KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Saturday, August 11, 2012

TAARAB YA SASA BIFU TUPU-KHADIJA KOPA

MTUNZI na mwimbaji nyota wa muziki wa taarab nchini, Khadija Omar Kopa amesema vikundi vya muziki huo kwa sasa vimetawaliwa na chuki binafsi miongoni mwa viongozi wake.
Khadija amesema chuki hizo pia zimetawala miongoni mwa wasanii, ambao baadhi yao wamekuwa hawaelewani na kuchukiana kwa sababu zisizokuwa na msingi.
Mwanamama huyo, ambaye ni kiongozi wa kikundi cha taarab cha Tanzania One Theatre (TOT), alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita alipokuwa akihojiwa katika kipindi cha Jambo Tanzania kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha TBC 1.
“Bifu la sasa ni bifu kweli kweli, sio la kutungiana nyimbo tu, utakuta kikundi fulani cha taarab hakielewani na kikundi kingine na hata wasanii wake nao hawaelewani, ‘ alisema.
Khadija alisema bifu la aina hiyo kamwe haliwezi kuleta maendeleo ya muziki huo, badala yake litaufanya muziki huo udumae na kupoteza umaarufu kwa mashabiki.
Alisema wakati vikundi vya TOT na Muungano vilipokuwa kwenye chati ya juu miaka ya 1990 hadi mwanzoni mwa 2000, viongozi na wasanii wake walikuwa na uhusiano mzuri na wa karibu na kamwe hawakuwa na bifu.
Alisema bifu la vikundi hivyo wakati huo lililenga kutafuta pesa na kuviletea maendeleo, halikuwa bifu la kuchukiana na kujengeana uhasama kama ilivyo sasa kwa baadhi ya vikundi vya muziki huo.
“Wakati ule tulikuwa tunatunga nyimbo za kujibishana, lakini lengo letu lilikuwa ni kutafuta pesa,”alisema Khadija, ambaye ni miongoni mwa waimbaji wakongwe wa muziki huo wanaotesa hadi sasa.
Khadija alisema ilikuwa kawaida ya vikundi hivyo viwili vilivyokuwa vikiongozwa na John Komba na Norbert Chenga kuandaa maonyesho makubwa ya taarab na kuhudhuriwa na mashabiki wengi kuliko hivi sasa.
Alisema waliweza kufanya maonyesho ya aina hiyo katika viwanja vikubwa kama vile wa Uhuru, Dar es Salaam, Jamhuri-Morogoro na ukumbi wa Vijana-Dar es Salaam, ambapo walipata pesa nyingi.
“Katika baadhi ya maonyesho, tuliweza kupata shilingi milioni 30 kwa onyesho moja na kwa wakati ule zilikuwa pesa nyingi sana,”alisema mwanamama huyo.
Khadija alisema baadhi ya wakati, Komba na Chenga walipoona kikundi kimoja kikitetereka kimuziki, walikuwa wakikutana na kupanga mikakati ya kukiinua.
“Mbinu walizokuwa wakizitumia kuinuana ni kuandaa kitu fulani cha pamoja na kutoleana lugha za kiushindani, zisizokuwa na matusi na mashabiki walikuwa wakishawishika kirahisi kujitokeza kuhudhuria maonyesho yetu,”alisema.
Licha ya kikundi cha TOT kutosikika sana kwa sasa kama ilivyokuwa miaka ya nyuma, Khadija bado anang’ara kimuziki kutokana na tungo zake mbalimbali, ambazo zimetokea kuteka hisia za mashabiki wa muziki huo. Baadhi ya tungo hizo ni kama vile Top in town.
Akizungumzia utunzi wa nyimbo za taarab, Khadija alikiri kuwa ni kazi ngumu na inayohitaji uvumilivu na kujituma. Alisema binafsi amekuwa akitunga nyimbo zake nyingi nyakati za usiku.
“Ninapoamua kutunga wimbo, huwa nakesha usiku kucha nikiandika mashairi. Naandika, nafuta, naandika tena hadi alfajiri,”alisema.
Aliongeza kuwa, kazi ya kutia muziki katika nyimbo zake huwa sio ngumu kwa vile huwaelekeza wapigaji wa ala upigaji anaoutaka nao hufanya hivyo.
Hata hivyo, Khadija alisema wakati mwingine anapokuwa stejini, hufanya vitu tofauti na alivyourekodi wimbo wake kutokana na kupandwa na mzuka.
Khadija alianza kupata umaarufu alipokuwa katika kikundi cha Culture cha Zanzibar, ambako aling’ara na vibao vyake kama vile Wahoi, Daktari na Kadandie.
Baadaye alihamia Bara, ambako alijiunga na kikundi cha TOT wakati kilipoanzishwa mwaka 1993 kabla ya kuwa miongoni mwa waanzilishi wa kikundi cha East African Melody. Pia aliwahi kuimbia kikundi cha Muungano.

No comments:

Post a Comment