KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Thursday, March 7, 2013

ALLY STAR AVUNJA UKIMYA



BAADA ya ukimya wa muda mrefu, mwimbaji taarab mkongwe nchini, Ally Hemed Star ameibuka na kibao kipya kinachokwenda kwa jina la Mvuvi Kinda.

Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Ally alisema amekirekodi kibao hicho kwa mtindo wa zing zong, nje ya kundi lake la Tanzania One Theatre (TOT-Plus).

Ally alisema kibao hicho kitakuwemo kwenye albamu yake binafsi, anayotarajia kuizindua hivi karibuni, ambayo ameirekodi kwa mtindo huo.

Alisema anaushukuru uongozi wa TOT Plus kwa kumruhusu kurekodi nyimbo zake binafsi kwa lengo la kujiongezea mapato.

Mkongwe huyo wa taaab alisema, muziki huo kwa sasa unalipa, tofauti na miaka ya nyumba ndio sababu si rahisi kwa msanii kutunga wimbo na kumpa msanii mwingine auimbe.

"Enzi zetu, msanii akitunga wimbo, alikuwa anafikiria ampe nani aimbe na atampatia mwimbaji, ambaye anaendana na wimbo huo kutokana na maudhui yake,"alisema.

"Lakini siku hizi, mtu akitunga wimbo mzuri, hataka kumpa mwingine kwa hofu ya kumpatia sifa na umaarufu,"aliongeza.

Ally alisema kutokana na muziki wa taarab kuwa na malipo mazuri hivi sasa, kila msanii anataka kutoka kivyake kwa lengo la kujiongezea mapato.

Ally alianza kupata umaarufu katika taarab wakati alipokuwa akiimbia kikundi cha Bima Modern Taarab kabla ya kutua Muungano Cultural Troupe na baadaye TOT Plus.

No comments:

Post a Comment