KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Monday, January 20, 2014

JAHAZI MODERN TAARAB YAPAGAWISHA MASHABIKI DAR LIVE

Mwimbaji na kiongozi wa kundi la Jahazi Modern Taarab akiwapagawisha mashabiki wakati wa onyesho hilo.
Mzee Yussuf na wacheza shoo wa Jahazi wakiwajibika jukwaani
 
 
Mwimbaji wa kundi la Jahazi, Leila Rashid akiwajibika jukwaani. Leila ni mke wa Mzee Yussuf

Mashabiki wa Jahazi wakijimwayamwaya wakati wa onyesho hilo

Mpiga kinanda Chid Boy akifanya vitu vyake

Mashabiki hawa walishindwa kuvumilia, walipandwa midadi na kupagawishwa na muziki wa Jahazi. (Picha zote na Mussa Mnally wa Global Publishers)

Thursday, January 9, 2014

JAHAZI YAFAFANUA SABABU ZA KUPELEKA UZINDUZI MOROGORO



KIKUNDI cha taarab cha Jahazi kimefafanua kuwa, kimetoa ufafanuzi
kuhusu uamuzi wake wa kuuchagua mkoa wa Morogoro kuwa mwenyeji
wa utambulisho wa nyimbo zake mpya.
Taarifa iliyotolewa na kikundi hicho wiki hii imeeleza kuwa, onyesho la
utambulisho wa nyimbo hizo, zitakazokuwemo kwenye albamu mpya,
litafanyika Januari 31 mwaka huu kwenye ukumbi wa Tanzanite Complex.
Mmoja wa viongozi wa Jahazi, Mohamed Mauji amesema wameamua
kuuchagua mji wa Morogoro kwa vile wanao mashabiki wengi huko.
Mauji, ambaye ni mpiga gita mahiri la solo, amesema mji wa Morogoro ni
ngome yao ya pili kwa ukubwa baada ya Dar es Salaam.
"Mara zote Jahazi imekuwa ikitambulisha nyimbo zake mpya Dar es
Salaam, na baadaye kuzitambulisha mikoani, lakini safari hii tumeamua
kuanzia Morogoro,"alisema.

Monday, December 23, 2013

DAR MODERN TAARAB KUZINDUA UKUMBI WAKE


KIKUNDI cha muziki wa taarab cha Dar Modern kinatarajia kuzindua ukumbi wake mpya wa burudani hivi karibuni.

Habari za uhakika kutoka ndani ya kikundi hicho zimeeleza kuwa, ukumbi huo umejengwa katika maeneo ya Magomeni, Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa habari hizo, uzinduzi wa ukumbi huo utakwenda sambamba na onyesho kabambe litakalofanywa na kikundi hicho.

Wednesday, November 6, 2013

VIKUNDI VYA TAARAB VYAUNDA UMOJA



HATIMAYE wasanii na viongozi wa vikundi vya taarab nchini, wameamua kuanzisha
umoja kwa lengo la kuzungumzia matatizo yao.

Lengo lingine la kuanzishwa kwa umoja huo ni kutetea maslahi yao na kupanga
mikakati ya kupanua soko la muziki huo.

Mkurugenzi wa kundi la East African Melody, Ashraf Mohamed amesema
wanatarajia kukutana hivi karibuni kuzungumzia matatizo yao.

Ashraf alisema wamefikia uamuzi huo baada ya kubaini kuwa, vikundi vyao
vimekuwa vikitumika kuwanufaisha watu wengine.

Amesema wakati wasanii wamekuwa wakiumia vichwa kutunga, kuimba na kupiga
nyimbo nyingi za taarabu, wanaonufaika ni wajanja wengine.

"Tunadhani huu ni  wakati wa bendi za taarab kujiendesha kibiashara kwani makosa
tunayoyafanya sisi viongozi, yanawaumiza sana wasanii wetu, hivyo ni bora tuamke
ili tupange mambo yetu kwa pamoja,"amesema.

Kiongozi huyo amesema japokuwa wamechelewa kuchukua uamuzi huo, lakini
wanao muda wa kutosha wa kuweza kurekebisha mwenendo na mwelekeo wao.

FIVE STARS SASA KUITWA VIP MODERN TAARAB



UONGOZI wa kikundi cha taarab cha Five Stars, umeamua kubadili jina la kundi hilo
na kujiita VIP Modern Taarab.

