KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Saturday, August 11, 2012

BANZA STONE AJA NA KIBAO KIPYA CHA TAARAB


MWIMBAJI na mtunzi mahiri wa nyimbo za muziki wa dansi nchini, Ramadhani Masanja ‘Banza Stone’ ameingia studio kurekodi kibao chake cha pili cha taarab.
Banza, ambaye kwa sasa ni mwanamuziki wa bendi ya Extra Bongo, alitarajiwa kuingia studio jana kurekodi wimbo huo chini ya usimamizi wa Thabiti Abdul.
Kibao hicho cha Banza kinajulikana kwa jina la Play Boy na kinatarajiwa kuanza kusikika hewani hivi karibuni.
Huo utakuwa wimbo wa pili kwa Banza baada ya kung’ara katika wimbo wake wa kwanza wa ‘Kuzaliwa mjini’, ambao pia ulitungwa na Thabit, ambaye ni mmoja wa wakurugenzi wa kikundi cha Mashauzi Classic.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Thabiti alisema ni kweli ameamua kumtungia Banza wimbo mwingine wa taarab baada ya kupata hamasa kutoka kwa mashabiki wa muziki huo.
“Mashabiki wengi walikuwa wanataka Banza aendelee kuimba nyimbo za taarab. Wamekuwa wakinilaumu kwa kumweka kimya kwa muda mrefu,”alisema Thabiti.
“Nami nimeona ni kweli, kwa vile wimbo wa Kuzaliwa mjini ulipokelewa vyema na mashabiki, ni vyema aendelee kuimba taarab,”aliongeza.
Mbali na kusumbuliwa na mashabiki, Thabiti alisema Banza mwenyewe naye amekuwa akimpigia simu mara kadhaa akimuomba amtungie wimbo mwingine wa taarab.
“Banza mwenyewe alikuwa akinisumbua, anasema nilipomtungia wimbo wake wa kwanza, nilikuwa kama nimembeeb, hivyo anataka aendelee kuimba taarab,”alisema Thabiti.
Kwa mujibu wa Thabiti, wimbo wa Kuzaliwa mjini, aliutunga miaka sita iliyopita, lakini hadi sasa bado unawavutia mashabiki wengi kutokana na maudhui ya wimbo na mipigo ya ala.
Banza amewahi kupigia bendi mbalimbali za muziki wa dansi nchini, lakini iliyomweka kwenye chati ya juu kimuziki ni Twanga Pepeta International.
Baadaye alijiunga na bendi ya TOT Plus, ambayo aliiongoza kwa miaka takriban mitano kabla ya kuanzisha bendi yake binafsi ya Bambino Sound.
Mtunzi huyo mahiri wa nyimbo za muziki wa dansi pia aliwahi kuimbia bendi ya Twanga Chipolopolo na Rufita Jazz kabla ya kujiunga na Extra Bongo, inayoongozwa na Ally Choki.
Ndani ya bendi hiyo, Banza amekuwa akitamba na kibao chake kinachojulikana kwa jina la Falsafa ya Maisha. Pia amekuwa akiimba nyimbo alizowahi kutamba nazo katika bendi mbalimbali.
Hivi karibuni, msanii nyota wa muziki wa kizazi kipya, Hamisi Ramadhani H-Baba aliamua kumshirikisha Banza kurekodi wimbo wake mpya wa Sina Raha. Kibao hicho kimo kwenye albamu mpya ya msanii huyo inayojulikana kwa jina la Shika hapa, acha hapa.

No comments:

Post a Comment