siku inayofuata, litamaliza ziara yake hiyo mjini Kilosa mkoani Morogoro kwa kufanya onyesho kwenye ukumbi wa Babylon.

Emmanuel amewataka mashabiki wa taarab kujitokeza kwa wingi kushuhudia maonyesho hayo, ikiwa ni pamoja na ujio mpya wa kundi hilo kwa vile limewaandalia mambo mazuri.

KHADIJA KOPA: NILIWAHI KUVUMISHIWA NIMEMUUA LEILA KHATIBU NA OMAR KOPA




WAKATI alipojiunga na kikundi cha taarab cha Tanzania One Theatre (TOT Plus), mwanzoni mwa miaka ya 1990, Khadija Omar Kopa, alionekana kuwa mwimbaji wa kawaida. Si mashabiki wengi wa muziki huo waliokuwa wakimfahamu.
Lakini kwa mashabiki wa taarab wa visiwa vya Zanzibar, jina la Khadija Kopa lilikuwa maarufu. Ni kutokana na uimbaji wake mahiri na sauti yake maridhawa, kupitia vibao vilivyompa sifa na umaarufu mkubwa, kama vile Kadandie, Daktari na Wahoi, alivyoviimba akiwa katika kikundi cha Culture.
Hiyo ndiyo sababu kubwa iliyoufanya uongozi wa TOT Plus, kumfuata Khadija visiwani Zanzibar na kumuomba ajiunge na kikundi hicho ili kukipa sura na mwonekano mpya, tofauti na taarab iliyozoeleka Tanzania Bara.
Kwa umbo, Khadija Omar Kopa ni mnene. Rangi yake ni nyeusi yenye mng’ao. Uso wake hujawa na tabasamu muda wote utadhani hajui kitu kinachoitwa kukasirika.
Licha ya kuwa na umbile hilo, Khadija ni mwepesi wa kuunyonganyonga mwili wake atakavyo awapo stejini, akiimba nyimbo za muziki wa taarab. Sauti yake nayo ni maridhawa na yenye mvuto wa pekee.
Sifa hizo ndizo zilizomfanya mwanamama huyo apachikwe jina la ‘Malkia wa Mipasho’ nchini. Waliompa jina hilo hawakubahatisha, walitambua vyema kwamba uwezo wake katika fani hiyo ni mkubwa.
Akiwa TOT Plus mwaka 1992, Khadija ambaye ni mmoja wa waanzilishi wa kundi hilo, alidhihirisha kwamba halikukosea kumfungia safari visiwani humo baada ya kuanza kung’ara kwa vibao kama ‘Tx mpenzi’, ‘Ngwinji’, ‘Wrong number’, ‘Mtie kamba mumeo’ na nyinginezo.
Hata hivyo, miaka miwili baadaye, Khadija alikorofishana na uongozi wa TOT Plus baada ya yeye na mwimbaji mwenzake, Othman Soud kuamua kuondoka kinyemela na kwenda Dubai, ambako walishiriki kuanzisha kundi la East African Melody.
Baada ya kurejea nchini kutoka Dubai, mwanamama huyo alilazimika kujiunga na kikundi cha Muungano Cultural Troupe kwa vile uongozi wa TOT uligoma kumpokea.
Kujiunga kwa Khadija na Othman katika kikundi cha Muungano, kulisababisha kuwepo kwa ushindani mkali kati ya vikundi hivyo viwili, ambavyo vilifanya maonyesho kadhaa ya pamoja kwa ajili ya kuonyeshana nani mkali.
Akiwa Muungano, Khadija aling’ara kwa vibao vyake murua kama vile ‘Homa ya Jiji’, ‘Kiduhushi’ na ‘Umeishiwa’. Pia kulizuka ushindani mkali kati yake na marehemu Nasma Khamis ‘Kidogo’, ambaye alichukuliwa na TOT kutoka Culture kwa lengo la kuziba pengo lake.
Akizungumza mjini Dar es Salaam hivi karibuni, Khadija alikiri kwamba asingeweza kufika mahali alipo bila ya kupata msaada mkubwa kutoka kwa Othman.
“Othman ndiye aliyekuwa mtunzi wa nyimbo zote nilizoimba tangu nikiwa Culture na TOT. Hata TOT waliponifuata Zanzibar, niliwaambia kwamba nisingeweza kujiunga na kikundi hicho bila ya Othman kwa sababu bila yeye nisingeweza kufanya lolote la maana,”alisema Khadija.
Kwa sasa, Othman ni askari wa Jeshi la Magereza visiwani Zanzibar na uamuzi wake wa kuacha kujihusisha na muziki wa taarab ulimfanya Khadija aanze kuchacharika na kutunga nyimbo zake mwenyewe.