Habari kutoka ndani ya kundi hilo zimeeleza kuwa, uamuzi huo umelenga kubadili
mwelekeo na kukifanya kikundi hicho kiwe na mwelekeo mpya.

Hata hivyo, viongozi wa kundi hilo hawakuwa tayari kusema lolote kuhusu uamuzi
huo kwa vile jambo hilo limefanywa kuwa siri kubwa.

Lakini habari za uhakika zimeeleza kuwa, tayari uongozi umeshalipitisha jina hilo na
baadhi ya wadau wa taarab wamelisifu kwa madai kuwa ni zuri.

Kundi la Five Stars lilijipatia sifa kubwa wakati lilipoanzishwa kutokana na kuibuka na
vibao vyenye mvuto, ambavyo viliwapa homa viongozi wa vikundi vingine.

Thursday, October 24, 2013

KHADIJA KOPA: NARUDI UPYA NA MAMBO MAPYA



HATIMAYE mwimbaji nyota wa nyimbo za muziki wa taarab nchini, Khadija Omar Kopa amemaliza eda na anatarajiwa kurudi ulingoni Oktoba 30 mwaka huu.

Khadija, ambaye alifiwa na mumewe Juni mwaka huu, alimaliza eda wiki iliyopita nyumbani kwa mumewe, Bagamoyo mkoani Pwani.

Mwanamama huyo kwa sasa amerejea nyumbani kwake Mwananyamala, Dar es Salaam, ambako ndiko alikokuwa akiishi kabla ya kuolewa.

Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Khadija alisema amealikwa kufanya onyesho maalumu Oktoba 30 mwaka huu kwenye ukumbi wa Villa Park ulioko Mwanza.

Khadija alisema baada ya onyesho hilo, atapanda tena stejini Novemba 3 mwaka huu katika onyesho litakalofanyika kwenye ukumbi wa Dar Live ulioko Mbagala mjini Dar es Salaam.

Alisema baadhi ya mashabiki wake wameandaa onyesho la Dar Live kwa lengo la kumchangia kutokana na msiba mzito alioupata wa kufiwa na mumewe.

Mume wa msanii huyo, Jaffari Ali Yusuf alifariki dunia nyumbani kwake Bagamoyo baada ya kuugua kwa muda mfupi na kuzikwa huko huko.

Kutokana na kifo hicho cha mumewe, Khadija alilazimika kuacha kufanya maonyesho ya taarab ili kukaa eda kwa miezi minne kwa mujibu wa taratibu za kisheria za kiislamu.

Khadija amewashukuru wakazi wa Bagamoyo kwa kumpa ushirikiano wa hali ya juu katika muda wote aliokuwa akiishi na mumewe katika wilaya hiyo ya kihistoria.

Malkia huyo wa mipasho alisema, baada ya kufiwa na mumewe, amegundua kwamba anapendwa na watu wengi tofauti na alivyokuwa akifikiria.

Khadija alisema kipindi chote alichokuwa kwenye matatizo, alishangazwa na ukaribu ulioonyweshwa na watu, ambao hakuwatarajia na ameijua nafasi yake kwenye jamii.

 “Nimesaidiwa na asasi mbalimbali, vikundi pamoja na watu wengi na wengine walikuwa wakiniambia nikitaka msaada, niwapigie ingawa sijafanya hivyo. Nimefarijika sana kuona napendwa kiasi hiki,” alisema mwanamama huyo, ambaye alimaliza eda Oktoba 16, mwaka huu.

Alisema itamchukua muda kidogo kuweza kupanda tena jukwaani kutokana na hali aliyonayo na kuongeza kuwa, anataka atakapotoka, aonekane mtu mpya na mwenye mambo mapya.

Kwa mujibu wa Khadija, katika onyesho lake la kwanza, anatarajia kutoka na wimbo mpya, unaojulikana kwa jina la Mwanamke kujiamini.

Alisema alitunga wimbo huo kabla ya kifo cha mumewe, lakini alichelewa kuutoa kutokana na kutingwa na mambo mengi.

"Nataka kwanza nitulize akili yangu. Namuomba Mungu anirejeshee nguvu upya ili nikitoka, nitoke kivingine,"alisema mwimbaji huyo wa kundi la Tanzania One Theatre (TOT).

Khadija, ambaye ni mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM alisema, baada ya onyesho la Dar Live, anatarajia kufanya onyesho lingine la kuwaaga wakazi wa Bagamoyo.

