KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Tuesday, February 19, 2013

FIVE STARS MODERN TAARAB CHASUKWA UPYA



KIKUNDI cha taarab cha Five Stars kimewanyakua nyota wapya wa muziki huo kutoka katika vikundi mbalimbali kwa lengo la kujiimarisha.

Miongoni mwa wasanii hao wapya ni pamoja na waimbaji wakongwe, Mwanahawa Ally, Sabah Salum, Maua Tego, Mosi Suleiman na mpiga kinanda Thabiti Abdul.

Mbali na kuajiri nyota hao, kundi hilo pia limeupiga chini uongozi wote wa zamani na kuweka viongozi wapya.

Kwa sasa, kundi hilo ambalo lilitamba vilivyo mwaka juzi kabla ya wasanii wake 14 kufariki dunia kwa ajali ya gari, lipo chini ya mkurugenzi, Maalim Sharrif Mambo maarufu kwa jina la Shacks.

Wasanii wa zamani wa kundi hilo waliofariki dunia kwa ajali ni Issa Kijoti, Sheba Juma, Tizzo Mgunda, Omary Hashim, Omary Haji, Hajji Mzania, Nassoro Madenge, Husna Mapande, Hamisi Omary, Maimuna Makuka, Hassan Ngeleza, Ramadhani Maheza na Ramadhani Mohamed.

Kiongozi wa kundi hilo, Ally J aliwaambia waandisi wa habari mjini Dar es Salaam jana kuwa, wameamua kulisuka upya kundi hilo ili kuhimili ushindani wa taarab uliopo sasa.

Wasanii wengine wapya waliojiunga na kundi hilo ni Jumanne Ulaya, Yussuf Tego, Mariam Mohamed, Mariam Omary na Hammer Q.

Jay alisema wasanii hao wameingia mkataba wa miaka miwili na Five Stars kila mmoja na kundi hilo linatarajiwa kuingia kambini wakati wowote kwa ajili ya kuandaa albamu mpya.

Kwa upande wake, Shacks alisema kundi lake halina uhasama na kundi lolote na kwamba ujio wao umelenga kuongeza ushindani katika muziki wa taarab na kusaka fedha kwa kutoa vitu vya uhakika.

Alisema tayari wamefanya makubaliano na Jahazi Modern Taarab ili kutochukuliana wasanii. Katika makubaliano hayo, viongozi wa makundi hayo mawili hawatapokea msanii kutoka kundi lingine.

Mbali na kuingia mkataba huo, Shacks alisema makundi hayo mawili yamekubaliana kushirikiana katika kuendeleza muziki wa taarab.

Friday, February 15, 2013

MASHAUZI CLASSIC WAKIWA KAZINI

AISHA Othman wa kundi la Mashauzi Classic akikamua jukwaani wakati wa onyesho lililofanyika kwenye ukumbi wa Mango Garden, Kinondoni, Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita.
ISHA Mashauzi akiwajibika jukwaani wakati wa onyesho hilo

SHABIKI huyu akiwa amepagawa kutokana na utamu wa sauti ya Isha Mashauzi

SAIDA Mashauzi akituzwa na mashabiki wakati wa onyesho hilo

SAIDA Mashauzi akiimba kwa hisia kali, akilalamikia penzi

MASHAUZI APATA KITAMBULISHO CHA UTAIFA

 
 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Ali Mohamed Shein,akiwa katika picha na msanii wa muziki wa Taarab, Aisha Mashauzi, baada ya kumkabidhi kitambulisho cha Taifa, wakati wa uzinduzi wa zoezi la kukabidhi vitambulisho vya Taifa jana mjini Zanzibar. Mashauzi ni miongoni mwa wananchi kutoka Tanzania Bara waliopewa vitambulisho vyao katika hafla ya utoaji wa Vitambulisho vya Taifa,kwa mara ya kwanza kwa Upande wa Zanzibar,hafla iliyofanyika katika viwanja vya Baraza la Wawakilishi Chukwani Nje ya Mji wa Zanzibar. Picha na Ramadhan Othman,Ikulu.

Saturday, February 2, 2013

MUME WANGU ALININYANYASA SANA-SALHA



MWIMBAJI nyota wa kikundi cha taarab cha Dar Modern, Salha Abdalla
amesema moja ya sababu kubwa iliyomfanya aachane na mumewe ni wivu
wa kupindukia.
Akihojiwa katika kipindi cha Mitikisiko ya Pwani, kilichorushwa
hewani na kituo cha redio cha Times FM wiki hii, Salha alisema wivu
aliokuwa nao mumewe, ulisababisha aamini kila alichoelezwa, hata
kama ni cha uongo.
Akitoa mfano, alisema wakati aliposafiri na kikundi chake kwenda
mikoa ya kusini, mumewe alipelekewa maneno ya uongo kwamba alikuwa
na uhusiano wa kimapenzi na msanii mmoja wa kikundi hicho na
akaamini.
Anasema alishangaa wakati wakiwa kwenye ziara hiyo, mumewe alikuwa
akimpigia simu na kumuuliza iwapo amerudiana na kijana huyo, lakini
alikuwa akimkatalia katakata.
"Ni kweli huyo mwanaume alikuwa mpenzi wangi kabla sijaolewa,
lakini wakati tulipokuwa safarini, sikuwahi kuhusiana naye kwa
lolote. Isitoshe alikuwa ameshaoa nami nimeolewa,"alisema Salha.
Aliongeza kuwa, baada ya kurejea kutoka katika ziara yao, mumewe
akaanza kumfanyia vituko nyumbani, ikiwa ni pamoja na kutomuachia
pesa ya matumizi wala kuzungumza naye.
Anasema kila alipomuuliza kulikoni, mumewe alionekana kuwa na
hasira na kuondoka nyumbani alfajiri na kurudi usiku wa manane.
Salha anasema baada ya kuona maji yamemfika shingoni, aliamua
kutengana na mumewe, lakini jambo la kushangaza, wiki zake waliamua
kumpokonya vitu vyote vya nyumbani, hata alivyotunzwa kwenye
sherehe ya kitchen party.
Anasema mmoja wa wifi zake alikuwa akiwapigia simu shoga zake
kuwauliza vitu walivyomtunza wifi yake na alipotajiwa, alimtaka
Salma aviache.
Kwa mujibu wa Salha, kilichokuja kumshtua zaidi ni kuona mumewe
akianzisha uhusiano wa kimapenzi na binamu yake wa kike, ambao hata
hivyo alisema ulidumu kwa siku chache.
"Kuna wakati alinifuata na kuniomba turudiane, lakini nilimkatalia
kwa sababu alishanidhalilisha sana, ikiwa ni pamoja na kunitoa
magazetini, hivyo nisingeweza kurudiana naye,"alisema Salha.
Mwanadada huyo, ambaye kwa sasa anatamba kwa kibao chake cha
Ninauvua ushoga, alisema kwa sasa anaye mpenzi mwingine na
wanatarajia kufunga ndoa hivi karibuni.