Khadija anakiri kuwa ushindani wa kimuziki uliokuwepo kati ya TOT na Muungano ulisaidia kwa kiasi kikubwa kuinua hadhi ya muziki huo. Anasema haitatokea kwa vikundi viwili vya taarab nchini kuwa na ushindani kama huo.
“Kila tulipofanya maonyesho ya pamoja, kumbi zilifurika. Iwe Dar es Salaam, Morogoro au Mwanza, mashabiki walikuwa wakifurika ukumbini kutushuhudia.
“Ni ushindani uliosababisha mashabiki wetu wajenge uhasama mkubwa, lakini sisi wasanii tulikuwa kitu kimoja. Wengine walidhani mimi na Nasma  tulikuwa na uadui kutokana na nyimbo tulizoimba, kumbe tulikuwa marafiki wakubwa na tulisaidiana kwa kila hali,”alisema Khadija.
Khadija amekiri kuwa ushindani wa taarab umepungua katika miaka ya hivi karibuni kutokana na kuwepo kwa utitiri wa vikundi vya muziki huo.
Aidha, alisema maonyesho ya vikundi vya taarab yamekuwa yakifanyika kuanzia Jumatatu hadi Jumapili hivyo kuwafanya wasanii wake kuchoka na kukosa ubunifu.
“Kinachosikitisha zaidi ni kuona kuwa baadhi ya vikundi vya mitaani vimekuwa vikiimba nyimbo za vikundi vingine na maonyesho yamekuwa yakifanyika bure hadi mashabiki wanachoka.
“Utakuta kikundi kimoja kinafanya onyesho mtaa huu, kingine kinafanya onyesho mtaa wa pili. Huyu akisikia mwenzake amekwenda kufanya maonyesho Lindi na mwingine naye anakwenda huko huko,”alisema Khadija.
Akizungumzia madai ya kuwepo kwa uhusiano kati ya muziki wa taarab na ushoga, Khadija alisema si kweli kwa sababu kumjua shoga kunahitaji ushahidi wa uhakika.
“Ushoga ni nafsi ya mtu kupenda kitu, si maumbile au mwonekano wake,”alisisitiza mwanamama huyo.
Mwimbaji huyo pia alieleza kusikitishwa kwake na tabia ya baadhi ya mashabiki wa muziki huo, hasa wanawake, kucheza kwa kukata viuno na pia kuvaa mavazi yanayowaonyesha wakiwa nusu uchi.
Alisema japokuwa kukata viuno ni asili ya mwafrika, lakini uvaaji wa mavazi ya nusu uchi si wa kistaarab, umepitiliza na unachangia kushusha hadhi ya muziki huo na kuufanya uonekane kuwa wa kihuni.
“Tatizo hili halipo kwenye muziki wa taarab pekee, hata hip hop na bongo fleva, utakuta wacheza shoo wamevalishwa nguo za nusu uchi. Mbona wanaume hawavai nguo za aina hiyo, wanawavalisha watoto wa kike?” Alihoji msanii huyo.
Amesema imefikia hatua hivi sasa, mzazi hawezi kutazama televisheni akiwa na watoto wake, vinginevyo analazimika kuwa na ‘remote’ mkononi ili kukitokea tukio la aibu, aweze kuzima televisheni mara moja ama kukimbilia nje ili kuepuka aibu.
Khadija amekiri kuwa umaarufu kwa wasanii ni mzuri, lakini wakati mwingine umekuwa ukiwasababishia madhara ya aina mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuzushiwa mambo ya uongo.
“Binafsi niliwahi kuzushiwa kwamba nimemuua mwanangu Omar Kopa kwa lengo la kujiongezea umaarufu baada ya kuonekana amenizima. Pia Leila Khatib alipokufa, niliambiwa kwamba mimi ndiye niliyemuua,”alilalamika.
Aliongeza kuwa, mbaya zaidi siku ambayo Leila alizikwa, hakuweza kuhudhuria kwenye mazishi kutokana na yeye kufiwa na bibi yake, hali iliyozidisha uvumi huo.
“Ukiwa msanii mzuri, unageuzwa kama malaika mtoa roho. Msanii mwenzako akiumwa, unaogopa hata kwenda kumuangalia,” alisema.
Khadija amekielezea kifo cha aliyekuwa mkurugenzi wa kikundi cha TOT Plus, Kepteni mstaafu, John Komba kuwa ni pigo kubwa katika fani ya sanaa nchini.
Amesema si rahisi kwa pengo la Kepteni Komba kuzibika kutokana na vipaji alivyokuwa navyo, isipokuwa anaweza kutokea msanii atakayeleta ahuni.
“Kuziba pengo lake si rahisi, litabaki kama lilivyo,”alisisitiza msanii huyo, ambaye ni mkurugenzi msaidizi wa TOT.