"Onyesho hili litakuwa maalumu kwa ajili ya kuwaaga wakazi wa Bagamoyo kutokana na kuishi nao vizuri muda wote niliokuwepo hapa na mume wangu,"alisema mwanamama huyo.

Khadija alisema anamshukuru Mungu kuona kuwa, bado yuko imara na amewaomba mashabiki wake, wamuombee dua ili aweze kurudi upya.

"Hii ni kazi yangu inayoendesha maisha yangu na ya familia yangu, nataka nitakaporudi ulingoni, niwe mpya, nitoke angalau na nyimbo mbili mpya, nawaomba mashabiki wangu waniombee kwa Mungu ili nirudi upya,"alisema.

Khadija alisema katika maonyesho hayo, anatarajia kuimba nyimbo zake mpya na za zamani na kuwaomba mashabiki wampokee kwa mikono miwili.

"Unajua ukiwa kwenye eda, unarudi nyuma sana, hivyo nahitaji muda kidogo wa kupanga mambo yangu upya ili nijue nitatoka vipi,"alisema mwimbaji huyo, ambaye aliwahi kung'ara kwa vibao vya Daktari, Wahoi na Kadandie wakati alipokuwa kikundi cha Culture cha Zanzibar.


Sunday, September 29, 2013

MWASITI AJIENGUA TOT PLUS



Mwasiti Suleiman (kulia) akiwa na waimbaji wenzake wa TOT katika moja ya maonyesho ya kikundi hicho.

MWIMBAJI Mwasiti Suleiman wa kikundi cha taarab cha Tanzania One Theatre (TOT Plus) ameamua kujiengua katika kikundi hicho.

Mwasiti amesema mjini Dar es Salaam leo kuwa, ameamua kujiengua TOT Plus kwa sababu ya maslahi duni.

Amesema amekuwa akifanyakazi katika kikundi hicho kwa zaidi ya miaka tisa na kuongeza kuwa, hakuwahi kuajiriwa zaidi ya kufanyakazi kama kibarua.

Amesema katika miaka miwili ya kwanza, hakuwa akilipwa chochote na kwamba katika miaka saba iliyofuata, alikuwa akilipwa posho.

Mwasiti amesema kwa sasa ameamua kufanyakazi katika kampuni moja ya Wakorea, ambayo hakutaka kuitaja, lakini pia amekuwa akijihusisha na muziki huo katika vikundi vya mitaani.

Mwanadada huyo amesema haoni tofauti yoyote katika maisha yake ya sasa na wakati alipokuwa akifanyakazi TOT Plus na kwamba muziki haikuwa ajira pekee ya kuendesha maisha yake.

"Nilipo naweza hata kuuza vitumbua au maandazi kwa sababu zote ni kazi. Kila siku tunapishana na akina mama wakifanyakazi mbalimbali na wanaishi,"amesema mwanamama huyo mwenye mwanya wa kuvutia.

Alisema hakuwahi kugombana na mtu yoyote kwa kipindi chote alichokuwa TOT Plus na kwamba aliwaaga viongozi wake huku akiwaeleza wazi kwamba maslahi duni ndiyo yaliyomkimbiza.
Amesema anaweza kuwa tayari kurudi katika kikundi hicho iwapo tu atahakikishiwa ajira na maslahi mazuri.

Mwanadada huyo amesema pia kuwa, yupo tayari kujiunga na kikundi kingine cha taarab iwapo kitamuhakikishia ajira na maslahi mazuri.

Friday, September 27, 2013

MZEE YUSUPH KUSTAAFU MUZIKI 2015


MWIMBAJI nyota wa muziki wa taarab nchini, Mzee Yusuph amesema anatarajia kustaafu kazi hiyo katika kipindi cha miaka miwili ijayo.

Mzee, ambaye ni kiongozi wa kikundi cha Jahazi. amesema uamuzi wake huo umelenga kuwapa nafasi vijana kuonyesha vipaji vyao.

"Ni vigumu sana kuacha muziki wakati kikundi chako kipo juu, lakini kwa kuwa nimeshaamua, lazima nitekeleze hilo,"amesema Mzee alipozungumza na blogu ya

"Sina muda mrefu mbele, nitaweka kipaza sauti pembeni ili kuwapisha vijana waendeleze tasnia hii,"aliongeza.

