KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Thursday, March 7, 2013

SIJAITOSA MASHAUZI CLASSIC-THABITI


MSANII nyota wa muziki wa taarab nchini, Thabit Abdul amesema uamuzi wake wa kujiunga na kikundi cha taarab cha Five Stars hauna maana kwamba amekitosa kikundi chake cha Mashauzi Classic.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Thabiti alisema amejiunga na Five Stars kwa makubaliano maalumu na kwamba bado ataendelea kuitumikia Mashauzi Classic.
Thabit, ambaye ni mmoja wa wapiga vinanda mahiri nchini alisema, uongozi wa Five Stars umemruhusu kufanya maonyesho na kikundi cha Mashauzi Classis kila atakapokuwa na nafasi.
Alisema kwa sasa yeye si msanii wa kupiga muziki jukwaani kwa muda mrefu kwa sababu kazi yake kubwa ni kutunga, kutengeneza muziki na kupiga ala.
"Katika kikundi cha Mashauzi Classic, sina kawaida ya kupiga nyimbo nyingi stejini. Naweza kupiga wimbo mmoja ama mbili tu kwa sababu wapo vijana wanaofanya kazi hiyo,"alisema.
Alipoulizwa atawezaje kuvitumikia vikundi vyote viwili iwapo vitakuwa na maonyesho kwa wakati mmoja, Thabit alisema kikundi chake cha kazini ni Five Stars.
"Inapotokea hivyo, lazima nikitumikie kikundi cha Five Stars, ambacho nina mkataba nacho,"alisisitiza.
Thabit ni mmoja wa wakurugenzi wa Mashauzi Classic, kinachoongozwa na mwimbaji machachari wa kike, Isha Mashauzi.
Hata hivyo, msanii huyo wiki iliyopita alitangaza kujiunga na Five Stars, ambacho kimesukwa upya baada ya kupata uongozi mpya. Wasanii wengine waliojiunga na kikundi hicho ni Mwanahawa Ally, Sabah Salum, Hammer Q, Maua Tego na Mosi Suleiman.

No comments:

Post a Comment