Miongoni mwa mafanikio ya Khadija kutokana na muziki huo ni pamoja na kutembelea nchi mbalimbali za Afrika, Ulaya na Marekani. Pia amefanikiwa kuanzisha kundi lake linalojulikana kwa jina la Ogopa Kopa Classic Music.
Moja ya malengo yake ni kurekodi upya nyimbo zake zote alizowahi kuziimba akiwa katika vikundi mbalimbali. Kikundi hicho kinaundwa na wasanii wasiozidi 10, akiwemo mtoto wake wa mwisho wa kiume, anayefahamika zaidi kwa jina la Black Kopa.
Iwapo mipango yake hiyo itafanikiwa, Khadija amesema anatarajia kuanzisha miradi mbalimbali ya kikundi kwa lengo la kuwaongezea wasanii mapato. Pia amepanga kuwashawishi wasanii wake wajiunge na mifuko ya hifadhi ya jamii ili kujiwekea akiba kwa maisha yao ya baadaye.
Khadija hakuwa tayari kuzungumzia kwa kirefu ndoa yake na mumewe, aliyefariki mwaka juzi mjini Bagamoyo, mkoani Pwani, ambaye inadaiwa alikuwa na umri mdogo kuliko yeye.
Alisema halikuwa jambo la ajabu kwake kuolewa na mwanaume mwenye umri mdogo kwa sababu hata Mtume Muhammad na mkewe Khadija, walifunga ndoa wakiwa wanatofautiana kwa miaka mingi.
“Mume wangu alikuwa anajua kunitunza. Nikienda kwenye maonyesho alikuwa akinifuata, tunarudi nyumbani pamoja, sijui kama naweza kumpata mume mwingine bora kama yeye. Kama atajitokeza, itabidi nimchunguze sana,”alisema Khadija huku akitabasamu.
Khadija ametoa mwito kwa wasanii wa muziki wa taarab kuwa na umoja kama ilivyo kwa wasanii wa muziki wa kizazi kipya, ikiwa ni pamoja na kurekodi nyimbo pamoja.
“Inasikitisha kuona sisi wasanii wa muziki wa taarab hatuna uwezo wa kufanya hivyo. Bongo fleva wanaungana na kuimba pamoja, lakini sisi hatuna uwezo huo. Mbaya zaidi hatuna mapromota na mameneja wa kutuvusha kutoka hapa tulipo,”alilalamika.