Mtunzi na mwimbaji huyo mwenye sauti yenye mvuto, amesema uamuzi wake huo unaweza kuwaumiza mashabiki wake, lakini hana lingine la kufanya zaidi ya kuutekeleza.

"Kwangu mimi ni maamuzi magumu sana kwa vile nitakiacha kitu ninachokipenda na mashabiki wamenizoea, lakini itabidi wakubaliane na maamuzi haya,"alisema mwimbaji huyo, ambaye pia amepachikwa jina la Mfalme.

Kwa mujibu wa msanii huyo, baada ya kustaafu muziki, atalazimika kukivunja kikundi chake cha Jahazi na kumpatia kila msanii haki anayostahili kwa ajili ya kuendeleza maisha yake.

"Ningependa wasanii nitakaowaacha, watafute bendi zingine za kufanyakazi kwa kipindi hicho ili waendelee kuimba na kukuza zaidi vipaji vyao,"alisisitiza.

THABITI ABDUL AMWACHA SOLEMBA ISHA MASHAUZI


MKURUGENZI msaidizi wa kikundi cha taarab cha Mashauzi Classic, Thabiti Abdul amejiengua katika nafasi hiyo.

Habari za uhakika kutoka ndani ya kundi hilo zimeeleza kuwa, Thabiti ameshawasilisha barua ya kujitoa kwenye  kundi hilo kwa mkurugenzi wake, Isha Mashauzi.

Hata hivyo, hakuna taarifa rasmi iliyotolewa na Abdul au Isha kuhusu uamuzi wake huo.

Thabiti ni mmoja wa wasanii wanaounda kundi la Five Stars Modern Taarab, lakini amekuwa akishiriki mara kwa mara kwenye maonyesho ya Mashauzi Classic.

Hivi karibuni, Isha alikaririwa akisema kuwa, Thabiti bado yupo kwenye kundi hilo na amekuwa akishiriki kwenye maonyesho mbalimbali.

Habari kamili kuhusu uamuzi huu utazipata hivi karibuni kupitia kwenye blogu yako ya Rusha Roho.

ISHA: SIPENDI KUUMIZWA KIMAPENZI


KIONGOZI wa kikundi cha muziki wa taarab cha Mashauzi Classic, Isha Mashauzi amesema kamwe katika maisha yake hapendi kuumizwa kimapenzi na mwanaume.

Isha amesema anapoachana na mwanaume, huwa hageuki nyuma na kwamba mapenzi kwake ni kitu cha kupita.

"Nikiacha nimeacha, sipendi kuumizwa, kazi yangu mwenyewe inaumiza,"alisema Isha alipokuwa akihojiwa katika kipindi cha Ng'aring'ari kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha Clouds TV mwishoni mwa wiki iliyopita.

Isha amesema amewahi kutongozwa na wanaume wengi, lakini kutokana na msimamo alionao kimapenzi, wamebaki kuwa rafiki zake baada ya kuwaeleza ukweli wa mambo.

"Wapo zaidi ya wanaume wanne, ambao walinitongoza na kunitaka kimapenzi, lakini niliwaeleza wazi kwamba, kwa vile kila mmoja ana mkewe nyumbani, siwezi kujihusisha nao katika suala hilo. Hivi sasa ni rafiki zangu wakubwa, huwezi kuamini,"alisema.

Hata hivyo, Isha ametahadharisha kuwa, mwanamke anapoamua kumtolea nje mwanaume, anapaswa kuwa makini ili kuepuka kujiingiza katika matatizo.

Alisema wapo wanaume wanaopenda vibaya na wanaoweza kufanya lolote pale wanapokataliwa kimapenzi, ikiwa ni pamoja na kuua ama kujiua.

"Hata kama humpendi, mchukulie taratibu, usimweleze kwa pupa, wewe ni mwanadamu, siyo ng'ombe, hujui anakupenda vipi,"alisema mwanamama huyo, ambaye alianza kupata umaarufu katika muziki wa taarab alipokuwa kundi la Jahazi.

Isha amekiri kuwa, aliwahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi na Jumanne Tevez, ambaye alipiga naye picha za video ya wimbo wake wa Nakupenda kwa dhati, lakini hawakuwahi kupata mtoto.

Anasema anajuta kumtambulisha Tevez kwa watu wengine kwa sababu baadhi yao walitumia nafasi hiyo kumtaka kimapenzi kwa lengo la kumkomoa.

