KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Saturday, August 11, 2012

MZEE YUSUPH AMZAWADIA ISHA MASHAUZI PIPI YA KIJITI

SHANGWE, vifijo, hoihoi na nderemo vilitawala mwishoni mwa wiki iliyopita wakati vikundi vya taarab vya Jahazi na Mashauzi Classic vilipofanya onyesho la pamoja.
Onyesho hilo la aina yake, lilifanyika katika ukumbi wa hoteli ya Travertine uliopo Magomeni mjini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na mashabiki lukuki.
Kivutio kikubwa katika onyesho hilo walikuwa kiongozi wa Jahazi, Mzee Yussuf ‘Mfalme’ na kiongozi wa Mashauzi Classic, Isha Mashauzi ‘Jike la Simba’.
Isha, ambaye ni mwimbaji mashuhuri wa nyimbo za taarab, alitumia onyesho hilo kumuomba radhi Yussuf kutokana na kitendo chake cha kujiengua katika kundi hilo bila kuaga.
Baada ya kujiengua katika kundi la Jahazi, Isha ambaye alikuwa miongoni mwa waimbaji tegemeo na kipenzi cha mashabiki wengi wa kundi hilo, alianzisha kundi lake la Mashauzi Classic.
Mashabiki walianza kufurika kwenye ukumbi huo kuanzia saa tatu usiku na hadi ilipotimia saa nne, walifurika pompni. Kundi la Jahazi lilikuwa la kwanza kupanda stejini na kuanza kutoa burudani.
Kama kawaida yake, kundi hilo lilianza kuporomosha nyimbo zake mpya na zile zinazotamba katika viunga vya burudani hivi sasa na kuwafanya mashabiki kuachia viti vyao na kujimwaga ukumbini kucheza.
Ilipotimia saa sita usiku, ndipo kundi la Mashauzi Classic lilipopanda stejini na kuanza kutoa burudani kwa mashabiki.Ni wakati huo, mwimbaji tegemeo wa kundi hilo, Mashauzi alipopanda stejini na kushangiliwa kwa mayowe mengi na mashabiki.
Akiwa stejini, Mashauzi alimwomba Yussuf ampatie zawadi aliyomuandalia. Kupanda jukwaani kwa Yussuf kuliamsha shangwe na nderemo katika ukumbi huo, ambapo Isha alipata nafasi ya kuzungumza na kiongozi huyo wa Jahazi.
Kabla ya Isha kusema lolote, Yussuf alitoa pipi ya kijiti na kumkabidhi mwimbaji huyo, aliyemlea katika medani ya muziki wa taarab.
"Siku zote zawadi ya mtoto ni pipi, kwa hiyo nakukabidhi zawadi yako mwanangu, nadhani umeipenda," alisema Yussuf huku akishangiliwa na mashabiki wengi.
Isha alipokea zawadi hiyo kwa heshima na kusema amefarijika na ameipokea kwa mikono miwili.
"Nakushukuru baba yangu kwa zawadi uliyonipatia, nimeipokea kwa mikono miwili na roho safi. Siku zote zawadi ya mtoto huwa pipi kwa hiyo nimeipokea," alisema.
Kwa mujibu wa Isha, hana ugomvi na Yussuf wala mwimbaji yeyote wa kundi la Jahazi na kuahidi kutoa ushirikiano wa hali na mali kwa kundi hilo linalosadikiwa kuwa na mashabiki wengi hapa nchini.
Alisema aliondoka katika kundi hilo kwa ajili ya kwenda kutafuta maisha na kwamba muda wowote anaweza kurudi na anaamini hawezi kuzuiliwa na mtu yoyote. Isha aliambatana na mama yake mzazi, Rukia Juma.
"Niliondoka kwenda kutafuta maisha, lakini muda wowote maisha yakinishinda, nitarejea nyumbani. Ng'ombe akivunjika mguu malishoni, hurejea zizini kusaidiwa," alisema.
Kwa upande wake, Yussuf alimuhakikishia muimbaji huyo kwamba Jahazi ni nyumbani kwake na anaweza kurejea wakati wowote atakapojisia kufanya hivyo.
"Mtu kwao anaweza kuondoka na kurudi wakati wowote na wewe unaweza kurudi wakati wowote unapohitaji kurudi, karibu na nitakupokea kwa mikono miwili," alisema.
Yussuf alisema amefarijika mno kumuona mtoto wake aliyemfundisha muziki anakiri kosa na kuomba radhi hadharani bila ya kushinikizwa na mtu yoyote.
Alisema kitendo alichofanya muimbaji huyo ni cha kiungwana na kinahitaji kuigwa na wasanii wengine na kwamba ni wachache wenye moyo kama wa Isha.
Yussuf alimpa ofa maalumu muimbaji huyo ambapo alimwambia atakuwa miongoni mwa watakaomsindikiza katika uzinduzi wa albamu mpya ya Jahazi ya 'Mpenzi Chokleti' itakayozinduliwa Desemba 24, mwaka huu.
Baada ya Isha kutoa maneno mafupi ya kumuomba radhi kiongozi huyo wa Jahazi, alimkabidhi zawadi maalumu ya ngao iliyochorwa kwa ustadi mkubwa.
Ngao hiyo ina nembo ya kundi la Jahazi, picha ya Yussuf na Isha huku maandishi yake yakiwa na ujumbe mbalimbali.
Tukio lililowavutia mashabiki wengi katika usiku huo maalumu uliopewa jina la 'Usiku wa baba na mwana' ni pale Isha alipopanda jukwaani akiwa amevalia jezi za timu ya Yanga.
Muimbaji huyo alisema ameamua kuvaa jezi za klabu hiyo kwa sababu ya kusherehekea ushindi wa Yanga dhidi ya Simba na pia kumpongeza Yussuf, ambaye ni mjumbe wa kamati ya utendaji ya klabu hiyo.
"Kwa vile baba yangu ni Yanga, nimeamua kuvaa jezi za klabu ya baba yangu kuonyesha mapenzi niliyonayo kwake. Yanga oyeeeeeee," alisema.
Wimbo wa 'Mpenzi Chokleti' ulioimbwa na Yussuf ndio uliofunika katika onyesho hilo na kuacha gumzo kwa mashabiki kutokana na kupangiliwa sauti na ala kwa utaalamu mkubwa.

No comments:

Post a Comment