Wednesday, April 29, 2015

MZEE YUSSUF ASEMA YUKO TAYARI KUIMBA TAARAB NA DIAMOND

KIONGOZI wa kikundi cha muziki wa taarab cha Jahazi, Mzee Yussuf, amesema yuko tayari kuimba wimbo wa miondoko hiyo kwa kushirikiana na nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Naseeb Abdul 'Diamond'.

Mzee ameelezea msimamo wake huo baada ya Diamond kukaririwa na vyombo vya habari wiki iliyopita akisema kuwa, anataka kuimba wimbo wa taarab kwa kushirikiana na Mzee Yussuf.

"Nimepata taarifa kwamba Diamond anataka kuimba taarab na mimi. Mi nasema nipo tayari kufanya hivyo wakati wowote,"alisema Mzee, ambaye pia anajulikana kwa jina la 'Mfalme'.

Nyota huyo wa taarab alisema kwa kipindi cha miaka 11, ambacho amekuwa akijihusisha na muziki huo, amefanya mambo mengi katika kuutangaza ndani na nje ya nchi na pia kuibua vipaji vya wasanii mbalimbali.

"Katika kipindi cha miaka 11 iliyopita, nimefanya mambo mengi na kuwatoa wasanii wengi mpaka leo hii naitwa mfalme,"alisema Mzee, ambaye ameoa wake wawili, akiwemo Leila Rashid, ambaye ni miongoni mwa waimbaji nyota wa Jahazi.

"Leo hii hakuna asiyemfahamu Isha Mashauzi, Thabiti Abdul, Ally J na wengineo. Wote hao ni matunda yangu,"alisema msanii huyo wa zamani wa vikundi vya East African Melody na Zanzibar Stars.

Mzee alisema si kweli kwamba alipanga kustaafu muziki huo mwaka huu, kama alivyonukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari. Alisema atafanya hivyo baada ya kuuweka muziki wa taarab kwenye chati ya juu.

Alisema alichomaanisha ni kwamba akitoa wimbo mpya, ndio utakuwa wa mwisho na hatoimba tena zaidi ya kuendelea kuwa mtunzi na shughuli zingine za nyuma ya muziki.

“Nilisema nitakapoimba wimbo mwingine, utakuwa wa mwisho sitaki tena kuimba, nimeshachoka kuimba,” alisema Mzee.

Alidai kuwa alianza muziki tangu mwaka 1997, lakini alianza kuimba mwaka 2004 na muda huo alikuwa akitunga nyimbo za watu wengine.

“Mimi kwenye bendi sifanyi kitu kimoja, natengeneza nyimbo za watu wote, napiga vinanda,” alisema.

Kwa upande wake, Diamond alisema anafikiria kujitosa katika muziki wa taarab baada ya kupata mafanikio makubwa katika muziki wa taarab.

Diamond alisema amefikia uamuzi huo kutokana na kuvutiwa na muziki huo wa taarab, ambao pia ni maarufu kwa jina la mipasho.

Kauli hiyo ya Diamond ilikuja siku chache baada ya kuibuka na kibao kipya cha miondoko ya mduara, akimshirikisha malkia wa taarab nchini, Khadija Kopa.

Mshindi huyo wa tuzo mbalimbali za muziki za Kilimanjaro amesema, anajua uamuzi wake huo utawashangaza mashabiki wengi, lakini ni jambo la kawaida kwa msanii.

Diamond alisema hadi sasa anaamini hana mpinzani katika muziki wa kizazi kipya na hakuna msanii anayeweza kufikia kiwango chake hapa nchini.

“Najua watu watanishangaa na kuniona mtu wa ajabu, lakini nimefanya hivyo kwa sababu sina mpinzani katika muziki wa kizazi kipya,”alisema.

