KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Thursday, February 4, 2016

MAJAZ MODERN TAARAB YAJA KWA KISHINDO


Majaz Modern Taarab ambayo imekarabatiwa upya, inakuja na kete yake ya pili, safari hii ikiwa ni zamu ya Hamuyawezi Kondo na wimbo “Mshamba Haishi Kujigamba”. 


Wimbo huu unakuja wiki chache baada ya bendi hiyo kuachia ngoma inayokwenda kwa jina la “Penzi halina makombo” ya kwake Ashura Machupa. 

Katika wimbo huu wa Hamuyawezi Kondo aliyetamba huko nyuma na nyimbo kama “Kalieni Viti” na “Mtu Mzima Ovyo”, utasikia solo la Kisolo na kinanda cha Kalikiti Moto huku bass likipigwa na Mussa Mipango. 

Ni kazi iliyorekodiwa katika studio za Sound Crafters chini ya producer Enrico.

KHADIJA KOPA APIGA MARUFUKU NYIMBO ZAKE KUIMBWA NA VIKUNDI VINGINE KWENYE MAONYESHO



Hatimaye Malkia wa mipasho Bi Khadija Kopa amepiga marufuku nyimbo zake kusikika kwenye bendi nyingine mbali na bendi yake ya Ogopa Kopa. 

Khadija Kopa alifunguka hilo Jumamosi usiku kwenye ukumbi wa Dar Live wakati akisindikiza onyesho la Jahazi Modern Taarab. 

Mara baada ya kupiga wimbo wake wa “Mama Mukubwa” Khadija Kopa akasema: “Huu ni wimbo wangu unaopatikana Ogopa Kopa na ni marufuku bendi nyingine kupiga nyimbo za Ogopa Kopa au nyimbo za Khadija Kopa.

 “Natangaza rasmi kuwa ni makosa na sitaruhusu nyimbo zangu pamoja na za Ogopa Kopa kwa ujumla wake kupigwa na bendi nyingine, ni marufuku”. 

Tamko la Khadija Kopa linafuatia malalamiko yake ya muda mrefu juu ya bendi zinazopiga muziki wa kunakili (Copy) kutumia kibiashara nyimbo za bendi nyingine. 

Wasanii wengi wanaothiriwa na hali hiyo ya nyimbo zao kutumika ovyo wamekuwa wakisema ni afadhali bendi hizo za ‘copy’ zipige nyimbo za bendi zilizokufa kuliko kupiga nyimbo za bendi ambazo bado ziko hai. 

Bendi zingine ambazo zimeshatangaza vita na makundi hayo ya kupiga nyimbo za kunakili ni Jahazi Modern Taarab na Mashauzi Classic.