Licha ya kuachana na Tevez baada ya mpenzi wake huyo wa zamani kuoa mwanamke mwingine, Isha amesema bado wanaendelea kuwasiliana na kuwa na urafiki wa kawaida.

"Hata mkewe tuna uhusiano mzuri na wakati mwingine huwa tunapigiana simu kujulikana hali, namwita wifi naye ananiita wifi,"alisema Isha.

Isha amesema katika maisha yake, kamwe hawezi kupigana na mwanamke mwenzake kwa ajili ya kugombania mapenzi. Alisema tabia hiyo imepitwa na wakati.

Ametoa mwito kwa wanawake wa Kitanzania kujenga utamaduni wa  kupendana na kukosoana badala ya kujengeana chuki bila ya sababu za msingi.

Amesema inapendeza mwanamke anapomuonea mwenzake wivu wa kimaendeleo kwa kufanya kile kilichomvutia kutoka kwa mwenzake hata kama atakuwa anamuiga.

Isha amesema licha ya mkurugenzi mwenzake wa Mashauzi Classic, Thabiti Abdul kuhamia kundi la Five Stars, bado amekuwa akiendelea kufanya maonyesho na kundi hilo.

"Thabiti bado tuko naye, anakuja mazoezini, anapiga kinanda na gita kwenye maonyesho, kwa ujumla bado tuko naye,"alisema.

Isha amesema kwa sasa kundi lake la Mashauzi Classic linajiandaa kuipua albamu mpya, itakayokuwa na nyimbo sita. Amesema albamu hiyo itajulikana kwa jina la Asiyekujua hakuthamini.
Albamu hiyo itakuwa ya pili kwa Mashauzi Classic tangu kundi hilo lilipoanzishwa miaka miwili iliyopita.

Albamu ya kwanza inajulikana kwa jina la Si bure una mapungufu, iliyofuatiwa na Viwavi Jeshi. Albamu hizo mbili zilikuwa na nyimbo nne kila moja.

Tuesday, September 17, 2013

MWIMBAJI AHMED MGENI WA ZANZIBAR STARS AFARIKI DUNIA



MWIMBAJI  wa kikundi cha taarabu cha Zanzibar Stars, Ahmed Mgeni, amefariki dunia.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa mmoja wa ndugu wa marehemu, alisema Mgeni alifariki jana saa kumi na mbili asubuhi katika hospitali ya Mnazi Mmoja mjini Zanzibar.

Alisema marehemu alikuwa akisumbuliwa na kichwa na alianza kuugua tangu mwezi wa nne mwaka huu lakini baadae alipata nafuu na kuruhusiwa kurudi nyumbani.

Alisema, hali ya marehemu ilibadilika ghafla juzi na kukimbizwa hosipitali kabla ya mauti kumfika na kusema alizikwa jana katika makaburi ya Mwanakwerekwe, Zanzibar.

Akiwa na kundi la Zanzibar Stars, marehemu aliwahi kutamba na nyimbo mbalimbali na mapema mwaka huu alianzisha kundi lake la muziki wa taarabu lililoitwa Nia Njema.

Thursday, August 8, 2013

FIVE STARS, MASHAUZI CLASSIC, DAR MODERN TAARAB KUTOA BURUDANI IDD EL FITR


Mwanahawa Ally-Five Stars
Isha Mashauzi-Mashauzi Classic
Mwimbaji wa Dar Modern Taarab

KUMBI mbalimbali za burudani za mjini Dar es Salaam kesho na keshokutwa zinatarajiwa kuwaka moto wakati vikundi mbalimbali vya taarab vitakapofanya maonyesho ya kusherehekea sikukuu ya Idd el Fitr.

Kikundi cha taarab cha Five Stars kitasherehekea sikukuu hiyo siku ya Idd Mosi kwa kufanya onyesho katika kitongoji cha Kigogo Fresh kilichopo Pugu, Ilala, Dar es Salaam.

Kiongozi wa kundi hilo, Ally J alisema juzi kuwa, siku ya Idd Pili, kundi hilo litatoa burudani kwenye ukumbi wa Roshi Garden ulioko Mwandege, Mbagala, Dar es Salaam wakati siku ya Idd Tatu itahanikiza maraha Kibiti, Rufiji mkoani Pwani.

