KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Saturday, August 11, 2012

MWANAHAWA ALLY AJIENGUA T-MOTTO, AREJEA EAST AFRICAN MELODY


MWIMBAJI mkongwe wa muziki wa taarab nchini, Mwanahawa Ally amesema katika maisha yake ya usanii, hajawahi kutunga wimbo wa taarab.
Mwanahawa (61) amesema hajawahi kufanya hivyo kwa sababu utunzi wa nyimbo za taarab ni kazi ngumu na inahitaji kuwa na kipaji cha aina yake.
Mkongwe huyo wa taarab alisema hayo wiki hii alipokuwa akihojiwa katika kipindi cha Raha Zetu kilichorushwa hewani na kituo cha redio cha Clouds.
“Kutunga wimbo ni kazi ngumu, tofauti na watu wanavyofikiria kwani nyimbo nzuri ni lazima iwe na mashairi yenye vina vinavyolingana,”alisema mwanamama huyo.
“Tangu nianze kuimba taarab huu ni mwaka wa 45 na sijawahi kutunga nyimbo yangu mimi mwenyewe. Natungiwa tu na watu wengine, siwezi hata kujaribu, mashairi yana kazi ngumu,” aliongeza.
Mwanahawa, ambaye kwa sasa anafanyakazi katika kikundi cha East African Melody, amesema amerejea kikundi hicho baada ya kushindwa kuelewana na uongozi wa T Motto.
Alisema ameamua kujiondoa T Motto kwa hiari yake baada ya kuona mkurugenzi wake, Amin Salmin ameshindwa kukiendesha kwa mafanikio.
“Wakati waliponifuata, walinieleza kwamba nitalipwa shilingi milioni mbili na kusaini mkataba wa mwaka mmoja, lakini hadi sasa sijui kama huo mkataba uliandikwa na sijawahi kulipwa mshahara wowote,”alisema.
“Nasikia tu matangazo ya redio na televisheni yakieleza kwamba nipo T Motto, lakini sijawahi kumuona mkurugenzi wake hata siku moja na sidhani kama anafahamu nina shida gani,”aliongeza.
Mwanahawa alisema, anahisi kundi hilo lilitaka kuleta ushindani katika muziki wa taarab, lakini halikuwa limeandaliwa vyema ama kujipanga vizuri.
Alisema tangu aliporekodi wimbo mmoja na kundi hilo na kushiriki kwenye uzinduzi, hajawahi kuitwa kwenye onyesho lolote na haelewi iwapo bado lipo ama limekufa.
Mkongwe huyo amewahi kuimbia vikundi mbalimbali vya taarab kama vile Jahazi, Five Stars, Zanzibar Stars na East African Melody.

No comments:

Post a Comment