Diamond alisema ameamua kupiga miondoko tofauti ya muziki kutokana na kipaji alichonacho katika fani hiyo, ambayo imempatia umaarufu mkubwa kimataifa na kumwezesha kutembelea nchi kadhaa za Ulaya.

Kutokana na kipaji chake hicho, Diamond alisema hakuna kitu anachoshindwa kukifanya katika muziki.

“Bado sijaanza rasmi kupiga muziki wa taarab, ninachokifanya kwa sasa ni kufanya tathmini ya soko lake ili kuona kama unaweza kuniletea mafanikio kama ilivyo kwa muziki wa bongo fleva,”alisema msanii huyo.

“Naweza kufanya kila aina ya muziki kwa sababu nina kipaji cha kuimba nyimbo aina zote, hivyo endapo nitafikia muafaka, naweza kufanya kitu hicho ingawa mashabiki wangu watashtuka sana,” alisema.

Diamond alikiri kuwa, muziki wa kizazi kipya umemfanya ajulikane sehemu nyingi duniani, ikiwa ni pamoja na kupata manufaa mbalimbali kimaisha kwa kuishi kwenye nyumba nzuri na kumiliki magari ya kifahari.

Msanii huyo mwenye haiba ya kuvutia alisema, kwake muziki ni kazi kama zilivyo kazi zingine hivyo amekuwa akifanya kazi zake kwa malengo.

Alisema siri kubwa ya muziki wake kuwateka mashabiki wengi ndani na nje ya nchi ni kufanyakazi zake kwa kujituma na pia kujiwekea malengo.

"Sifanyi muziki kwa ajili ya kujifurahisha, kutafuta pesa na kuwaacha mashabiki wangu wabaki na kiu ya burudani,”alisema Diamond.

“Ninapofanya muziki nahakikisha kuwa, nakata kiu ya mashabiki wangu kwa kuwapa burudani wanayoihitaji,”aliongeza.

Katika kufanikisha hilo, Diamond alisema amekuwa na utaratibu wa kushirikiana na watu mbali mbali kwa vile anaamini sio rahisi kuweza kufanya kila kitu peke yake.

Alisema miongoni mwa watu, ambao wamekuwa wakimpa ushirikiano mkubwa katika kazi zake ni wacheza shoo kwa vile wamekuwa wakibuni vionjo vipya kila kukicha.

"Siwezi kuwa na ubahili ninapofanya kazi na hili ndilo lililonifanya nizidi kusonga mbele katika kazi ya muziki. Ili upate ni lazima utoe na ili uwafurahishe mashabiki wako ni lazima uzingatie kanuni hizo,”alisema.

MASHAUZI: NYIMBO ZANGU ZA DANSI ZIMEPOKELEWA VIZURI

MTUNZI na mwimbaji nyota wa muziki wa taarab nchini, Isha Ramadhani 'Mashauzi' amekiri kuwa, uamuzi wake wa kuimba nyimbo za miondoko ya dansi umepokelewa vizuri na mashabiki wake.

Isha, ambaye kwa sasa anamiliki na kuliongoza kundi la taarab la Mashauzi Classic, amesema amekuwa akipata pongezi nyingi kutoka kwa mashabiki baada ya kurekodi nyimbo hizo.

Nyimbo hizo, ambazo zimekuwa zikipigwa mara kwa mara kwenye vituo mbalimbali vya redio na televisheni nchini ni 'Nimlaumu Nani' na 'Nimpe Nani'.

"Wapo wanaonisifia na wanaonibeza kutokana na uamuzi wangu huo. Lakini binafsi nampenda sana mtu anayesema ukweli kutoka moyoni mwake,"alisema Isha alipokuwa akihojiwa na kituo kimoja cha televisheni nchini.

Ameongeza kuwa kila kundi lake la Mashauzi Classic linapofanya maonyesho kwenye kumbi za burudani, mashabiki wamekuwa wakimuomba aimbe nyimbo hizo na kuzifurahia.