Ally J alisema katika maonyesho hayo, kundi hilo litatambulisha kibao chake kipya kinachokwenda kwa jina la Habari ya mjini.

Kundi la muziki wa taarab la Dar Modern litasherehekea siku ya Idd Mosi kwa kushusha burudani nzito kwenye kiota kipya cha maraha kinachojulikana kwa jina la Serengeti Golden Paradise Resort, Mbagala, Mbande, Dar es Salaam.

Meneja wa hoteli hiyo, Wambura  Sungura alisema juzi kuwa, kundi hilo limeahidi kuporomosha vibao vyake vipya zaidi ya vitano, vitakavyokuwemo kwenye albamu yao mpya.

Sungura amewataka wakazi wa Mbagala na vitongoji vya jirani kufika kwa wingi kwenye ukumbi huo ili kupata burudani adhimu kutoka katika kundi hilo, ambalo lilikuwa kimya kwa zaidi ya miezi miwili.

Kwa mujibu wa Sungura, kabla ya burudani hiyo, kutakuwepo na onyesho ya utangulizi la muziki wa disco kwa ajili ya watoto. Alisema onyesho hilo litaanza saa sita mchana na kuhitimishwa saa kumi na moja jioni.

Kundi la Mashauzi Classic linaloongozwa na Isha Mashauzi limeamua kukwea basi kwenda Morogoro kuwapa burudani ya kusherehekea sikukuu hiyo mashabiki wake katika kitongoji cha Mji Mpya.

Mashauzi alisema juzi kuwa, siku ya Idd Pili kundi hilo litahamishia burudani zake kwenye ukumbi wa City Pub mjini Mbeya wakati Iddi Tatu litamwaga lazi kwenye ukumbi wa Garden Park ulioko Mafinga mkoani Iringa.

Katika maonyesho hayo, Mashauzi alisema kundi hilo litatambulisha nyimbo zake nne mpya, zinazotarajiwa kuwemo kwenye albamu yao mpya, itakayokuwa na nyimbo sita.

Alizitaja nyimbo hizo, watunzi wakiwa kwenye mabano kuwa ni Asiyekujua hakuthamini (Isha na Saida), Bonge la bwana (Hashim Said), Ropokeni yanayowahusu (Saida) na Ni mapenzi tu (Zubeda Maliki).

Monday, August 5, 2013

AMIN-T MOTO BADO IPO HAI

MKURUGENZI wa kikundi cha taarab cha T Moto, Amin Salmin amesema kundi hilo bado lipo hai na limezidi kujiimarisha.

Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Salmin alisema wamepanga kuliimarisha kundi lao kwa kuongeza wasanii wengine sita kutoka makundi mbalimbali.

Salmin alisema wasanii hao watatoka katika vikundi vya Jahazi na Kings Modern Taarab, lakini hakuwa tayari kutaja majina yao.

Kwa mujibu wa Salmin, wasanii wanne watatoka Jahazi na wengine wawili kutoka Kings Modern Taarab.
Katika hatua nyingine, Mkurugenzi wa kundi la G5 taarab, Hamisi Slim amesema kundi lake lipo katika maandalizi ya kuipua nyimbo mpya nne.

Mbali na kupika nyimbo nne, Slim alisema kundi lake linatarajia kuendelea kujiimarisha kwa kuongeza wasanii wawili wapya. Hakuwa tayari kutaja majina yao.

Saturday, August 3, 2013

KHADIJA KOPA: BAADA YA KUFIWA NA MUME WANGU, NIMEGUNDUA NAPENDWA

MALKIA wa Mipasho Afrika Mashariki, Khadija Kopa amesema baada ya kufiwa na mumewe kipenzi, Jafari Ally, amegundua kuwa anapendwa na watu wengi tofauti na alivyokuwa akifikiria.
 Akistorisha na mwandishi wetu, Khadija alisema kuwa kipindi alipokuwa kwenye matatizo alishangazwa na ukaribu ulioonyweshwa na watu hata ambao hakuwatarajia na ameijua nafasi yake kwenye jamii.

 “Nimesaidiwa na asasi mbalimbali, vikundi pamoja na watu wengi, huku wengine wakiniambia kuwa nikitaka msaada niwapigie ingawa sijafanya hivyo, nimefarijika sana kuona napenda kiasi hiki,” alisema mwanamama huyo ambaye anatarajia kumaliza eda Oktoba 16, mwaka huu kabla ya kurejea…