Kutokana na mafanikio hayo, Isha amesema anatarajia kurekodi albamu yake binafsi yenye nyimbo sita za muziki wa dansi.

"Nataka kuwapa mashabiki burudani yenye vionjo tofauti," alisisitiza mwanamama huyo mwenye mwili tipwatipwa, lakini anayejituma katika kulishambulia jukwaa kwa minenguo yake maridhawa na murua.

Isha amesema katika nyimbo zake mbili za awali za miondoko hiyo, ameimba sauti zote pekee yake baada ya kutengenezewa 'mipigo' ya ala katika studio za Gift.

"Nilimfuata prodyuza na kumuomba anitengenezee 'beats' za wimbo wa kwanza wa Nimlaumu nani, akanitengenezea beats mbili. Niliporejea nyumbani, nikaanza kutengeneza mashairi.

"Kesho yake nikaenda studio na kuanza kuurekedi. Ajabu ni kwamba baadhi ya mashairi yalinijia nikiwa studio, tofauti na yale niliyokuwa nimeyaandaa. Lakini mwisho wa siku ukatoka wimbo mzuri,"alisema mwanamama huyo, ambaye ni shabiki mkubwa wa klabu ya Yanga.

Isha amesema amekuwa na uhusiano mzuri na wasanii wa muziki wa kizazi kipya nchini, na baadhi yao wamekuwa wakimkubali kutokana na umahiri wake wa kuimba nyimbo za miondoko tofauti.

Wednesday, March 18, 2015

JAHAZI, MASHAUZI CLASSIC KAZI IPO MACHI 22



Hatimaye wakurugenzi wa Mashauzi Classic na Jahazi Modern Taarab, wamefanya mkutano na waandishi wa habari na kuthibitisha kuwepo kwa onyesho la pamoja la makundi hayo yenye nguvu katika muziki wa taarab.

Onyesho hilo litafanyika Jumapili, Machi 22, mwaka huu, ndani ya ukumbi wa Travertine, Magomeni, Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Jahazi, Mzee Yussuf na Mkurugenzi wa Mashauzi Classic, Isha Ramadhani maarufu kama Isha Mashauzi, wamesema siku hiyo hatumwi mtoto dukani.

Wakiongea katika mkutano huo na waandishi wa habari uliofanyika Jumatatu iliyopita katika hotel ya Travertine, wakurugenzi hao, ambao wote ni waimbaji nyota, walisema onyesho hilo si mpambano,
bali si la masihara kwani kila bendi imejipanga kuhakikisha inaangusha burudani iliyokwenda shule.

Saturday, February 14, 2015

ISHA MASHAUZI AIBUKA NA KITU KINGINE KIPYA


Wala hakosei kusema ‘kujua kazi ni raha’.

Isha Mashauzi anakushukIa tena kivingine na wimbo mpya kabisa “Nimpe Nani” unaodhihirisha kuwa anaijua vema kazi yake.

Hii ni ‘single’ yake ya pili nje ya taarab ukiacha ule wa kwanza “Nimlaumu Nani” uliopigwa katika miondoko ya rhumba.

“Nimpe Nani” ni wimbo unaoelea kwenye miondoko ya zouk rhumba lakini ukikolezwa kwa mbali na vionjo vya mduara.

Wimbo huo wa dakika tatu na nusu umerekodiwa katika studio za C9 Records chini ya producer C9 Kanjenje.

Kinanda kimepigwa na Kali Kitimoto na C9, magitaa ya bass na solo yamepigwa na Babu Bomba wa Malaika Band.

Sauti zote tamu unazozisikia humo ni za Isha Mashauzi kasoro sehemu ndogo sana isiyozidi sekunde 5 iliyotikiwa na Easy Man.

Tuesday, February 3, 2015

THANIA MSOMALI AJA NA 'HIVI NDIVYO NILIVYO'



MIEZI michache baada ya kujiengua katika kundi la Mashauzi Classic, mwimbaji machachari na mwenye sauti maridhawa ya ndege mnana, Thania Msomali ameibuka na kibao kipya kinachokwenda kwa jina la Hivi ndivyo nilivyo.

Katika kibao hicho, ambacho kimeshaanza kuteka hisia za mashabiki, Thania anasimulia jinsi alivyo na kwamba yuko tofauti na vile watu wanavyomfikiria.

Thania alianza kung'ara kimuziki alipokuwa katika kundi la Five Stars, baadaye akajiunga na kundi la T-Moto kabla ya kutua Mashauzi Classic, kundi linaloongozwa na Isha Ramadhani 'Mashauzi'.

Binti huyo jamali na mwenye sauti murua na adhimu, anakiri kuwa kipaji chake kiligunduliwa na mpiga kinanda Omary Kisira, ambaye ndiye aliyempika na kumfanya awive kisawasawa.

Thania alijiengua mwenyewe kutoka kundi la Mashauzi Classic baada ya kuona kwa sasa anaweza kusimama peke yake.

Binti huyo amesema kibao hicho ni maandalizi ya ujio wa albamu yake ya kwanza, anayotarajia kuitoa mwaka huu.

Amesema alianza maandalizi ya kutoa albamu mpya muda mrefu uliopita, lengo likiwa ni kutoa kitu kilichokamilika na chenye ladha isiyomithilika kwa utamu.

"Sikukurupuka kurekodi kibao hiki, nilijiandaa vyema ikiwa ni pamoja na kufanya mazoezi ya kutosha,"alisema.

Thania kama msanii mchanga, amekubaliana na changamoto zote atakazokumbana nazo, pia anawasihi wasanii wote kupendana na kusaidiana pale unapoona mwenzako amekwama au anakwenda sivyo, hata mawazo tu.

"Napenda kuwashukuru wale wote waliofanikisha kwa mimi kuwepo hapa nilipo:- Walimu wangu Fikirini Urembo na Kibibi Yahaya, vilevile nitakuwa mwizi wa fadhila kukosa kutoa shukrani zangu kwa walimu wangu waliopita ambao ni Ally Jay, Shaibu wa Mwamvita pamoja na Kali Kiti Moto Mafya.

"Pongezi kubwa ziwaendee Amin Salmin, Mkurugenzi wa T-Moto pamoja na Ismail Suma Ragger, Meneja wa Mashauzi Classic.

Amewaomba wapenzi wote wa taarab kumpokea na wausikilize kwa makini wimbo wake huo ili wajue kaimba nini na zaidi ya yooote, huu ni mwanzo tu, yaani mvua za rasharasha masika inakuja, ni mvua ya mawe kama si elnino.

WAKALI WAO MODERN TARADANSI WAJA NA VIBAO VIWILI VIPYA, MISAMBANO ASHUSHA MOJA KALI



KUNDI jipya la muziki wa taarab la Wakali Wao Modern Taradansi, limeibuka na vibao vingine viwili vipya.

Vibao hivyo, ambavyo tayari vimeshaanza kusikika kwenye vituo mbalimbali vya redio nchini ni Kumbe ndio tabia yake na Jasho la mnyonge hulipwa na Mola.

Kibao cha Kumbe ndio tabia yako kimeimbwa na mwanadada Nasra Shaaban wakati kibao cha Jasho la mnyonge hulipwa na Mola kimeimbwa na kiongozi wa kundi hilo Thabit Abdul.

Akizungumza na mtandao huu wiki hii, Thabit alisema ujio wa vibao hivyo viwili ni maandalizi ya ujio wa albamu yao mpya, inayotarajiwa kutoka hivi karibuni.

Alisema tayari wameshakamilisha vibao viwili na kwamba vingine vitatu bado vipo jikoni na vinatarajiwa kupakuliwa hivi karibuni.

Thabit alisema kama ilivyo kawaida, wamepiga vibao hivyo kwa miondoko ya taarabu ya kisasa kwa lengo la kuwavutia zaidi mashabiki.

Wakati huo huo, mkali wa miondoko ya taarab, Abdul Misambano naye ameibuka na kibao kipya kinachokwenda kwa jina la Sio mie ni moyo.

Tuesday, January 13, 2015

ONYESHO LA MIAKA 51 YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (wa pili kulia) akiwa na Waziri wa Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo, Said Ali Mbarouk (kulia) Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda (kushoto) na Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Abdalla Mwinyi Khamis.
 Mke wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Pili Seif Iddi (kulia) akiwa na Waziri wa Kilimo na Maliasili, Dk. Sira Ubwa Mamboya
 Baadhi ya wananchi na mashabiki wa Taarab waliohudhuria katika hafla ya Taarab hiyo ya kusherehekea miaka 51 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar
 Mwimbaji wa Kikundi cha Taifa cha Culture Musical Club, Mtumwa Mbarouk akiimba wimbo wa "Mpewa hapokonyeki" wakati wa taarab rasmi ya kusherehekea miaka  51 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar
 Waimbaji wa  Kikundi cha Taifa cha Culture Musical Club, Asha Alli  na Khamis Nyange, wakiimba wimbo wa Miaka 51 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar, uliotungwa na Profesa Gogo
Mwimbaji wa Kikundi cha Taifa cha Culture Musical Club, Saada Mohammed akiimba wimbo unaosema  "kweli nnae" wakati wa taarab rasmi ya kusherehekea miaka  51 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar, mbele ya mgeni rasmi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein jana katika ukumbi wa Salama Bwawani Hotel Mjini Unguja [Picha na Ikulu]

Monday, January 5, 2015

OGOPA KOPA ILIVYOPAGAWISHA MASHABIKI DAR LIVE

 Malkia wa Mipasho nchini, Khadija Omar Kopa akiimba kwa hisia wakati wa onyesho hilo
 Waimbaji wa Ogopa Kopa wakiwajibika jukwaani wakati wa onyesho hilo
 Mtoto wa Khadija Kopa aitwae Mohammed Kopa akikamua huku nyuma yake akisapotiwa na wenzake
 Mkali wa miondoko ya Kigodoro, Msaga Sumu, akivamia jukwaa na kuwainua mashabiki waliokaa vitini
 Msaga Sumu akimpelekesha Khanifa Khalid anayeserebuka kwa staili ya gwaride
 Malkia wa Mipasho, Khadija Kopa (kulia) na Khanifa Khalid wakikamua
 Aziza Kimodo akifanya makamuzi wakati wa onyesho hilo
Shad Chotara, mmoja wa waimbaji wa Ogopa Kopa akishusha mpasho wake mpya

ISHA MASHAUZI KUREKODI WIMBO WA MCHIRIKU


Baada ya kutesa na wimbo wake wa rhumba “Nimlaumu Nani” Isha Mashauzi sasa anajiandaa kuachia ‘single’ nyingine, safari hii ikiwa katika miondoko ya mchiriku.

Akiongea na Saluti5, Isha alisema wimbo huo utakwenda wa jina la “Ado Ado” na utarekodiwa wiki hii kabla ya kauchiwa redioni mwishoni mwa mwezi huu.

“Ni ngoma ya dakika nne ambayo sina shaka kuwa itakimbiza ile mbaya,” alisema Isha.

Isha amesema baada ya kauchia mchiriku, ataachia wimbo mwingine ambao uko katika miondoko ya mutwashi, wimbo ambao umepewa jina la “Usisahau”.

“Lengo langu ni kutoa albam yenye jumla ya nyimbo sita ambayo itakuwa nje kabisa ya miondoko ya taarab, alisema Isha na kuongeza: “Nataka kudhihirisha kuwa nina uwezo wa kuimba aina yoyote ya muziki.”